Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi alizungumza na Balozi na
Naibu Mwakilishi wa Kudumu Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Dkt. Suleiman
Haji aliefika Ikulu kumuaga.
Alimtaka Balozi huyo kuangalia fursa zitakazopatikana katika kituo chake cha kazi na kusaidia kuinua uchumi wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kupitia nyanja mbali mbali, ikiwemo ya Uwekezaji pamoja na ile ya kujenga uwezo.
Alisema Kituo hicho kina fursa pana kutokana na kutembelewa na watu kutoka Mataifa mbali mbali Duniani, hivyo akamtaka kuikumbuka Zanzibar kwa jicho la pekee.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imefarijika sana na Uwakilishi wa Balozi huyo katika kituo hicho.
Mapema, Balozi na Naibu Mwakilishi wa Kudumu Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa Dkt. Suleiman Haji aliahidi kutumia nguvu, maarifa na juhudi zake zote ili kutekeleza vyema majukumu yake na kuiletea Maendeleo Tanzania.
Alitoa shukrani za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi kwa uteuzi wake wa kushika wadhifa huo.
Katika hatua nyengine akizungumza na waandishi wa habari, Mwakilishi huyo ambae muda mfupi ujao anatarajiwa kuripoti katika Kituo chake cha kazi Jijiji New York Marekani, alisema kituo hicho kina fursa nyingi zinazoweza kuinufaisha Tanzania endapo zitatumika vizuri, ikiwemo suala la ufadhili katiika sekta ya Uchumi wa Buluu ambapo wavuvi, wafanya biashara na wakulima wa mwani wataweza kunufaika.
Alilitaja eneo jengine ambalo Zanzibar, ikiwa nchi ya Kisiwa itaweza kunufaika ni upatikanaji wa fedha katika kukabiliana na athari za kimazingira, akibainisha maeneo mbali mbali ya Visiiwa vya Unguja na Pemba kukabiliwa na hali mbaya ya kimazingira kutoka na uvamizi wa maji chumvi.
Aidha, alisema anakusudia kufanya juhudi ili kuhakikisha Watalii wa madaraja ya juu kutoka Marekani wanakuja nchini, na hivyo akatumia fursa hiyo kuitaka Serikali kujipanga kwa kuwa na miundo mbinu bora ili kuvutia watalii hao.
Balozi Suleiman alisema Wa-Tanzania wana fursa pana ya kufundisha Lugha ya Kiswahili nchini Marekani kwa kuzingatia uwepo wa Vyuo vikuu kadhaa vinavyohitaji huduma hizo, hivyo akaiomba Serikali kupitia Baraza la kiswahili (BAKIZA) kujidhatiti katika suala la kuzalisha walimu wengi wenye uwezo wa kufundisha lugha hiyo.
Imetayarishwa na Idaya ya Mawasiliano
Ikulu Zanzibar.
.
No comments:
Post a Comment