Habari za Punde

Mbunge wa Jimbo la Kisesa Mhe. Mpina Amwaga Machozi Akimlilia Dkt.John Magufuli. Akosa Zawadi ya Kumpa Anena Mazito Kwa Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.

MBUNGE wa Jimbo la Kisesa,Mhe. Luhaga Mpina akizungumza na waandishi wa habari wakati akiwa msibani Chato

BUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina amemlilia aliyekuwa Rais wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli akimtaja kama kiongozi wa mfano na kielelezo barani Afrika katika kuleta maendeleo na kushughulikia kero na matatizo ya wananchi yaliyoshindikana kwa miaka mingi.

Mpina ambaye katika kipindi cha miaka mitano ya Rais Magufuli aliwahi kuwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira na baadae kuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Akizungumza mara baada ya kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa Marehemu Dk. Magufuli kwenye uwanja wa Magufuli mjini Chato, Mpina alisema taifa limepata pigo kubwa kwa kuondokewa na kiongozi makini na shujaa ambaye alitumia muda wake wote wa uongozi kusaka maendeleo ya nchi huku akikomesha na kumaliza dhuluma na vikwazo vilivyokuwepo dhidi ya ustawi wa jamii, uchumi na maendeleo ya nchi yetu.

“Nilizipokea taarifa za kifo cha Mhe. Rais Dk. Magufuli kwa huzuni na majonzi makubwa nililia kwa kupaza sauti zaidi ya saa moja na baadae machozi yaliendelea kutiririka kama maji nikiwa sijui hata la kufanya jitihada za kuninyamazisha na kufuta machozi hazikuwezekana, tangazo la kifo cha kiongozi huyu ilikuwa ni mkuki uliochoma moyo wangu na kuujeruhi sana, Kiongozi nimpendaye mchakapazi na hodari asiyeyumba wala kuyumbishwa katika maamuzi asiyechoka kupambania taifa lake na asiye na rekodi ya kushindwa jambo lolote kweli ndio hatunaye tena” alisema Mpina.

Mpina amesema maamuzi ya mwenyezi Mungu hayana rufaa na hayahojiwi popote tumebaki wakiwa na majonzi yasiyokufani Mungu atabaki kuwa Mungu na mwenye mamlaka yote, hivyo tunamuomba Mungu wa mbinguni amuongoze  Rais wetu Samia Suluhu Hassan katika kuliongoza taifa letu kwa bidii na upendo mkubwa.  

“Nimehudumu kama Naibu Waziri kwenye iliyokuwa ofisi yake ya Makamu wa Rais hivyo Sina mashaka kabisa na utashi, uwezo, dhamira  na kipaji cha  wa Mhe. Rais Samia katika kuhakikisha kuwa taifa linasonga mbele kwa mafanikio makubwa namuomba Mungu azidi kumwagia Baraka ili ndoto za mafanikio ya taifa letu zifikiwe” alisema Mpina.

Alisema Rais Magufuli kwa muda mfupi wa miaka mitano alipambana na kufanikiwa kukosemesha vita dhidi ya madawa ya kulevya ambapo sehemu kubwa ya vijana waliangamia alidhibiti na kuvunja mitandao ya biashara hiyo haramu hapa nchini ambapo madawa yaliyoingizwa nchini yalikamatwa na kutaifishwa na Serikali na jumla ya watuhumiwa 37,104 walitiwa mbaroni ambapo imepelekea kupunguza uingizaji wa dawa za kulevya nchini kwa asilimia 90.

Kuhusu Mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, Mpina amesema Rais Magufuli  alikuwa kiongozi wa kwanza kuanzisha Mahakama ya Uhujumu Uchumi ambapo watu wote bila kujali nafasi zao wamefikishwa kwenye mahakama hiyo pia aliipa meno  TAKUKURU kushughulika na wala rushwa ambapo kwa miaka mitano rushwa imepungua kwa kiasi kikubwa nchini, Serikali yake imefanikiwa kurejesha mali za umma zilizochukuliwa na watu binafsi ama taasisi kinyume cha sheria na pia ameweza kuokoa kiasi cha shilingi bilioni 273 zilizokuwa zimeibiwa.

Pia Rais Magufuli alifanikiwa kukomesha ujangili na ujambazi ambapo kabla ya hatua zake biashara ya pembe za ndovu na nyara zingine za Serikali ilipamba moto katika taifa letu na wanyama wengi kuuawa na kusafirishwa hai kwenda nje ya nchi kinyume cha sheria, majambazi yalitamba kila kona na kuhatarisha usalama wa raia na mali zao. Hatua alizochukua Rais Magufuli zimemaliza vitendo hivyo na mapato yatokanayo na  utalii yameongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 1.9 mwaka 2015 hadi Dola za Marekani bilioni 2.6.

Mpina alibanisha kuwa kabla ya Rais Magufuli mauaji ya vikongwe na albino yalikithiri kila kona ya nchi na kufanya kundi la wananchi hao kuishi kwa hofu na fedheha kubwa ndani ya nchi yao ambapo kwa muda mfupi wa uongozi wake vitendo hivyo vimekomeshwa na sasa makundi haya yanaishi kwa amani na kushiriki shughuli za kiuchumi bila wasiwasi wowote .

Pia Mpina kabla ya Rais Magufuli uvuvi haramu ulitamalaki kila kona kunakofanyika shughuli za uvuvi na kusababisha samaki kupungua kwa kiasi kikubwa hali iliyochangia viwanda vingi vya samaki kufungwa huku mauzo ya samaki nje ya nchi yakiporomoka na nchi kutegemea samaki wa kutoka nje ya nchi, kwa upande wa pwani uvuvi haramu wa kutumia mabomu ulisababisha watu wengi kupoteza maisha na kupata ulemavu wa kudumu wa viungo.

Kutokana na hali hiyo Rais Magufuli alichukua hatua thabiti ya kudhiti uvuvi haramu nchini ambapo uvuvi wa kutumia mabomu umedhibitiwa kwa asilimia 100 na uvuvi wa kutumia zana haramu umedhibitiwa kwa asilimia 80 hali iliyopelekea ongezeko kubwa la samaki, viwanda kuongezeka, kupungua kwa uagizaji wa samaki kutoka  nje ya nchi kutoka thamani ya tsh. Bilioni 56 kwa mwaka hadi tsh. bilioni 0.16 kwa mwaka, mauzo ya samaki nje ya nchi yameongezeka kutoka bilioni 379 mwaka 2015 hadi  bilioni 692 mwaka 2019 hayo ni mafanikio makubwa ya Dk. Magufuli.

Kuhusu kuongeza ukusanyaji wa mapato na udhibiti wa upotevu wa mapato ya Serikali, alisema Rais Magufuli aliweka mifumo imara ya TEHAMA, alipanua wigo wa walipa kodi, kupunguza misamaha ya kodi, kufuta mikataba ya kinyonyaji, kudhibiti utoroshaji wa fedha na rasilimali nyingine kwenda nje ya nchi.

Kutokana na jitihada hizo Mpina alisema ukusanyaji wa mapato ya kodi kwa mwezi umeongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 850 mwaka 2015 hadi wastani wa shilingi trilioni 2 kwa mwezi mwaka 2020. Kwa ujumla mapato ya ndani yameongezeka kutoka trilioni 11 mwaka 2015 hadi kufikia trilioni 18.5 mwaka 2019.

Pia Mpina alisema wakati Dk John Magufuli anaingia madarakani nchi yetu ilikuwa miongoni mwa nchi zinazotorosha fedha nyingi za umma kwenda nje ya nchi kinyume cha sheria na bila kulipa kodi stahiki za Serikali (Illicit Financial Flows).

Mpina aliongeza kuwa makampuni ya kimaitaifa yaliyowekeza na kufanya biashara nchini hususani makampuni ya simu, madini na gesi yalikuwa  yakiongeza gharama za uwekezaji kwa lengo la kukwepa kodi (Transfer Pricing) na kuisababishia Serikali kukosa mapato.

Dk. Magufuli alichukua hatua mahususi ya kumaliza tatizo sugu la utoroshaji wa fedha na uongezaji gharama ambapo tulishuhudia kufutiwa kwa leseni baadhi ya mabenki na maduka ya kubadilisha fedha  yaliyokiuka sheria za usimamizi wa fedha. Pia mifumo thabiti ikawekwa ya usimamizi na matumizi ya fedha za kigeni nchini pamoja na kutungwa sheria mpya kuongeza udhibiti.

Mpina alisema mbali na hayo pia Rais Magufuli alifuta mikataba ya kidhalimu iliyokuwa ikilinyonya taifa kila uchao ambapo alizima mitambo ya IPTL, Aggreko na Syimbion na kuokoa shilingi  bilioni 719 kwa mwaka.

Mpina alisema Rais Magufuli alidhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma kwa kuzuia au kupunguza safari za nje zisizo za lazima, semina, warsha, makongamano, matamasha na udanganyifu kwenye manunuzi.

Kutokana na jitihada kubwa alizofanya Dk. Magufuli katika udhibiti na usimamizi wa mapato na matumizi umewezesha nchi yetu kuongeza bajeti ya maendeleo kutoka wastani wa asilimia 26 hadi asilimia 40 na ndio chimbuko kwa nchi kuanza kujenga miradi mikubwa kwa fedha za ndani ikiwemo Reli ya SGR na Ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere.

Alisema Dk. Magufuli alianzisha mfumo wa utoaji elimu bila malipo kwa shule za msingi na sekondari ambapo umetoa unafuu mkubwa kwa watoto masikini kuweza kupata haki ya elimu hali hiyo imewezesha ongezeko la vijana wengi kusajiliwa kujiunga na masomo ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Aidha Rais Magufuli aliendelea kuishangaza nchi alipokuwa akiongeza bajeti ya mikopo ya elimu ya juu kutoka shilingi bilioni 348.7 mwaka 2014/2015 hadi shilingi bilioni 450 mwaka huu wa Fedha 2019/2020 na kuwezesha vijana wengi kupata mikopo na kuendelea na masomo ya juu.

Kwa upande wa sekta ya afya, Mpina alisema kwa kipindi kifupi cha uongozi wa Dk. Magufuli vituo vipya vya kutolea huduma za afya 1,769 vimejengwa huku bajeti ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015 hadi shilingi bilioni 270 hivi sasa

Pia Rais Magufuli aliimarisha matibabu ya kibingwa nchini hususan magonjwa ya moyo, mifupa na figo ambapo imewezesha idadi ya rufaa za kwenda nje ya nchi kupungua kwa asilimia 95 ambazo zilikuwa zikiingarimu nchi fedha nyingi huku wagonjwa wasio na uwezo wa kwenda nje ya nchi walikufa bila  matibabu.

Mpina alisema Rais Magufuli aliimarisha huduma za mawasiliano kwa kuongeza usikivu wa simu kutoka asilimia 74 mwaka 2015 hadi asilimia 94 mwaka 2020 na kuwezesha kupungua kwa gharama za kupiga simu kwa dakika moja kutoka shilingi 267 mwaka 2015 hadi shilingi 40 tu hivi sasa hali iliyoleta unafuu mkubwa kwa wananchi na kukuza uchumi kupitia sekta hiyo.

Mpina alisema Rais Magufuli amesimamia ujenzi wa barabara na madaraja mengi nchi nzima akiwa Waziri wa Ujenzi na baada ya kushika wadhifa wa urais kwa kipindi cha miaka mitano amewezesha kujengwa na kukamilika barabara za lami zenye jumla ya kilometa 3,500  pia Barabara nyingine zenye urefu wa zaidi ya kilometa 2,000 zinaendelea kujengwa kote nchini na kurahisha shughuli za kiuchumi na kijamii.

Pia Rais Magufuli amejenga  madaraja makubwa 13 yaliyoshindikana kujengwa kwa miaka mingi na kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu amejenga barabara za juu (flyover na interchange) Dar es Salaam za Kijazi na Mfugale pamoja na  barabara ya njia nane kutoka Kimara kwenda Kibaha ili kupunguza tatizo la msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam.

Rais Magufuli aliamua kujenga reli ya kisasa ya SGR kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza ambapo utekelezaji wake uko kwenye hatua mbalimbali mradi huu mkubwa unajengwa kwa fedha za ndani. Pia usafiri wa reli ya Dar es Salaam –Tanga – Moshi - Arusha, ambao ulisimama kwa takriban miaka 20. Lakini, katika kipindi chake alifanikiwa kurudisha tena usafiri wa treni kutoka Dar es Salaam kwenda Tanga, Moshi hadi Arusha na kurahisha shughuli za usafiri na uchukuzi.

Aliongeza kuwa bandari nyingi zimepanuliwa katika ukanda wa Pwani na maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na kujenga na kukarabati meli zilizokuwa zimetelekezwa kwa miaka mingi ambapo  Ziwa Victoria pekee amekarabati meli tano na kujenga Chelezo moja kubwa kwa ajili  kujenga na kukarabati meli hizo.

Mpina alisema Rais Magufuli amejenga wa viwanja vya ndege vipya 11 na kununua ndege mpya 11 za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) na kupelekea kuongezeka kwa huduma za usafiri wa anga ndani na nje ya nchi.

Mpina aliongeza kuwa Dk. Magufuli alifanya maamuzi yaliyoshindikana kwa miaka mingi na kuanza ujenzi wa  Mradi mkubwa wa Bwawa la Nyerere kwenye Bonde la Mto Rufiji. Mradi huu unagharimu shilingi trilioni 6.5 na utakapokamilika utazalisha umeme Megawati 2115 ambapo itapunguza gharama za umeme na kumaliza tatizo la upungufu wa umeme nchini.

Pia Mpina alisema kupitia Mradi wa REA Dk. Magufuli katika kipindi chake kifupi ameongeza idadi ya vijiji vilivyofikishiwa umeme kutoka 2,018 mwaka 2015 hadi vijiji 9,112 mwezi Aprili 2020 na jumla ya viwanda vipya 8,477 vimejegwa nchini na kupunguza tatizo la ajira.

Mpina alisema kabla ya Dk. Magufuli hajaingia madarakani wafugaji walifukuzwa kama wakimbizi kwenye nchi yao na kutakiwa kurudi walikotoka, migogoro ya  wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi ilishamiri na kusababisha mapigano yasiyokoma ambapo walijeruhi na kuuana  pia mifugo mingi ilikufa kwa kukatwa mapanga na kuwekewa sumu na mingine kutaifishwa.

Mpina alisema Hayati Dk. Magufuli alipunguza kwa kiwango kikubwa migogoro hiyo kwa Serikali yake kufanya ziara maeneo yenye migogoro na kuunda timu ya mawaziri nane, alichukua uamuzi wa kurasimisha vijiji 920 vilivyoanzishwa ndani ya hifadhi.

Pia alisema Dk. Magufuli alifuta baadhi ya hifadhi na mashamba ya Serikali na kugawa ardhi hiyo kwa wananchi ili itumike kwa shughuli za kilimo na ufugaji pia katika kukabiliana na magonjwa ya mifugo nchini alijenga majosho mapya 104 na kukarabati majosho 542 yaliyokuwa yametelekezwa kwa zaidi ya miaka 30 na ameimarisha utoaji chanjo za mifugo na kuanzisha kampeni ya uogeshaji mifugo kwa dawa za ruzuku kote nchini, Pia ukusanyaji wa mapato yatokanayo na mifugo na uvuvi yaliongezeka kutoka wastani tsh bilioni 21 mwaka 2015  hadi kufikia tsh bilioni 74 mwaka 2020.

Mpina amesema katika kipindi chake Rais Magufuli aliweza kutatua tatizo la ukosefu wa mitaji kwa wakulima, wafugaji na wavuvi ambapo Serikali imeipa TADB shilingi bilioni 325  ili kuongeza uwezo wa kutoa mikopo kwa wakulima, wafugaji na wavuvi nchini ambao kwa miaka mingi walikuwa hawakopesheki.

Mpina alibainisha kuwa katika kipindi cha Magufuli alifanikiwa kumaliza tatizo la uvuvi haramu ambapo tulishuhudia wingi wa samaki pamoja na Samaki wakubwa kupatikana mfano sangara kwenye Ziwa Victoria waliongezeka kutoka tani 417,936 mwaka 2016 hadi tani 816,964 mwaka 2020, na urefu wa sangara umeongezeka kutoka wastani wa sentimeta 16 hadi sentimeta 25.2. 

pia  Uzalishaji wa vifaranga vya samaki katika vitotoleshi vya Serikali na Sekta binafsi uliongezeka kutoka 8,090,000 mwaka 2015 hadi kufikia vifaranga zaidi ya 50,000,000 mwaka 2020. Kutokana na uzalishaji huo hivi sasa nchi yetu haiagizi vifaranga vya samaki tena kutoka nje ya nchi.

Mpina alisema katika kipindi cha utawala wa Rais Magufuli sheria nyingi mpya  zilitungwa na zingine kufanyiwa marekebisho ili kulinufaisha taifa akitolea mfano wa Sheria ya kulinda rasilimali za taifa( The Natural Weath and Resources -Permanent Sovereignty –Act 2017) sheria hii imewezesha kuanzishwa kwa Kampuni ya Twiga Minerals Company ambapo Serikali yetu inamiliki hisa asilimia 16 na Kampuni ya Barrick asilimia 84 ya Hisa utaratibu huu haukuwepo hali iliyosababisha nchi kutopata mapato stahiki katika madini na gesi.

Mpina aliongeza kuwa kutokana na hatua alizochukua Rais Magufuli mapato yatokanayo na madini  yameongezeka kutoka shilingi bilioni 194 mwaka 2016 hadi wastani wa shilingi bilioni 500 mwaka 2020.

Pia Rais Magufuli alikomesha dhuluma kwa wachimbaji wadogo ambapo kila walipokuwa wanagundua madini walifukuzwa kama wakimbizi ndani ya nchi yao ili kupisha wawekezaji lakini chini ya utawala wake wametengewa maeneo na wanafanya  kazi ya uchimbaji vizuri na kujipatia kipato.

Hata hivyo Mpina alisema kutokana na jitihada zake hizi Rais Magufuli aliiwezesha nchi yetu kuwa miongoni mwa nchi zinazokua kwa kasi kiuchumi na Tanzania kuwa miongoni mwa nchi 10 zenye uchumi mkubwa zaidi Barani Afrika.

“Nikupe zawadi gani Dk. Magufuli kwa wema uliolitendea  taifa lako katika kipindi kigumu na chenye vitisho vingi hukusita kuchukua maamuzi, hukukubali kutishwa, kuyumbishwa wala kukatishwa tamaa na mtu yoyote au taasisi za kimataifa katika kufanya maamuzi sahihi kwa taifa lako ambapo uimara wako huo ndio umepelekea nchi yetu kupiga hatua kubwa za kimaendeleo na kiuchumi ambapo kumepelekea nchi yetu kuingia uchumi wa kati ndani ya miaka mitano badala ya miaka 10 iliyotarajiwa” alisema Mpina

Mpina alisema pia Rais Magufuli alikuwa mtetezi wa wanyonge ambapo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita aliyakumbuka makundi ambayo yalikuwa hayathaminiwi na kufanyiwa kila aina ya dhuluma na baadhi ya watendaji wa Serikali kama Mama ntilie, Bodaboda na Machinga ambapo dhuluma zilikomeshwa kwa kutengewa maeneo biashara na kuondolewa mzigo mkubwa wa ushuru uliokuwa unawaelemea kila uchao kwa kutengenezewa vitambulisho vya wajasiriamali.

Pia Rais Magufuli alifanikisha kutungwa Sheria yenye kuzitaka halmashauri zote kutenga asilimia 10 ya mapato yao kwa ajili ya kutoa mikopo isiyo na riba kwa wanawake (asilimia 4), vijana (asilimia 4) na wenye ulemavu (asilimia 2), ambapo hadi mwezi Machi 2020 kiasi cha shilingi bilioni 93.2 kilikuwa kimetolewa.

“Dk. John Pombe Magufuli jembe umeliacha shambani namuomba Mungu ampe nguvu na uwezo mkubwa Rais wetu Mhe. Samia Suluhu Hassan kukamilisha na kuendeleza kazi iliyobaki shambani tutakukumbuka kwa wema wote uliotufanyia watanzania na utabaki kuwa shujaa katika taifa letu.

Si rahisi kuoredhesha mambo yote uliyofanya Magufuli, Uchapakazi wako umesisimua wananchi na ulimwengu mzima leo unaenda Kaburini taifa likiwa kwenye majonzi makubwa wananchi wote wa Tanzania, Afrika Mashariki na Dunia nzima wanakulilia ona maandamano makubwa ya watu toka sehemu mbalimbali wanaomiminika kuja kukuaga na kukusindikiza katika safari yako ya mwisho duniani,  Mungu aiweke roho yako mahali pema peponi, upumzike kwa amani, Buriani Rais Magufuli, Buriani Rais wa Wanyonge pumzika kwa amani“ alisema Mpina

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.