Habari za Punde

Tukio la Sunni Madrasa, Waziri wa Elimu awasimamisha kazi Walimu wanaodaiwa kushiriki kuwaadhibu wanafunzi kinyume na taratibu

Baadhi ya Waandishi wa habari wakiskiliza Ufafanuzi uliyotolewa na Naibu Katibu Mkuu kutoka Chama cha Walimu Zanzibar (ZATU) Salim Ali Salim (hayupo pichani) juu ya tukio lilotokea katika Skuli ya Sunni Madrasa iliyopo Mkunazi Mkoa wa Mjini Magharibi hafla iliyofanyika katika Ofisini za Chama hicho Kijagwani Zanzibar.



 Naibu Katibu Mkuu kutoka Chama cha Walimu Zanzibar (ZATU) Salim Ali Salim akitoa ufafanuzi  kwa Waandishi wa habari juu ya tukio lilotokea katika Skuli ya Sunni Madrasa iliyopo Mkunazi Mkoa wa Mjini Magharibi, wa kwanza (kulia) ni Afisa Jinsia kutoka Chama cha Walimu Zanzibar (ZATU) Shuwena Faki Haji hafla iliyofanyika katika Ofisini za Chama hicho Kijagwani Mjini Unguja.

Picha na Maryam Kidiko – Maelezo Zanzibar.


Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe Simai Mohammed Said ametoa agizo la kuwasimamisha  kazi Walimu wote walioshiriki kuwaadhibu  watoto kinyume na kanuni elekezi  hadi uchunguzi utakapo kamilika.


Mhe Simai ametoa agizo hilo kufuatia Mwalimu Suleiman Mohamed Suleiman  kumuadhibu Mwanafunzi kinyume na utarabu wa adhabu  kwa Mwanafunzi pamoja na kutoa taarifa katika vyombo vya habari taarifa zisizo na ukweli.


 Mhe Simai ameyasema hayo wakati wa mkutano wa pamoja na  watendaji wa Skuli  ya Sunni Madressa na Wazazi huko Mkunazini Mjini Unguja.


Amesema kumpiga mtoto si njia sahihi ya kumfunza bali zipo njia mbadala ambazo anaweza kuelekezwa kwa mujibu wa taratibu za adhabu mbadala kwa watoto na akawa mtoto mwema.


Aidha Mhe Simai amempa agizo Mrajis  wa elimu kufanya uhakiki wa leseni za Walimu wote hasa wa Skuli binafsi na kuwachukulia hatua wale wote watakaobainika kukosa sifa za ualimu.


Amesema kuna baadhi ya Walimu wanafanya kazi bila ya kuthibitishwa na kupewa leseni na hivyo kufanya kazi kinyume na maadili na taratibu za fani hiyo.


Akizungumzia suala la watoto  walio na umri  mdogo kuendesha vyombo vya moto hasa wanapokwenda Skuli, Mhe. Simai  amewataka wakuu wa Skuli binafsi  kulikemea suala hilo kwani linaleta athari kubwa hasa wanapopata ajali.


Pia Mhe Sjmai amezitaka Skuli zote za binafsi kuhakikisha wanajiunga na chama cha wamiliki wa Skuli binafsi ili kuondosha  baadhi ya malalamiko yanayozikabili Skuli  hizo, kupitia umoja wao.


Nae Mrajis wa Elimu Wizara ya Elimu Zanzibar bi Zuwena Mataka  amesema sheria ya elimu ina miongozo na kanuni zake ambazo zinaelekeza juu ya adhabu mbadala hivyo kila mwalimu hana budi kuzifuata sheria na kanuni hizo. 


Kwa upande wake Mwenyekiti wa jumuiya ya Skuli binafsi bwana  Feisal Mohamed Said amesema lengo la kuwekwa jumuia hiyo ni kushirikiana  na kusaidiana katika mambo mbali hasa ya kitaaluma pamoja na kutatua changamoto zinazozikabili Skuli za binafsi.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.