Habari za Punde

Rais Dk Hussein Mwinyi aishukuru Jumuiya ya Ulaya (EU) kwa ufadhili wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo

 


STATE HOUSE ZANZIBAR

OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

PRESS RELEASE

 

Zanzibar                                                                                10 Agosti,2022

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Dk. Hussein Ali Mwinyi ameishukuru Jumuiya ya Ulaya (EU) kwa Zanzibar kuwa miongoni mwa maeneo yatakayopata misaada kutoka Jumuiya hiyo  kwa ajili ya kuendeleza miradi mbali mbali ya Maendeleo.

 

Dk. Mwinyi ametoa shukrani hizo alipozungumza na Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji  Jestas Abouk Nyamanga , aliefika Ikulu Zanzibar kwa kujitambulisha pamoja na mazungumzo mafupi.

 

Amesema ni jambo jema kwa Zanzibar, hususan kisiwa Cha Pemba  kuwa miongoni mwa maeneo ambapo miradi mbali mbali ya maendeleo itatekelezwa chini ya Ufadhili wa EU  hapa Tanzania, ikiwemo mradi wa ‘kuboresha mtazamo wa Majiji’ (green City), ambao unakusudiwa kutekelezwa katika miji mitatu ya Tanzania ya Tanga, Mwanza na Pemba.

 

Alisema tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya nane, yenye mfumo wa Umoja wa Kitaifa (GNU), kumekuwepo dalili za EU kurejesha Uhusiano wake na Zanzibar kufuatia kuwepo kwa Demokrasia.

 

Aidha, Dk.Mwinyi alieleza kuwa Utalii ni sekta kuu ya Uchumi wa Zanzibar, na kusema Zanzibar imejipanga kuimarisha sekta hiyo  baada ya kuathirika kutokana na  Ugonjwa wa Covid-19.

 

Alimtaka Balozi huyo kuendeleza mazungumzo  na mamalaka zinazosimamia Utalii nchini Ubelgiji ili kufanikisha lengo la kuwepo safari za ndege za moja kutoka Ubelgiji hadi Zanzibar na hivyo kuleta matumaini ya kuongeza ujio wa Watalii  hapa nchini.

 

Akigusia suala la kuwepo fursa za Biashara nchini Ubelgiji, Dk. Mwinyi alisema Diplomasia ya Uchumi inazingatia umuhimu wa kuangalia fursa za biashara, hivyo akasema pamoja na kuwepo changamoto mbali mbali katika utayarishaji wa Dagaa kwa wajasiriamali hapa nchini, Serikali itaishughulikia changamoto hiyo hatimae fursa hiyo iweze kutumika ipasavyo.

 

Alisema Zanzibar imekuwa ikishughulikia miradi mbali mbali  kwa ajili ya maendeleo, hivyo  kuwepo kwa taasisi zinazotoa mikopo nafuu ni jambo jema  na kubainisha namna Serikali itazingatia namna itakavyoweza kupata  mikopo hiyo kupitia mashirika hayo ya Fedha yaliopo EU.

 

Aidha, alisema Zanzibar itashukuru kupata fedha za mkopo kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu kupitia sekta ya uchumi wa Buluu.

 

Mapema Balozi wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania nchini Ubelgiji, ambapo pia anaiwakilisha Tanzania nchini Luxenbourg na Jumuiya Umoja wa Ulaya (EU Jestas Abouk Nyamanga amesema kuanza kwa safari za moja kwa moja za ndege kati ya Ubelgiji na Zanzibar kuanzia mwezi Oktoba mwaka huu, kutaongeza idadi ya  Watalii watakaozuru nchini.

 

Alisema mawasiliano yamefanyika kuona kunakuwepo usafiri wa  ndege ya moja kwa moja kati ya Ubelgiji – Zanzibar  kwa wastani wa mara mbili kwa wiki na hivyo kuongeza idadi ya ujio wa Watalii baada ya kuathirika kutokana na Ugonjwa wa Covid -19, ambapo kabla ya ugonjwa huo wastani wa  watalii 16,000 walikuwaa wakizuru nchini kila mwaka.

 

Alisema katika mazingira ya sasa Watalii kutoka nchi hiyo hutumia Shirika la Ndege la Qatar, jambo ambalo lina changamoto mbali mbali.

 

Aidha, alisema nchi hiyo ina fursa mbali mbali za msomo ya juu, hususan katika kiwango cha Master na PHD, hivyo akatoa wito kwa Vyuo vikuu vya Zanzibar,  ikiwemo SUZA pamoaj na wananchi wengine wenye uwezo kuhamasika ili kutumia fursa ziliopo.

 

Balozi Nyamanga alisema mahusiano kati ya Tanzania na Ubelgiji yameimarika na kubainisha fursa kadhaa za kibiashara, ambapo  Tanzania inaweza kufanya, ikiwemo kuuza minofu ya samaki, dagaaa, mbogamboga, mchele pamoja na viungo vya aina mbali mbali.

 

Alisema Zanzibar inaweza kunufaika na fursa hiyo kupitia uuzaji wa Dagaa, mkazo ukiwekwa katika utayarishaji na uhifadhi bora wa dagaa hilo ili kuliongezea thamani, pamoja na usafirishaji  wa viungo ikiwemo Pilipili.

 

Kuhusiana na Uwekezaji, Balozi Nyamanga alisema  Luxembourg ni kituo kikuu cha  Mashirika ya Fedha pamoja na Mabenki , huku akibainisha kuwepo  Kampuni zinazoonyesha nia ya kutoa mikopo nafuu kwa Zanzibar, hivyo akaiomba Serikali kubainisha maeneo yanayoweza kutumika.

 

Akizungumzia mahusiano ya Tanzania na Jumuiya Umoja wa Ulaya, Balozi Nyamanga alisema kuwa ni mazuri, ambapo EU imekwua ikiendelea kutoa misaada, hususan ya kifedha kwa Tanzania.

 

Alisema EU imetenga kiasi cha Euro Milioni 554 kwa Tanzania ili kuiwezesha kuingia katika soko la Ulaya pamoja na Euro Milioni kumi kwa ajili ya kuimarisha uzalishaji wa Asali ya Nyuki.

 

Aliitaja mikoa  ya Katavi, Rukwa, Tabora, Dodoma na Pemba kuwa  itanufaika na msaada huo, lengo likiwa ni kuzalisha asali yenye viwango .

 

Aidha, alieleza kuwa katika kipindi cha mwaka 2021 – 2027 EU imeahidi kusaidia Tanzania kiasi cha Euro Milioni 425, ambapo Euro Milioni 703 zimelengwa katika uboreshaji wa mitazamo ya Majiji (green city) katika miji mitatu ya Tanga, Mwanza pamoja na Pemba.

 

Alisema fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuimarisha miundo mbinu pamoja na masoko katika miji hiyo.

 

Aidha, Balozi huyo aliishukuru Serikali kwa kutilia mkazo   uimarishaji wa sekta ya Uchumi wa Buluu, akibainisha kiasi cha Euro Milioni 140 zilizotengwa na Jumuiya hiyo kwa ajili ya uimarishaji wa Uchumi wa Buluu ambapo miongoni mwa matumizi yake yatahusisha mikopo kupitia Sekta binafsi.

 

WAKATI HUO HUO; Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi alikuwa na mazungumzo na Balozi wa Ethiopia nchini Tanzania Shibu Mamo Kedida.

 

Katika mazungumzo hayo yaliofanyika Ikulu Zanzibar viongozi hao  walizungumzia haja ya kuendeleeza mahusiano na mashirikiano ya kihistoria kati ya Zanzibar na Ethiopia katika njanja mbali mbali  kwa maslahi ya Mataifa hayo na wananchi wake.

 

Miongoni mwa maeneo ya mashirikiano yaliogusiwa ni pamoja na Utalii, Michezo, utamaduni, masuala ya Anga pamoja na elimu.

 

  

Imetayarishwa na Idaya ya Mawasiliano

Ikulu Zanzibar.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.