Habari za Punde

Dk. Mwinyi Mgeni Rasmin Kongamano la Kupinga Udhalilishaji Zanzibar.

Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar  ZAFELA Jamila Mahmoud (kushoto) akijibu maswali ya waandishi wa habari wakati wa utoaji wa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu kongamano la kupinga Udhalilishaji Zanziabar linalotarajiwa kufanyika julai 28 katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil saa 8:00 mchana ambapo Rais wa Zanzibrar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Mwinyi  anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kongamano hilo. Kulia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya wanasheria wanawake Zanzibar Safia Hija Abras.

Picha na Fauzia Mussa - Maelezo Zanzibar.

Na Sabiha Khamis    Maelezo  23/07/2021.                                                                  

Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar ZAFELA inatarajia kufanya  kongamano la kitaifa kuhusu udhalilishaji wa kijinsia pamoja na uzinduzi wa mfumo wa ukusanyaji wa taarifa za kesi za udhalilishaji ulionzishwa na jumuiya hiyo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari katika ofisi za ZAFELA Mpendae, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Safia Hija Abras amesema Jumuiya  imeandaa mfumo mpya wa ukusanyaji data ili kuipima utendaji  kazi katika utetezi wa maswala  ya Udhalilishaji ambao  utasaidia kuondoa mgongano wakati wa kutoa taarifa za kesi zilizoripotiwa baina ya taasisi moja na nyengine .

Bi safia alieleza kuwa kila taasisi inayosimamia kupiga vita vitendo vya udhalilishaji itaweza kutumia mfumo huo ili kuepuka kujirejea kwa taarifa wakati wa uwasilishaji wa kesi hizo.

“Katika utendaji wa kazi zetu tumeona ili tuweze kupima na kujipima jinsi gani utetezi unafanyika katika masuala ya udhalilishaji ni vyema kuwa na mfumo maalum amabao utakuwa unakusanya data hii itaepusha utofauti wa kuripoti kiwango cha taarifa za udhalilishaji kutoka taasisi moja na nyengine” alisema Mwenyeiti.  

Mwenyekiti huyo alifahamisha kuwa  kupitia kungamano hilo watapata nafasi ya kutoa taarifa za utekelezaji, mafanikio na changamoto wanazokumbana nazo kuanzia kipindi cha Januari hadi sasa  katika kuhakikisha kwamba wanafikio lengo la jumuiya hiyo la kutokomeza vitendo hivyo vya udhalilishaji wa kijinsia nchini.

Nae Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar ZAFELA Jamila Mahmoud amesema jamii imekuwa na muamko mkubwa  wa kufika katika vituo vya sheria katika kutoa  malalamiko ambapo kutoka mwaka 2020 hadi 2021  jumuiya hiyo imepokea kesi zaidi ya 100 za vitendo vya udhalilishaji.

 Kongamano hilo ambalo linalotarajiwa kufanyika Julai 28, katika Ukumbi wa Idrisa Abdulwakil  litajumuisha Asasi za kiraia na taasisi za Serikali ikiwemo jeshi la Polisi, na watendaji wa Mahkama ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Ali Mwinyi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.