Na. Mbaraka Kambona
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imejipanga kupeleka miradi ya maendeleo ya ufugaji Kuku, Mbuzi na Samaki katika Wilaya ya Ruangwa ili iwasaidie kuinua Uchumi wao.
Ulega aliyasema hayo
wakati akiongea na Viongozi wa Wilaya ya Ruangwa iliyopo Mkoani
Lindi Septemba 22, 2021.
Alisema kutokana na kasi kubwa ya maendeleo ya Wilaya hiyo
inayochochewa na shughuli za uchimbaji madini Serikali imeona ni vyema kupeleka
miradi hiyo kwa kina mama na vijana ili kukuza uchumi wao na kukidhi mahitaji
ya mazao ya Mifugo katika Wilaya hiyo.
Naibu Waziri Ulega aliitaja miradi hiyo ambayo itapelekwa katika Wilaya hiyo na kuwasaidia
wakina mama na vijana ni pamoja ufugaji
wa kuku na ufugaji wa Samaki na Mradi wa Kopa mbuzi lipa mbuzi.
"Mwezi Oktoba tutaanza na Vikundi kumi, tutaleta
Wilayani hapa kuku elfu mbili (2000) ikiambatana na semina ya kuelekeza namna
ya kufuga kuku hao kibiashara," alisema Ulega
Aidha, Waziri Ulega alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa,
Hassan Ngoma kutafuta eneo zuri ambalo watalitumia kuanza kufanya ufugaji wa
Samaki.
"Sasa tafuteni eneo na kikundi kimoja kizuri ili tuje
kuweka shamba darasa la ufugaji wa samaki, kikundi hicho kitakuwa kinavuna
Samaki hao na watawafundisha na wengine kuhusu ufugaji huo wa samaki,"
aliongeza Ulega
Waziri Ulega alimuahidi Mkuu wa Wilaya hiyo kuwa atapeleka
wataalamu wa shughuli ya ufugaji wa Samaki ili kuwasaidia wananchi hao.
Naye, Mkuu wa Wilaya hiyo alisema kuwa kufuatia kuchipuka
kwa shughuli za madini Wilayani humo kumepelekea kuongezeka kwa mahitaji
mbalimbali muhimu ikiwemo mahitaji ya nyama, mayai, Samaki na maziwa ambayo
mengi yamekuwa yakiagizwa katika maeneo mengine ya nchi na hivyo alimuomba
Naibu Waziri kuona hizo fursa na kuwawezesha wananchi wa Wilaya hiyo ili waweze
kuzitumia.
No comments:
Post a Comment