Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi amefanya mazungumzo na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje wa Oman anayeshughulikia
Fedha na Utawala Mohammed Nasser Al Wahaibi na kumueleza kwamba Zanzibar
inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya pande mbili
hizo.
Mazungumzo hayo yalifanyika leo Ikulu Zanzibar wakati Rais Dk. Mwinyi alipokutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman anayeshughulikia Fedha na Utawala Mohammed Nasser Al Wahaibi akiwa amefuatana na ujumbe wake akiwemo Balozi wa Oman nchini Tanzania Saud Hilal Al Shidhani.
Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi alimueleza Katibu Mkuu Mohammed Nasser Al Wahaibi kwamba kwa kiasi kikubwa Oman imeweza kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya afya, elimu na mengineyo bila ya kusahau hatua ya nchi hiyo kusaidia ujenzi wa jengo la Beit al Jaib.
Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza
uhusiano na ushirikiano huo kwa kutambua kwamba Oman ni mshirika mkubwa wa
maendeleo ya Zanzibar.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Mwinyi alieleza haja ya kuwepo kwa
mashirikiano kwa sekta binafsi kati ya pande mbili ili kuweza kutoa fursa mbali
mbali za maendeleo hasa ikizingatiwa umuhimu wa sekta hiyo katika maendeleo.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alimueleza Waziri huyo juhudi zinazochukuliwa
na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwaletea maendeleo wananchi wake
huku akipongeza hatua za nchi hiyo kuendelea kuziunga mkono juhudi hizo.
Nae Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje wa Oman anayeshughulikia Fedha na Utawala
Mohammed Nasser Al Wahaibi alimueleza Rais Dk. Mwinyi kwamba Oman inatambua
uhusiano na ushirikiano wa kihistroa uliopo kati yake na Zanzibar na kuahidi
kuziendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.
Katibu Mkuu Wizara Mohammed Nasser Al Wahaibi alisema kuwa nchi ya Oman kwa
kupitia Balozi zake hapa nchini zitaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika
kuendeleza na kuimarisha sekta zake za maendeleo.
Pia, alitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa kuishirikisha sekta
binafsi katika maendeleo jamabo ambalo limeweza ksuaidia kwa kiasi kikubwa
kusukuma uchumi na medneleo nchini Oman.
Katika mazungumzo hayo, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje wa Oman
anayeshughulikia Fedha na Utawala Mohammed Nasser Al Wahaibi alizipongeza
juhudi za makusudi zinazoendelea kuchukuliwa na Rais Dk. Mwinyi katika
kuwaletea maendeleo endelevu wananchi wa Zanzibar.
Aidha, Katibu Mkuu huyo alimpa salamu Rais Dk. Mwinyi zilizotoka kwa Sultan
wa Oman Haitham bin Tariq Al Said ikiwa ni pamoja na kueleza namna nchi hiyo
itakavyoendelea kuunga mkono vipaumbele vilivyowekwa na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kwa ajili ya maendeleo ya Wazanzibari.
Wakati huo huo, Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi
anatarajiwa kuendelea na ziara yake kisiwani Pemba hapo kesho (Julai 25,2022)
ikiwa ni pamoja na kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbali mbali
ya maendeleo ikiwemo inayotekelezwa kwa fedha za ahuweni ya UVIKO -19.
Imetayarishwa
na Idara ya Mawasiliano,
Ikulu Zanzibar.
No comments:
Post a Comment