Habari za Punde

KAMWELWE ATENGUA NAFASI ZA MAMENEJA WA TANROADS MKOA WA PWANI NA LINDI

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), mara baada ya kukagua ubovu wa barabara ya Nangurukuru hadi Mbwemkuru (km 155), iliyopo katika Barabara Kuu ya Dar es Salaam hadi Lindi (km 452).
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, akitoka kukagua mzani wa Nangurukuru uliopo mkoani Lindi wakati alipowasili mkoani humo kwa ajili ya utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli  baada ya kukagua barabara ya kutokea Lindi hadi Dar es Salaam na kutoridhishwa na hali ya miundombinu ya barabara hiyo.
Naibu waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa,  akitoa maelekezo kwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anayeshughulikia Sekta ya Ujenzi Arch. Elius Mwakalinga, kuhusu ukarabati wa sehemu iliyoharibiwa na malori ya mizigo ya mawe katika barabara ya Mtwara - Lindi - Dar es Salaam.
Viongozi na Wataalam kutoka wizara ya Ujenzi,uchukuzi na mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), wakisikiliza maelezo kutoka kwa wasafirishaji wa mawe katika eneo la Kilanjelanje mkoani Lindi tayari kwaajili ya kusafirishwa kuelekea jijini Dar es Salaam.

Na. Deniza Cyprian

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe, ametengua nafasi ya Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), mkoa wa Pwani na Lindi kutokana na kutoridhishwa na usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi ya barabara ya Dar es Salaam - Kilwa - Lindi hadi Mingoyo yenye urefu takriban kilometa 450.

Aidha, ameagiza Mameneja wapya wa mikoa hiyo na mameneja wa mikoa mingine kuhakikisha wanaziba mashimo yote yaliyopo kwenye barabara zao ndani ya saa 48 kuanzia muda wa shimo hilo linapojitokeza.

Mhandisi Kamwelwe, ametoa agizo hilo akiwa mkoani Lindi  ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, baada ya kutoridhishwa na hali ya miundombinu ya barabara kuanzia Nangurukuru hadi Mbwemkuru wakati alipoikagua barabara hiyo siku chache zilizopita ambapo pamoja na mambo mengine amesema kuwa hadi sasa bilioni 10 zimeshatengwa kwa ajili ya zoezi la kuziba mashimo yote kabla hayajaleta athari zingine.

"Nimetengua nafasi za watendaji hawa wawili kwa makosa yaliyojitokeza katika barabara hizi zinazounganisha mkoa kwa mkoa na hadi kufikia mwishoni mwa mwezi  huu nahitaji wananchi wawe wanapita salama katika barabara hii", amesema Waziri Kamwelwe.

Waziri huyo ameeleza kuwa sehemu kubwa ya barabara iliyoathirika ni kuanzia eneo la Muhoro mkoani Pwani hadi Mbwemkuru  mkoani Lindi yenye jumla ya urefu wa kilometa 190 na zote zipo katika utaratibu wa kuanza kukarabatiwa.

Waziri Kamwelwe amebainisha kuwa ataendelea kusimamia muongozo wake alioutoa mwezi Juni mwaka huu kuwa barabara yoyote yenye mashimo katika barabara kuu na za mikoa basi huyo Mhandisi wa Mkoa ajiondoe mapema kwani hayuko tayari kufanya kazi na wataalamu wasio weledi na kushindwa kusimamia rasilimali fedha na watu vizuri.

Ameongeza kuwa hadi sasa Serikali imeshatoa kiasi cha fedha bilioni 40 kwa ajili ya matengenezo ya barabara zote nchini zilizoathriwa na maji ya mvua.

"Fedha zipo sasa sitarajii kuona barabara yoyote hapa nchini ina mashimo, huyo Meneja ambaye barabara zake zina mashimo tutamalizana hapo hapo", amesisitiza Mhandisi Kamwelwe.

Waziri Kamwelwe ameelezea umuhimu wa barabara hiyo kiuchumi  ambayo ilijengwa toka mwaka 2008  na kusema kuwa ongezeko la usafiri wa abiria na usafirishaji wa bidhaa, mazao na malighafi za viwandani katika kipindi cha miaka hii 12 ndiyo imetuonesha namna ya kujipanga upya katika ukarabati wa barabara hii.

"Tunaleta watalaamu katika barabara hii kwa ajili ya kuanza kusanifu upya na kuona kwanini imeharibika kabla ya wakati wake na maandalizi yanaendelea vizuri", amefafanua Waziri Kamwelwe.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri wa Ujenzi, Elias Kwandikwa akiongozana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Arch. Elius Mwakalinga, wameikagua pia sehemu ya barabara hiyo na kueleza  kuwa hatua za awali za ukarabati zimeanza  ambapo kazi hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, mwaka huu.

Naibu Waziri Kwandikwa amewataka wakandarasi watakaopewa kazi ya ukarabati wa barabara hiyo kukamilisha kabla ya kuanza kwa  mvua za vuli zinazotarajiwa kunyesha hivi karibuni kwani barabara hiyo ina mchango mkubwa sana wa kiuchumi na kijamii kwa wakazi wa Nyanda za Kusini.

Naye, Katibu Mkuu Arch. Elius Mwakalinga, amewahakikisha wakazi wa mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara kuwa maeneo ya barabara yaliyokuwa yameharibika yameanza kufanyiwa matengenezo kwa sababu asilimia 80 ya bajeti ya wizara imetengwa kwa ajili ya ukarabati wa barabara nchini.

“Sina mashaka na kazi ya ukarabati wa sehemu ya barabara hii kwa sababu fedha zipo  na mimi nipo eneo la tukio tangu Rais Magufuli alipotoa agizo la ukarabati wa barabara hiyo na hadi sasa maandalizi yanaendelea vizuri", alisisitiza Arch. Mwakalinga.

Barabara ya Dar es Salaam hadi Lindi inakarabatiwa kwa fedha za ndani na inatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba mwaka huu hii ikiwa ni hatua zili

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.