Na.Mbaraka Kambona, Tanga
Mapato ya Halmashauri
ya Mkinga, Mkoani Tanga kupitia Sekta ya Uvuvi yamepanda kufikia shilingi
Milioni 96.6 mwaka 2019/ 2020 kufuatia mikakati
waliyoiweka dhidi ya Uvuvi haramu.
Mkurugenzi wa Halmashauri
ya Mkinga, Rashid Gembe wakati akiongea na timu ya Wataalamu kutoka Mradi wa Ulinzi
Shirikishi wa rasilimali za bahari kusini magharibi mwa bahari ya Hindi (SWIOfish)
ofisini kwake mwishoni mwa wiki alisema kuwa kabla ya mradi huo kuanza kuhamasisha
uvuvi endelevu na wenye tija, mwaka 2015/ 2016 Halmashauri ya Mkinga ilikusanya
kiasi cha shilingi Milioni 45.3 kutoka katika sekta ya Uvuvi.
Gembe aliwaeleza
wataalamu hao waliokwenda kufuatilia maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo
Wilayani humo kuwa mradi umechangia kwa kiasi kikubwa kukomeshwa kwa uvuvi
haramu hususani uvuvi wa kutumia mabomu na makokoro.
“Mradi wa SWIOfish
ulipoanza kufanya kazi hapa Wilayani kwetu mwaka 2016 ulianzisha Vikundi vya
Ulinzi Shirikishi wa Rasilimali za
Bahari (BMU) zipatazo 14 ambazo zimesaidia kutoa elimu ya ulinzi wa rasilimali
za uvuvi kwa wananchi ikiwemo kutunza mazingira ya fukwe za bahari”,alisema
Gembe
“Pamoja na kuimarisha
BMU hizo, pia iliimarisha Doria za Baharini na nchi kavu kwa lengo la kulinda
rasilimali za uvuvi, na nikiri kuwa Doria hizo zimesaidia kupungua kwa uvuvi
haramu na sasa mapato ya Halmashauri yameanza kupanda kwa sababu wavuvi sasa
wanafanya uvunaji endelevu wa rasilimali za uvuvi”,aliongeza Gembe
Kufuatia mafanikio
hayo, Gembe aliuomba mradi wa SWIOfish kuendelea kutoa elimu kwa wananchi
wanaoishi katika mwambao wa bahari wilayani humo ili rasilimali za uvuvi
zilizopo ziendelee kuwanufaisha waliopo na vizazi vijavyo.
Aidha, aliwasihi
wananchi wanaoishi katika mwambao wa bahari waliopata elimu hiyo ya utunzaji wa rasilimali za bahari
na uoto wake waendelee kuienzi elimu hiyo kwa kuisambaza kwa wengine ili
rasilimali hizo ziendelee kunufaisha jamii hizo na Taifa kwa ujumla.
“Niwatake wananchi
kuacha kukata mikoko na waendelee kuwa sehemu ya ulinzi wa rasilimali za uvuvi ili
ziendelee kuwa na tija kwa
jamii”,alisisitiza
Aliwakumbusha wananchi
wa Wilaya hiyo kuwa mapambano dhidi ya uvuvi haramu sio nguvu ya soda ni
mapambano endelevu na hawatakuwa na huruma na yeyote atakaye kwenda kinyume.
“Wananchi watambue kuwa
tunafanya haya kwa nia njema, sisi tutaondoka lakini hii nchi itaendelea
kuwepo, tufikirie Tanzania ya miaka 50 ijayo, tusiwe na mawazo ya kupata sasa
tu, huo utakuwa ubinafsi”,alifafanua Gembe
Mkurugenzi huyo aliushukuru mradi wa SWIOfish kwa kuwapatia vifaa mbalimbali ambavyo vimeweza kuisaidia halmashauri hiyo kuvitumia katika kulinda rasilimali za bahari.
No comments:
Post a Comment