Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amefunga mafunzo ya siku tano ya kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea ndani na nje ya Bara la Afrika uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika mafunzo hayo Mhe. Masanja
amesema kuwa mafunzo hayo yametoa mbinu za kuhakikisha hifadhi zinahifadhiwa
vizuri ili kulinda wanyamapori na kuendeleza utalii.
“Wataalamu wa masuala ya uchunguzi wamejifunza
mbinu za kuzuia uharibifu wowote unaoweza kutokea kwenye maeneo ya hifadhi katika
nchi wanachama wa Mkataba wa Lusaka (Lusaka Agreement)”.
Amesema mafunzo hayo yameshafanyika katika nchi
za Tanzania, Kenya na Uganda na Tanzania itaendelea kushiriki kama nchi
mwanachama ili kuzilinda hifadhi na wakati huohuo kuendeleza utalii.
Naye, Mkurugenzi Msaidizi wa Kuzuia Ujangili, Wizara
ya Maliasili na Utalii, Bw.Robert Mande amesema kuwa mafunzo hayo yataendelea
kufanyika ili kutekeleza sera za Serikali za kuendeleza uhifadhi.
“Lazima tuhakikishe kuwa tunalinda rasilimali
za wanyamapori ili watalii wanavyokuja waweze kuziona na waweze kuwa na
usalama”Mande amefafanua.
Ameongeza kuwa washiriki zaidi ya 21 kutoka
nchi wanachama wamejengewa uwezo katika masuala ya uchunguzi, upelelezi,
intelijensia na uendeshaji mashitaka ili waweze kufikia viwango vya umahiri
mkubwa kwa sababu makosa ya ujangili yanavuka mipaka ya nchi na yanahitaji ushirikiano na vyombo vingine
vya nje ya nchi.
Kwa upande wake Mshiriki wa Mafunzo kutoka
nchini Kenya, Bw. Jami Yamina amesema mafunzo hayo yametoa mbinu mbalimbali za
kutumia ili kuwakamata majangili na kuzikamata mali zao na kuziwasilisha
mahakamani.
“Tukiweza kuwakamata hawa majangili tutakuwa
tumefanikiwa kuzuia biashara hii haramu ya wanyamapori ” amesisitiza.
Mafunzo hayo yamehudhuriwa na wataalamu
wanachama wa Lusaka Agreement (unaojihusisha na kuzuia uuzaji, usafirishaji
wa wanyamapori pamoja na mimea) Grace Farm Foundation, US
Homeland Security na washiriki kutoka nchini Uganda, Kenya na Tanzania.
No comments:
Post a Comment