NA SABIHA KHAMIS MAELEZO
Wizara ya Afya Zanzibar imewataka wanajamii kujitokeza kwa wingi katika zoezi la upimaji wa macho ili kujua afya zao na kupatiwa matibabu ya ugonjwa huo.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Hospital ya Mnazimmoja Mratibu wa Huduma ya Afya ya Macho Fatma Juma Omar amesema Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Tasisi binafsi ina mpango wa kuwapatia matibabu watu wenye matatizo ya macho Unguja na Pemba.
Amesema wananchi hawatakiwi kuogopa, kujificha wala kufuga maradhi bali wajitokeze kwa wingi katika kupima afya ya macho na kupatiwa matibabu kwani tatizo hili husababisha upofu.
“lengo kuu kuwapima na kuwapatia matibabu ya upasuaji kwa wale watakaogundulika na matatizo ya macho, huduma hio tunatoa bila ya malipo ili kusaidia wananchi kuondokana na tatizo hilo” alisema Mratibu.
Alieleza kuwa zoezi hilo litachukua siku tano lilianza tarehe 14 Novemba na kumalizika 18 Novemba ambalo lina lengo la kuwapa matibabu watu 150 lilianzia katika kijiji cha Tazari na kufanikiwa kupata wagonjwa wenye matatizo ya mtoto wa jicho.
Pia alisema kuwa huduma hizo zitaendelea tena mwezi ujao na wananchi wasiopungua 50 wanatarajiwa kupatiwa matibabu, kisiwani Pemba ambayo inatarajiwa kufanyika katika Hospital ya Abdalla Mzee Mkoani au Chakechake na kuwataka wananchi wajitokeze.
Baadhi ya wagonjwa walioshiriki katika zoezi hilo wametoa wito kwa wananchi kuacha kufuga maradhi na wajitokeze kwa wingi ili kupata matibabu na kuepukana na upofu unaotibika.
Aidha wamesema huduma zinazotolewa Hospitalini hapo ni muhimu na nzuri pia Madaktari wanawahudumia wagonjwa ipasavyo.
Wananchi wasiopungua 60 wamefanyiwa upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Mnazimmoja wakiwemo wanaume 40 na wanawake 20.
No comments:
Post a Comment