Habari za Punde

Hali ya Mtaro uliopo Biziredi inasikitisha na kuhatarisha afya

Mkurugenzi wa Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar Makame Khatibu Makame akielezwa kusikitishwa na hali ya uchafu katika mtaro iliopo eneo la Biziredi na kuwataka Wafanyabiashara na Baraza la Manispaa Mjini  kuirekebisha hali hiyo wakati alipofanya ziara na Kikosi Kazi cha Kutokomeza Kipindupindu Zanzibar
Baadhi ya Wajumbe wa Kikosi Kazi cha Kutokomeza Kipindupindu Zanzibar (ZACCEP) wakionyesha kutokuridhika kwao na hali ya uchafu  katika mtaro uliopo kwa Biziredi  wakati wa ziara  ya kutembelea maeneo hatarishi ya maradhi ya mripuko  



Huu ndio hali halisi ya muonekano  mtaro ambao umetuama uchafu katika eneo la  Biziredi. 

PICHA ZOTE NA KHADIJA KHAMIS - MAELEZO ZANZIBAR


Na Kijakazi Abdalla           Maelezo      7/02/2021

Baraza la Manispaa Mjini limetakiwa kushirikiana na wafanyabiashara  kuhakikisha mitaro ya maji machafu inakuwa safi ili kujiepusha na maradhi ya mripuko.

Hayo ameyasema Mkurugenzi wa Kamisheni ya kukabiliana na Maafa Makame Khatibu Makame wakati alipofanya ziara akiwa na kikosi kazi cha kukabiliana na maradhi ya kipindupindu (ZACCEP) katika mtaro uliopita biziredi kuelekea Gulioni .

Ameonyesha kutoridhishwa na hali ya mtaro huo kutokana na kujaa uchafu jambo ambalo linaweza kusababisha mripuko wa maradhi ya matumbo na kipindupindu.

Alilitaka Baraza la Manispaa kuwa na utaratibu wa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika maeneo ya maduka na mitaro ili kuweza kudhibiti uchafu ambao unaweza kuleta madhara kwa wananchi.

Aidha Mkurugenzi Makame amewashauri wafanya biashara kujenga utamaduni wa kufanya usafi katika maeneo yao na kuhifadhi taka  katika sehemu ambazo zitazuia kusambaa na kuingia katika mitaro na hatimae kuleta athari.

Kaimu Msaidizi Mkurugenzi Idara ya Maendeleo Huduma za jamii Baraza la Manispaa Mjini Said Soud Mtambuka amesema kuwa kuna baadhi ya nyumba katika eneo hilo zimekuwa zikitiririsha maji machafu katika mtaro huo jambo ambalo limekuwa likileta usumbufu kwa Baraza hilo.

Amesema kuwa suala la usafi ni la wananchi wote sio kwa kampuni pekee hivyo ni vyema kwa wananchi kushirikiana ili kudhibiti maradhi kusambaa.

Kaimu Mkurugenzi Soud amesema kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa na dhana kuwa Baraza la Manispaa pekee ndilo lenye jukumu la kufanya usafi lakini jukumu hilo linawahusu wananchi wote wanaoishi ndani ya Manispaa husika.

Kaimu Mkurugenzi huyo ameyafungia baadhi ya maduka  ambayo yamekaidi agizo la kuweka vyombo maalum  veya kuhifadhia taka katika maeneo  ya maduka yao.

Ziara za kutembelea maeneo yenye visababishi vya maradhi ya mripuko zitaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuhakikisha usafi wa mazingira unaimarishwa ikiwa ni miongoni mwa Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Kipindupindu Zanzibar (ZACCEP). 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.