Habari za Punde

Benki ya TADB Yatoa Shilingi .281.74 Kuendeleza Kilimo Nchini.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (Mb), akijibu swali bungeni, jijini Dodoma.

Na. Sandra Charles na Regina Frank, WFM, Dodoma

Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imetoa mikopo yenye jumla ya Shilingi bilioni 281.74 kwa ajili ya kuendeleza miradi ya kilimo, ufugaji na uvuvi nchini kwa wakulima 1,514,695 vikiwemo vyama vya wakulima 151.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni  (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Tabora Kaskazini Mhe. Athumani Almas Maige, aliyetaka kujua riba za Benki ya Kilimo zinatofauti gani na riba za benki za biashara ili kumsaidia mkulima mdogo.

Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) imeweka utaratibu wa kutoza riba ya kiwango kisichozidi asilimia 10 kwa kuzingatia uwezo wa wazalishaji wa madaraja tofauti katika sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi,” alieleza Mhandisi Masauni.

Mhandisi Masauni alisema mikopo inayotolewa kwa wakulima wadogo hutozwa riba nafuu isiyozidi asilimia 10 na kwa masharti nafuu ya urejeshwaji yanayozingatia misimu ya mavuno na mauzo ya mazao.

Sambamba na utoaji wa mikopo ya moja kwa moja, Benki ya maendeleo ya kilimo inasimamia Mfumo wa Dhamana kwa Wakulima Wadogo (Smallholder Credit Guarantee Scheme – SCGS) unaolenga kuchagiza mabenki na taasisi za fedha kuongeza ukopeshaji katika sekta ya kilimo,” alisema Mhandisi Masauni.

Aliongeza kuwa hadi kufikia mwisho wa mwezi Juni 2021, Mfumo wa Dhamana kwa Wakulima Wadogo ilitoa udhamini wa mikopo kwa wakulima wadogo 11,244, vikundi vya wakulima 181 na SMEs 43 waliopata mikopo yenye thamani ya Shilingi bilioni 89.92 kutoka benki 9 washiriki katika uendeshaji wa mfuko huo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.