Habari za Punde

Majengo mapya hospitali yaendane na uwepo wa vifaa vya kisasa - Rais Dk Hussein Mwinyi

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa ujenzi wa majengo mapya ya Hospitali ni lazima uendane na uwepo wa vifaa vya kisasa.

Hayo aliyaeleza leo mara baada ya kufika na kupata maelezo ya ujenzi wa jengo jipya la wodi ya wanawake na watoto linalojengwa katika eneo la hospitali ya Chake Chake, iliyopo Mkoa wa Kusini Pemba.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, itahakikisha kuwa baada ya kumalizika kwa ujenzi huo kunakuwepo vifaa vitakavyoendana na jengo hilo jipya.

Alisema kuwa mbali ya kujengwa jengo hilo ni vyema kukaangaliwa uwezekanao wa kujenga majengo mengine ya ghorofa kutokana na mazingira ya eneo hilo.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa amefarajika na ujenzi wa Hospitali ya Chake Chake unavyoendelea na kuahidi kutafuta fedha za ziada ili kuona kuwa ujenzi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Alifahamisha kuwepo kwa ujenzi huo pamoja na vifaa utapunguza changamoto wanazozipata wananchi za kufanyiwa vipimo katika Hospitali hiyo na hatimae kusomwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja ama hospitali ya Muhimbili.

Alieleza Serikali itaendelea kutatua changamoto zinazowakumba watendaji wa Wizara ya Afya ikiwemo stahiki zao lakini aliwasihi kufanya kazi kwa uadilifu wakifikiria kauli nzuri kwa wagonjwa ambayo pekee yake ni tiba.

Akitoa maelezo ya ujenzi huo, Daktari dhamana wa Hospitali ya Chake Chake, Abrahman Said Suleiman , alisema kuwa kumalizika kwa jengo hilo la wodi ya akinamama na watoto  kutaondoa matatizo mengi ikiwepo ongezeko la Vitanda kutoka 63 vilivyoko sasa na kufikia vitanda 116.

Hata hivyo, alisema kuwa Hospitali ya Chake Chake imekuwa ikipokea wagonjwa wengi ikiwa ni ya pili ukiachia ya Mnazi mmoja kwani katika mwezi wa July 2020 hadi June 2021 tayari wagonjwa 61,000 walishapatiwa matibabu hospitalini hapo.

Aliomba baada ya kumalizika kwa Wodi hiyo ya akinamama na watoto wanaomba kupatiwa vifaa mbali mbali vya matibabu ikiwemo mashine ya kutambua maradhi yasiyoambukiza na mashine ya Xray.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alipata fursa ya kusikiliza changamoto mbali mbali zilizotolewa na wananchi waliofika katika eneo hilo la Hospitali ya Chake Chake.

Akitembelea mradi wa maji katika kijiji cha Chanjaani Pemba, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa miongoni mwa vipaumbele vya Serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama kwa uhakika ambalo ni suala muhimu kwa wanaadamu.

Alieleza kuwa Serikali itatafuta njia ya kuiwezesha ZAWA, kupata fedha za kusambazia mabomba ya maji kwa haraka ili tatizo  walilonalo wananchi hao liweze kumalizika kwa haraka.

Akizungumzia juu ya kero ya barabara, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa hivi sasa kuna makubaliano na kampuni ya ujenzi wa bara bara  za kilomita 220 za Unguja na Pemba hivyo, aliwataka wananchi kuvuta subira.

Akikagua ujenzi wa barabara ya Kipapo – Mgelema, Rais Dk. Mwinyi alitowa ahadi kwa wananchi kuwa Serikali itaimaliza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami bila ya kuchelewa.

Sambamba na hayo, katika kuwaunga mkono wananchi wa kijiji cha Mgelema katika sekta ya elimu na yeye kwa upande wake aliahidi kuchangia TZS. millioni 5 kwenye ujenzi wa Skuli ya msingi ambayo tayari wananchi wenyewe wameonesha juhudi ya kuchangishana elfu hamsini (50,000/=) kwa kila mtu , ili kukamilisha ujenzi huo.

Mapema, Rais Dk. Mwinyi alipokea taarifa ya Utekelezaji ya Mkoa wa Kusini Pemba huko katika ukumbi wa Makonyo uliopo Wawi, Chake Chake Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.