Bahati Habibu Maelezo Zanzibar 29/12/2020.
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Khamis Hamza Khamis (Chilo) amesema hajaridhishwa na matumizi ya fedha za ujenzi wa nyumba za askari kisiwani Pemba kwani gharama zilizotumika haziendani na ubora wa nyumba hizo.
Ameyasema hayo wakati alipotembelea mradi wa ujenzi wa nyumba za Polisi na askari wa Uhamiaji katika ziara ya siku mbili huko Mkoa wa Kaskazini Pemba ambao umegharimu zaidi ya shilingi milioni ishirini kwa kila nyumba.
Amesema kuwa thamani iliotumika katika ujenzi wa nyumba hizo ilitakiwa ziwe tayari kwa makazi lakini bado nyumba hizo haziwezi kukalika na gharama iliotumika ni kubwa.
“Ujenzi wa nyumba hizi kuanzia msingi hadi kuezekwa sijaona ubora wowote ambao umefanya zitumike milioni ishirini kiukweli sijaridhishwa na ujenzi huu hauna kiwango” alisema Naibu Waziri
Awali naibu waziri wa mambo ya ndani ya nchi alipokea taarifa ya mradi huo kutoka kwa Kamanda wa Polisi Wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Juma Sadi Khamis kuwa mradi wa nyumba hizo umegharimu shilingi million ishirini na mbili laki saba na elfu nane na mia mbili kwa kila nyumba
Hivyo Naibu Waziri huyo amevitaka vyombo vya Ulinzi na Usalama vilivyopo chini ya Wizara hiyo kutumia kwa umakini fedha za miradi mbalimbali inayotekelezwa na Taasisi hizo huku akiwaasa kuangalia thamani ya mradi husika.
Aidha naibu waziri huyo amesema wapo baadhi wa watu huitumia vibaya bandari ya Wete kwa kuingiza dawa za kulevya pamoja na bidhaa nyengine zisizo ruhusiwa nchini hivyo amevitaka vyombo vya ulinzi kulishughulikia tatizo hilo mara moja.
Pamoja na hayo alipata nafasi ya kuzungumza na wafanya biashara na wavuvi wa samaki katika pwani ya Shumba Mjini iliyopo Wilaya ya Micheweni ambapo wavuvi hao wameiomba Serikali kuwapelekea boti ya kuokolea wahanga wa ajali za majini pindi zinapotokea.
Akiendelea na mazungumzo hayo mwenyekiti wa wafanyabiashara hao ndugu Husein Rashid alimwambia naibu wazir kuwa jumla ya watu kumi wamepoteza maisha baada ya kuzama kutokana na kukosa vifaa vya kuokolea.
akijibu Naibu Waziri amewataka wafanya biashara hao kuwa wastahamilivu kwani Serekali inayoongozwa na Dkt Hussein Ali Mwinyi imekusudia kuzirasimisha Bandari zote bubu za Zanzibar kuwa Bandari rasmi.
No comments:
Post a Comment