Na.Oscar Assenga - TANGA
KIWANDA cha Tanga Pharmaceutical and Plastic Limited (TPPL) leo wametoa msaada wa vifaa tiba katika kituo cha Afya Pongwe Jijini Tanga vyenye thamani ya Sh Milioni 2.4 kwa ajili ya kusaidia kambi ya upasuaji wa pua, masikio na koo.
Vifaa vilivyokabidhiwa ni Endotracheal Tubes 100, Syringe 10 CC 1000,Syringe 5CC 1000,Syringe 2 CC 1000 na JIK Tablets 5000 ambavyo vitasaidia katika utoaji wa huduma kwenye kituo hicho.
Akizungumza wakati akikabidhi Msaada huo,Afisa Rasilimali Watu wa Kiwanda hicho,Jenipher Mburuja alisema kiwanda hicho kimetoa msaada huo ikiwa ni katika kurudisha kwa jamii inayowazunguka ambapo wamekuwa wakifanya hivyo kwenye kusaidia masuala mbalimbali.
Alisema baada ya kupokea maombi ya ufadhili kwa ajili ya kambi ya upasuaji wa Pua,Masikio na Koo waliona ni muhimu kuwasaidia msaada huo wa vifaa ili kuweza kufanikisha kambi hiyo ikiwa ni kuondosha changamoto ambazo zinaweza kujitokeza wakati wakiendelea na zoezi hilo.
“Tulipopokea maombi ya ufadhili wa Kambi hiyo kwa ajili ya vifaa tiba vya upasuaji wa pua,masikio na koo na tukiwa kama wadau wa afya tukaona tununue vifaa hivi vyenye thamani ya milioni 2.4 kwa ajili ya kuwasaidia uponyaji wa magonjwa hayo “Alisema Mburuja ambaye ni Afisa Rasilimali Watu wa Kiwanda cha (TPPL)
Aidha alisema pia katika kurudisha kwa jamii inayowazunguka kiwanda hicho ambacho ni wadau wakubwa wa Elimu,Usalama na Afya,wametoa misaada mbalimbali kwa jamii ikiwemo kujenga banda la watoto la kliniki kituo cha Afya Makorora,Benchi la kukalia wagonjwa kituo cha Afya Duga,wamewakatia Bima ya Afya ya NHIF wanafunzi walemavu 83 Pongwe.
Afisa Rasilimali huyo alisema pia walikwisha kununua viti vya kusubiria wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga Bombo ikiwemo kutoa vitanda 20,magodoro 20 na shuka 20 katika kituo cha Afya Duga ikiwemo friji la kuhifadhia damu kwenye kituo cha Afya Pongwe.
Akizungumza wakati akipokea msaada huo ,Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Pongwe Dkt .Ummykulthum Kipanga alishukuru kwa msaada huo ambao wamepatiwa na kiwanda hicho huku akieleza umefika wakati muafaka kwani Tanga kuna tatizo la Koo na Pua ambalo linapelekea watu kwenda Dar kwa ajili ya kufuata matibabu .
Alisema baada ya kuliona hilo waliwaomba madaktari bingwa wafike kwa ajili ya kufanya upasuaji kwenye kituo hicho na kiwanda hicho hakikuweza kuwaacha nyuma waliwashika mkono kufanikisha jambo hilo.
Naye kwa upande wake Afisa Muuguzi wa Kituo cha Pongwe Bahati Shiminogeni alisema wamefurahi sana wao kama watumishi kwa vifaa hivyo hasa Jik ambayo ni gharama kubwa ukiangalia kopo moja bei yake ni elfu 65000.
No comments:
Post a Comment