Habari za Punde

Wizara na Majeshi Wapitisha Mpango wa Muda Mfupi wa Michezo kwa Mashindano ya Kimataifa.

 

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Nasra Mohamed  akifungua kikao cha Kamati ya Kitaifa ya kuendeleza michezo nchini inayojumuisha Wizara ya Sanaa Utamaduni na Michezo, Baraza la Michezo la Majeshi Tanzania (BAMMATA), Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar (BTMZ) leo Oktoba 12, 2021 jijini Dar es Salaam ambapo wamepitisha  mpango wa muda mfupi wa kuandaa  Timu za Michezo za Taifa  zitakazoshiriki  Michezo  ya Jumuiya ya madola nchini Uingereza mapema Julai hadi Agosti 2022.

 Wajumbe wakiwa katika kikao wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Nasra Mohamed (hayupo pichani) akifungua kikao hicho cha Kamati ya Kitaifa ya kuendeleza michezo Nchini.                                     

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Nasra Mohammed akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa mkutano wa Baraza la Michezo la Majeshi Tanzania (BAMMATA) na Wajumbe wa Wizara ya Sanaa Utamaduni na Michezo, baada ya kumalizika kwa mkutano wao.

Kamati ya Kitaifa ya kuendeleza michezo nchini inayojumuisha Wizara ya Sanaa Utamaduni na Michezo, Baraza la Michezo la Majeshi Tanzania (BAMMATA), Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar (BTMZ) leo Oktoba 12, 2021 jijini Dar es Salaam wamepitisha  mpango wa muda mfupi wa kuandaa  Timu za Michezo za Taifa  zitakazoshiriki  Michezo  ya Jumuiya ya madola nchini Uingereza mapema Julai hadi Agosti 2022.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Nasra Mohamed amesema tayari kamati yake imepitisha mpango huo hatua inayofuata ni kupeleka kwa Wizara yenye Sera na dhamana ya michezo nchini ili utekelezaji wake uanze mara moja kulingana na ratiba.

“Ninafuraha kusema kuwa mpango huu umeandaliwa vizuri sana na wataalam wa michezo ni matumaini yetu kabla ya mwezi ujao utakuwa umewasilishwa Wizarani ili tupate baraka na maelekezo yatakayosaidia  utekelezaji wake”. Amefafanua Afande Mohamed

Aidha amesema Kamati imeteua Kamati ndogo ambayo itafanya kazi ya kuainisha mpango unaonyesha timu zitakazoshiriki, vifaa vya michezo, aina ya michezo itakayochezwa, wachezaji wa kila mchezo na kambi kwa ajili ya michezo hiyo ambapo amesema kambi hizo zitatakiwa kuanza rasmi mapema Januari 2022.

“Tumeitaka kamati ndogo kufanya kazi usiku na mchana na kukutana na wataalam wa michezo, mashirikisho na vyama vya michezo kwa kuwa kila mchezo una taratibu zake ”. Amesisitiza Afande Nasra

Naye, Mwenyekiti Mwenza wa kamati hiyo, Addo Komba ambaye ni  Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo kutoka Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo aliyemwakilisha Mkurugenzi wa Michezo amesema uundwaji wa kamati hiyo ya kitaifa utasaidia kuleta  mageuzi makubwa na hatimaye ushindi kwenye mashindano ya kimataifa yatakayoanza  mwakani.

“Kipekee namshukuru Mhe. Rais  kwa maelekezo yake ya kutaka  Vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa kushirikiana na Wizara tukae na kuaundaa  Kamati kwa ajili ya kuboresha michezo nchini ambapo leo  tumeshuhudia  Mpango wa Muda mfupi wa kuandaa Timu za Taifa umekamilika”. Amefafanua Mkurugenzi Komba

Kaimu Katibu wa BMT Neema Msitha amepongeza  kazi kubwa iliyofanywa na kamati ndogo na kutaka bajeti  na  gharama halisi kwa ajili ya mashindano hayo iandaliwe ambapo amesema ikikamilika  italisaidia  taifa kupiga hatua kwenye michezo kama ilivyokuwa kwenye siku za nyuma.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.