Habari za Punde

MAGUFULI ALIKUWA MCHOYO AU MKARIMU?

 
Na.Adeladius Makwega-DODOMA

Nilipokuwa mwanafunzi wa shule ya msingi nakumbuka katika somo la Kiswahili tulikuwa tukifundishwa mada mojawapo ya kukuza misamiati ya lugha. Hapa tulitakiwa kutaja kinyume cha maneno na neno majawapo ambalo lilikuwa likiulizwa kinyume chake ni neno MCHOYO, ilikuwa tabu sana kupata masahihisho, hapo ndipo nilitambua kinyume cha MCHOYO ni MKARIMU.

Neno Mchoyo linatokana na neno Choyo ni tabia anayokuwa nayo mtu kutotaka na kutoa kitu kwa mtu mwingine. Pia uchoyo unaweza kuitwa kuwa ni UBAHILI, UROHO, UNYIMIVU na UGUMU. Kwa hiyo unapoweka kiambishi M+CHOYO anakuwa mtu mwenye tabia hizo.

Neno Mkarimu linatokana na neno Karimu ni tabia ya mtu kutoa na kuwasaidia watu wengine/mtu mwenye tabia hizo. Pia inamaanisha enye KUTOA au KUKIRIMU.

Mwanakwetu leo kwanini ninayakumbuka haya? Julai 2, 2022 nilijifunza jambo moja kubwa kutoka jamii kwa wakazi wa Chamwino Ikulu, mkoani Dodoma.

“Ndugu yangu kanisa langu ninalosalia haina hadhi yangu naombeni msaaada tunataka kuliboresha sasa naomba mchango wako.” Nilimsikia kwa masikio yangu akipiga simu kwa marafiki zake wakati tunaanza ujenzi wa kanisa letu, alisema ndugu mmoja mtoa ushuhuda ambaye alikuwepo siku hiyo.

Kweli simu zake zote alizopiga kwa watu kadhaa zilizaa matunda na tukaweza kujenga kanisa letu hadi leo hii linaonekana namna lilivyo.

Ndugu yetu huyu hakuishia kujenga kanisa lake tu bali, mbinu hiyo hiyo ilitumika kuujenga msikiti kando na eneo letu ambapo lipo umbali mchache kutoka Ikulu ya Chamwino na kweli ndoto ya kuwa na majengo ya ibada ilikamilika kwa baadhi ya dini na madhehebu.

“Wengine wanaweza kudhani kwa kuwa alikuwa rais basi alikuwa akihomola (akichota) pesa kutoka huko serikalini akatoa ili tujenge kanisa na huu msikiti la hasha hilo hatukulishuhudia, bali masikio yetu yalisikia sauti ya simu zilizopigwa kwa watu mbalimbali na macho yetu kuona watu hao kuchangia nyumba hizi za ibada kila walipojulishwa.” Alisema ndugu huyu.

Kiu ya walio wengi kutoka madhehebu ambayo hayakujaliwa kunufaika na harambee zake ilikuwa je akimaliza msikiti atasaidia dini au dhehebu lipi? Hapa Chamwino Ikulu. Bilauli hiyo yenye maji ya kukata kitu kwa dini na madhehebu yaliyosalia hapa Chamwino Ikulu ilizikwa kaburini kwake huko Chato mkoani Geita.

Swali ambalo ninakuacha nalo msomaji wangu kwa leo ni Je Magufuli alikuwa mchoyo au mkarimu?

Nina hakika msomaji wangu jibu lako unalo.

makwadeladius@gmail.com

 0717649257.

1 comment:

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.