Habari za Punde

Tanzania Yapokea Msaada wa Shilingi Bilioni 68 Kutoka Ujerumani.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba na Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, wakisaini Mkataba wa Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, kwa ajili ya miradi ya uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba na Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, wakipongezana baada ya kusainiwa Mkataba wa Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, kwa ajili ya miradi ya uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba na Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, wakionesha Mkataba wa Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, baada ya kusainiwa, jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba, akielezea malengo ya Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, zilizotolewa na Serikali ya Ujerumani kuwa ni uhifadhi madhubuti na endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Mhe. Regine Hess, akieleza umuhimu wa utunzaji wa mazingira, wakati wa hafla ya kusainiwa Mkataba wa Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, kwa ajili ya miradi ya uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, akieleza nia ya nchi yake kuongeza msaada wa uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, katika hafla ya kusainiwa Mkataba wa Msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82, jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Emmanuel Tutuba (wa pili kushoto), Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Mhe. Regine Hess (wa pili kulia), Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens (kulia) na Kamishna wa Fedha za Nje wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Sauda Msemo, wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe kutoka Tanzania na Ubalozi wa Ujerumanai, baada ya kusainiwa Mkataba wa Msaada wa shilingi bilioni 67.82, kwa ajili ya miradi ya uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia, jijini Dar es Salaam.

(Picha na WFM, Dar es Salaam)

Na. Farida Ramadhani na Peter Haule, WFM, Dar es Salaam

Tanzania imepokea msaada wa Euro milioni 25 sawa na shilingi bilioni 67.82 kutoka Serikali ya Ujerumani kupitia Benki yake ya Maendeleo ya KfW, kwa ajili ya mradi wa Uhifadhi endelevu wa Maliasili na Mifumo ya Ikolojia nchini.

Mkataba wa msaada huo umesainiwa jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Emmanuel Tutuba, kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na  Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, kwa niaba ya Serikali ya Ujerumani.

Bw. Tutuba alisema kuwa  fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuendeleza na kuhifadhi maliasili katika hifadhi ya Serengeti pamoja na kugharamia mradi wa uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya ikolojia katika maeneo ya ushoroba wa Katavi – Mahale.

“Lengo la mradi wa Serengeti ni  kuchangia katika maendeleo ya kijamii, kiuchumi na usimamizi endelevu wa maliasili katika Wilaya ya Bariadi, Bunda, Serengeti na Ngorongoro wakati mradi wa Ushoroba wa Katavi- Mahale unalenga usimamizi wa maliasili sambamba na kuboresha maisha ya wananchi kwa kuhusisha matumizi bora ya ardhi na utoaji wa Hati miliki za kimila”, alieleza Bw. Tutuba.

Alisema kuwa kiasi cha shilingi bilioni 21.7 zitatumika katika mradi wa kuendeleza na kuhifadhi maliasili katika hifadhi ya Serengeti na shilingi bilioni 46.12, zitatumika katika mradi wa uhifadhi endelevu wa maliasili na mifumo ya Ikolojia ushoroba wa Katavi – Mahale.

Kwa upande wake Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Mhe. Regine Hess, aliahidi kuwa nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha mazingira ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabia nchi ambayo hayaiathiri Tanzania pekee bali Dunia kwa ujumla.

Naye Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (KfW) wa Umoja wa Afrika, Bw. Christoph Tiskens, alisema kuwa Benki hiyo itaendelea kuisaidia Tanzania katika Sekta ya Utalii kwa kuboresha maeneo ya hifadhi pamoja na kuziwezesha jamii zinazozunguka maeneo hayo ili waweze kutunza hifadhi hizo.

Tanzania imekuwa ikinufaika na ufadhili wa Serikali ya Ujerumani katika sekta ya afya, maji, nishati, matumizi endelevu ya maliasili na usimamizi bora wa fedha za umma ambapo kiasi cha shilingi bilioni 678.54 zilitolewa kwa ajili ya miradi inayoendelea kutekelezwa na shilingi bilioni 599.23 kwa miradi iliyokamilika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.