Katibu Mkuu Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ)Bw. Islam Seif Salum akieleza hatua zilizochukuliwa na zitakazochukuliwa na Wizara hiyo katika kuhakikisha kwamba urasimishaji biashara unaleta tija na kuzalisha ajira zaidi kama ilivyo dhamira ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Na Mwandishi wetu- Unguja
Katibu Mkuu Wizara ya
Biashara na Maendeleo ya Viwanda ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) Bw.
Islam Seif Salum amesema kuwa Wizara hiyo itaongeza kasi katika kuhakikisha
urasimishaji biashara unakuwa chachu ya kuzalisha ajira visiwani humo baada ya
Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Bishara
za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) kujenga uwezo ili kutekeleza azma ya
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwezesha
wananchi kwa kuzalisha ajira zaidi katika sekta hiyo.
Ameyasema hayo
leo katika eneo la Darajani Unguja
wakati wa hafla ya uzinduzi wa
Kituo jumuishi cha Biashara iliyoshirikisha wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya
MKURABITA waliopo ziarani visiwani humo
kuwatembelea wanufaika wa mpango huo na kuona hatua walizofikia baada ya
urasimishaji kufanyika kupitia mpango huo.
“Kituo hiki kinalenga kuwawezesha wananchi
kupata huduma zote za urasimishaji biashara katika eneo moja ili kuwaondolea
adha ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma katika taasisi mbalimbali za
Serikali, Wizara na taasisi zilizopo chini yake zitaendelea kutenga bajeti ili
kuwezesha suala la urasimishaji biashara kutekelezwa kwa kasi zaidi hali itakayochangia katika kuzalisha ajira
kwa wingi zaidi na kukuza uchumi hapa Zanzibar”,alisisitiza Salum
Akifafanua, amesema
urasimishaji uliofanyika umeenda sambamba na kuwapatia mafunzo wafanyabiashara
wadogowadogo ili waweze kusimamia biashara zao vizuri,kuweka kumbukumbu, kuwa
na akaunti za biashara na kufanya biashara kwa tija.
“Katika hatua za
ujenzi wa kituo Wizara ilipokea kutoka MKURABITA jumla ya shilingi milioni
57,109,500/ambazo kati hizo shilingi milioni 27,969,000/- zilitumika katika
shughuli za urasimishaji kwa Unguja na pemba na Shilingi milioni 29,140,500/
zilitumika kwa ajili ya ujenzi mdogo wa kuweka vibanda sita,ununuzi wa
vifaambalimbali ikiwemo meza 6, viti6, kabati 1, Computer na vifaa vingine.
Kuhusu hatua
zilizochukuliwa na Serikali katika
kuwezesha wananchi baada ya urasimishaji amesema kuwa ni pamoja na kupunguza
ada ya usajili wa majina ya biashara,kuanzishwa kwa mfumo wa kielekrtoniki ili
kusogeza zaidi huduma kwa wananchi.
Naye Makamu
Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya MKURABITA Bi Immaculata Senje amesema kuwa
kamati imeridhishwa na utekelezaji wa kazi za urasimishaji katika maeneo yaliyofikiwa na mpango huo
visiwani humo.
Aidha, Bi. Senje
amesema kuwa ushirikiano uliopo katika ya MKURABITA na Wizara hiyo umewezesha
tija katika urasimishaji biashara
Zanzibar.
Aliongeza kuwa kuna
umuhimu wa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu urasimishaji biashara ili wajitokeze zaidi na kutumia fursa hiyo
kuongeza tija.
Mratibu wa MKURABITA
Dkt. Seraphia Mgembe amesema kuwa wananchi waliorasimisha biashara zao wameanza
kuona faida ya mpango huo wenye azma ya kuleta ukombozi wa kiuchumi kama ilivyo
dhamira ya Serikali zote mbili.
Aliongeza kuwa
mafanikio yaliyofikiwa ni chachu ya kuongeza kasi katika kuwahamasisha wananchi
wengi zaidi kujitokeza na kurasimisha biashara zao ili ziweze kufanyika kwa
kuzingatia mifumo ya sheria na taratibu zilizopo na pia kuwawezesha wananchi
kunufaika na mikopo kutoka taasisi za fedha.
Akitoa taarifa ya
urasimishaji visiwani humo , Mkurugenzi wa Biashara na Masoko Bw. Khamis Ahmada
Shauri amesema kuwa jumla ya
wafanyabiashara 461 wamerasimisha biashara zao visiwani humo baada ya kujengewe
uwezo kupitia mafunzo yaliyoendeshwa na MKURABITA na Wizara hiyo katika awamu
zote za urasimishaji hadi kufikia mwaka 2020.
MKURABITA na Wizara ya Biashara na Maendeleo ya
Viwanda ya Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar (SMZ), pamoja na Tume ya Mipango imefanikiwa katika kuwezesha wananchi
kurasimisha biashara na ardhi ili kujikwamua kiuchumi na kushiriki katika
ujenzi wa uchumi.
No comments:
Post a Comment