Habari za Punde

Jamii yatakiwa kuwafichua wanaojihusisha na madawa ya kulevya

Waumini wa Mskiti wa Tunduni uliopo wilaya ya Kati Unguja wakimskiliza Makamu wa Pili wa wa Zanzibar alipowasalimia mara baada ya kutekeleza Ibada ya Sala ya Ijumaa.

 Mhe. Hemed akiwakumbusha waumini waliotekeleza ibada ya sala ya Ijumaa katika Mskiti wa Tunduni na wananchi kwa ujumla kuwafichua kwa kutoa taarifa katika mamlaka husika watu wanaojihusisha na vitendo haramu vya dawa za Kulevya.  


Na Kassim Abdi, OMPR

Jamii Nchini imetakiwa kutoa taarifa kwa mamlaka husika kwa kuwafichua  watu wanaojihusisha na vitendo haramu dhidi ya dawa za kulevya.

Makamu wa Pili wa Rais Mhe. Hemed  Suleiman Abdulla alieleza hayo baada ya kutekeleza  ibada ya sala ya Ijumaa alijumuika na waumini katika mskiti wa Tunduni  uliopo Wilaya ya Kati Unguja.

Alisema viongozi wa Dini wana nafasi kubwa ya kukemea vitendo viovu ikiwemo kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya  jambo linalosababisha athari hasa kwa rika la vijana.

Mhe. Hemed alieleza kuwa, suala la uwingizaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya katika jamii halikubaliki na linapaswa kupigwa vita na kila mtu bila kujali tofauti zozote zile za kisiasa, Kiimani au kimaeneo.

Akizungumzia juu ya takwimu za watu wanaotumia madawa ya kulevya Makamu wa Pili wa Rais  alisema kwa sasa Zanzibar ina watu takribani Elfu Kumi (10,000) wanajihusisha na matumizi ya dawa za kulevya kitendo ambacho kinaashiria miaka kumi ijayo kila nyumba Zanzibar itakua na mtumiaji wa dawa hizo jambo ambalo halitoi picha nzuri kwa kizazi cha baadae.

Alieleza katika kudhibiti kadhia hiyo serikali ina mpango wa kubadilisha sheria haraka iwezekanavyo ili kuwabana wale wote wanaojihusisha na vitendo hivyo sambamba na kuchukuwa hatua kali zitakazotoa fundisho kwa kila mmoja anaeshiriki.

“Nawaomba waumini na wananchi wote kwa ujumla tusimame kidete kupinga madawa ya kulevya Zanzibar” Alisema Makamu wa Pili

Akigusia juu ya maradhi ya Covid -19 Mhe. Hemed alitaka jamii kuendelea kuchukua tahadhari  juu ya maradhi hayo kwa kufuata miongozo na maelekezo kutoka kwa watalamu wa Afya nchini ikiwemo kuepuka mikusanyiko isiokuwa ya lazima.

Alifafanua kwamba, Jamii imeshuhudia athari zitokanazo na ugonjwa wa Corona kupitia mataifa mbali mbali duniani hivyo kuna haja ya wazanzibar kujilinda kwa nguvu zote ili kuepuka athari za ugonjwa huo.

Nae, Khatibu katika mskiti huo Sheikh Hassan Sleyum aliwakumbusha waumi kuwa kitu kimoja kwa kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwao ili kufuata kwa vitendo mafundisho ya dini ya kislamu pamoja na kuunga mkono maelekezo yanayotolewa na viongozi  wakuu wa nchi katika mustakbali wa kuwaletea maendeleo wananchi wake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.