STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Dodoma
16.12.2020
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi ameapishwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Hamis Juma kuwa
Mjumbe wa Baraza la Mawaziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili aweze
kushiriki na kutekeleza vyema majukumu yake katika Baraza hilo.
Kiapo hicho kimeshuhudiwa na Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli.
Viongozi kadhaa walihudhuria hafla hiyo akiwemo
Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan,Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Majaliwa, Mwanasheria
Mkuu Adelardus Kilangi, Mawaziri, Katibu Mkuu Kiongozi John William Kijazi
pamoja na Manaibu Mawaziri na watendaji wengine wa Serikali.
Hafla hiyo imefanyika leo katika ukumbi
wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma ambapo wakati huo huo mara tu baada kiapo
hicho kikao cha Baraza la Mawaziri kilifunguliwa na Mwenyekiti wake Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli.
Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo
kumpongeza Rais Dk. Hussein Mwinyi kwa kula kiapo na kushiriki katika kikao
hicho cha ngazi ya Juu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aidha, Rais
Dk. Magufuli aliwapongeza Mawaziri wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
kuwa ni sehemu ya Baraza hilo la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kwa ushiriki wao katika kikao hicho pamoja na kuwapongeza Manaibu Mawaziri kwa
uteuzi walioupata ndani ya Serikali.
Mikutano ya
Baraza hilo huongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ndiye
anaekuwa Mwenyekiti wa vikao vya Baraza la Mawaziri.
Mara baada ya kiapo hicho Rais Dk.
Hussein Mwinyi alishiriki katika Kikao hicho cha kwanza katika kipindi cha pili
cha uongozi wa Awamu ya Tano ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.
John Pombe Magufuli ambaye ndiye aliyekuwa Mwenyekiti wa kikao.
Ushiriki wa
Rais Dk. Hussein Mwinyi unatokana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kifungu cha 54 Ibara ya kwanza ambayo inawataja Wajumbe wa Baraza la Mawaziri
kuwa ni Makamu wa Rais, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa mujibu wa
kifungu hicho cha 54 cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Baraza la
Mawaziri litakuwa ndicho chombo kikuu cha kumshauri Rais juu ya mambo yote
yanayohusika na utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba.
Sambamba na
hayo, kifungu hicho cha 54 cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kinaeleza
kwamba Baraza la Mawaziri litamsaidia Rais na kumshauri juu ya jambo lolote
litakalowasilishwa kwenye Baraza hilo kwa mujibu wa maagizo maalum au maagizo
ya jumla yatakayotolewa na Rais.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment