Habari za Punde

NAIBU WAZIRI WA MAJI KUWAPIGANIA WATAKAOSTAHILI KULIPWA FIDIA



MGOMBEA Ubunge wa jimbo la Pangani, ambaye pia ni naibu waziri wa maji Jumaa Aweso jana amerudisha fomu yake kugombea Ubunge kwa msimamizi wa uchaguzi ambaye ni Mkurugenzi Ndg.Isaya Mbenje.
Baada ya kukabidhi fomu yake, Ndg.Aweso alipata fursa ya kuongea na waandishi wa habari ambapo alisema kuwa endapo wananchi watampa ridhaa ya kuongoza jimbo hilo kwa miaka mingine mitano atahakikisha anamaliza kama sio kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya barabara na maji.
Pamoja na hilo Aweso aliwataka wanachama na wananchi kulinda amani na kudumisha umoja ndani na nje ya Chama ili kuweza kushinda kwa kishindo katika uchaguzi mkuu mwezi oktoba 2020 mwaka huu.
"Kikubwa ninachoweza kusema ni Wana Ccm tuungane na tuwe kitu kimoja ili tuweze kushinda kwa kishindo, kuna barabara ya Pangani - Tanga hadi Saadani tayari mkandarasi yuko kazini, nitaongea mengi nitakapoanza kampeni lakini kikubwa ni kuondoa changamoto hizo" alisema.

Na Hamida Kamchalla, PANGANI.
NAIBU Waziri wa maji ambaye pia ni Mgombea ubunge jimbo la Pangani Jumaa Aweso ameahidi kusimama kidete kuwapigania wananchi watakaopisha ujenzi wa barabara iliyoanza kujengwa kulipwa fidia zao mara tu atakapoingia madarakani kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Ahadi hiyo aliitoa jana mbele ya waandishi wa habari mara tu baada ya kukabidhi fomu kwa msimamizi wa uchaguzi ambaye ni mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Pangani Isaya Mbenje na kuulizwa kipaumbele chake baada ya kupata ridhaa ya wananchi kwa nafasi hiyo ya ubunge.

Aweso alisema kuwa atahakikisha anasimamia na kudumisha amani ya nchi ndani ya wilaya hiyo kwa kufanya kazi akishirikiana na wananchi ili kuleta maendeleo na kumuinga mkono rais John Magufuli na kuyasimamia yale yote aliyoyaanzisha likiwemo la kuwasimamia wananchi hao kulipwa fidia zao.

"Kubwa nitakalolifanya katika kipindi hiki ambacho nitaipeperusha bendera ya Ccm nitasimamia yale yote niliyoanzisha hasa katika ujenzi wa barabara ya Pangani - Tanga, Pangani- Bagamoyo, Saadani - Bagamoyo, tumeona ujenzi umeanza na mkandarasi yupo kazini" alisema.

"Pamoja na ujenzi wa barabara hiyo zipo athari ambazo zitawapitia wananchi ambao watapisha ujenzi huo, kikubwa nitakachofanya ni kuhakikisha wananchi wale wanalipwa fidia zao ili na wao waweze kufanya shuhuli nyingine za kimaendeleo" alisisitiza Aweso.

Aidha alisema kuwa atahakikisha mradi wa ujenzi huo unaleta mafanikio chanya kwa kuwahamasisha wananchi kutumia fursa hiyo ili kuchangia maendeleo ya uchumi na kuingiza kipato ndani ya wilaya na taifa kwa ujumla.

Aweso alifafanua kwamba mbali na ujenzi huo kuna mradi mkubwa wa maji kupitia mto Pangani ambao ukimalizika utaweza kuleta manufaa kwa wilaya tatu ndani ya mkoa wa Tanga ambao ulishaanza kuratibiwa na uko katika hatua za mwisho za kumpata mkandarasi kwa ajili ya makabidhiano.

"Tuna mradi mkubwa sana wa maji kupitia mto Pangani, maji ambayo yatatumika katika wilaya yetu ya Pangani, Muheza na Handeni, nikiwa mbunge mtarajiwa nitalisimamia hilo kuhakikisha mradi ule unaanza mara moja na maeneo hayo yote yanapata maji ili kukamilisha ahadi za rais" alisema.

Hata hivyo aliwataka wanachama wa Ccm wasikubali kufitinishwa ndani na nje ya chama chao na badala yake waendelee kushikamana kwa umoja wao na kufanya kampeni za kistaarabu ili kuendelea kuilinda amani yao kwani ndiyo silaha kubwa ya kujipatia ushindi.

"Mengi nitayasema nitakapoanza raami kampeni lakini kikubwa tutasimamia amani ya nchi, amani tutaipa kipaumbele kwa kufanya kampeni za kistaarabu na ninachoweza kusema kwa chama chetu, ushindi wetu unatokana na umoja na mshikamano wetu kwahiyo tuendelee kushikamana ili tuweze kishinda kwa kishindo, tusifitinishwe" aliongeza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.