Habari za Punde

Watalii Bara na Visiwani Waongezeka Kufikia 922,692

 


 

Na Immaculate Makilika – MAELEZO, Zanzibar

 

Bodi ya Utalii Tanzania Bara (TTB) na Kamisheni ya Utalii Zanzibar (ZCT) zimeendelea kufanyakazi kwa   pamoja katika eneo la Utangazaji wa utalii nchini.

 

Ambapo imeelezwa kuwa, utalii una mchango mkubwa katika uchumi wetu. Takwimu zinaonyesha kuwa kwa mwaka 2019/2020 utalii ulichangia asilimia 17.2 katika pato la Taifa la Tanzania Bara na asilimia 27 upande wa Zanzibar.

 

Akizungumza leo akiwa Visiwani Zanzibar, Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari – MAELEZO, Gerson Msigwa wakati akitoa taarifa ya wiki kuhusu utekelezaji wa miradi ya Serikali katika maeneo mbalimbali nchini, alisema kuwa sekta hii imekumbwa na changamoto kubwa ya Janga la Uviko-19 lakini juhudi za kukabiliana na changamoto hizo zimeendelea kuzaa matunda ambapo mwaka 2020 watalii walikuwa 620,867 na sasa wameongezeka hadi kufikia watalii 922,692 Bara na Visiwani.

 

“Tumepata changamoto ya janga la ugonjwa wa Korona (Uviko-19) ambapo sekta hii imeathirika na kusababisha idadi ya Watalii kushuka kutoka 1,527,230 waliotembelea Tanzania mwaka 2019 hadi 620,867 mwaka 2020. Hata hivyo juhudi tulizozifanya za kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo na kuwavutia zaidi watalii tumefanikiwa kuanza kuongeza idadi ya watalii ambapo katika mwaka 2021 idadi imeongezeka hadi kufikia 922,692,” alisisitiza Msigwa.

 

Aidha amesema kuwa, TTB na ZCT zimeendelea kufanya jitihada mbalimbali katika kuratibu na kushiriki kuandaa maonesho ya Kimataifa ya Utalii, mfano ni Onesho la Utalii la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC Tourism Expo) lililofanyika Arusha kwa mafanikio makubwa na Dubai Expo 2020 ambayo inaendelea huko Dubai.

 

Vilevile, kumekuwepo na ushirikiano wa Sekta Binafsi, Wafanyabiashara wa Sekta ya Utalii wa Bara na Zanzibar (Tour Operators) ambao wanafanya kazi pamoja hasa katika kupokea wageni na kuuza safari kwa wageni wanaokuja kutembelea vivutio  vya utalii nchini.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.