Habari za Punde

Watendaji wakuu watakiwa kusimamia ipasavyo watendaji wao ili kuleta ufanisi


 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na Makatibu na Manaibu Makatibu Wakuu wa Wizara za Serikali ya Mapinduzi katika Kikao Kazi kilichofanyika  Afisini kwake Vuga Jijini Zanzibar.

Na Ally Mohammed, OMPR

Watendaji Wakuu wa Taasisi za Serikali wametakiwa kusimamia ipasavyo watendaji walio chini yao na kutatua changamoto zilizopo ili kuleta ufanisi mzuri wa kazi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ametoa Agizo hilo katika Kikao Kazi kilichowakutanisha Makatibu Wakuu na manaibu Katibu wakuu wa Wizara za Serikali ya Mapinduzi kilichofanyika  Afisini kwake Vuga Jijini Zanzibar.

Amesema Makatibu Wakuu ndio Watendaji Wakuu wa Serikali hivyo ni vyema kusimamia ipasavyo ukusanyaji na utumiaji wa Fedha za Serikali kwa Maslahi ya Umma.

Aidha Mhe. Hemed amewataka Makatibu Wakuu kusimamia Watumishi na kufuata utaratibu uliowekwa Kisheria kwa Watumishi na kuchukua hatua Stahiki hasa kwenye Vitengo vya Manunuzi na Wahasibu ili kuhakikisha Fedha za Serikali hazipotei na kuishia Mikononi mwa wachache.

Pia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewataka Makatibu Wakuu hao kusimamia ipasavyo ukusanyaji wa Mapato kwa Taasisi zao ili Serikali iweze kufikia Malengo iliyojipangia kwenye Bajeti ya Serikali na kufanya mambo yake ya kimaendeleo kwa Wananchi wake kwani ukusanyaji wa Mapato kwa sasa bado hairidhishi.

Mhe. Hemed amewataka Watendaji hao kuacha Muhali kwa watendaji walio chini yao na kutomuonea yoyote bali kila Katibu Mkuu afuate Wajibu wake na kuwataka kufuata Sheria iliyopo kwa Watumishi Serikalini na kuamua kwa mujibu wa Sheria hizo.

Akigusia Suala la Nidhamu Serikalini Mhe. Hemed amewataka Makatibu Wakuu hao kwenda kusimamia Watendaji ambao hawawajibiki ipasavyo na kuwatolea Taarifa za haraka wale wote ambao hawapo kwenye Mamlaka zao ili Serikali iweze kuchukua hatua na wale ambao wapo kwenye Mamlaka zao ni lazima wawachukulie hatua stahiki kulingana na Sheria ya Utumishi inavyosema.

“Kuna Watumishi hawaji kazini, kuna watumishi wanapokea pesa bila ya kufanya kazi ya aina yeyote kuna watumishi wasiokuwa  na nidhamu  chukuweni hatua na sio kila mtumishi anaeharibu munamrejesha utumishi bila ya maelezo yeyote, chukueni hatua”

Sambamba na hayo Mhe. Hemed amewataka watendaji hao kuondosha Malalamiko yaliyopo kwa Watumishi wao na kusimamia haki za wafanyakazi ili kuleta ufanisi mkubwa wa kazi

“Ni lazima Wakurugenzi Utumishi kukaa na wafanyakazi wao kuwapa elimu na kuwasikiliza shida zao na kuweza kuzitafutia ufumbuzi stahiki ili na wao waone kuwa serikali inawajali”

Mhe. Hemed amewataka Makatibu Wakuu kuongeza ushirikiano na kuimarisha Mawasiliano baina yao na  Watendaji wa chini ili kuimarisha utendaji wa kazi Serikalini.

Akigusia suala la ajira zilizotangazwa hivi karibuni Mhe, Hemed amemtaka Katibu Mkuu Utumishi wa Umma kukamilisha mchakato huo wa kuwafatilia walioomba nafasi hizo za walimu na madaktari ili kuondosha chanagamoto ambapo serikali imepanga kuwaondoshea wananchi changamoto zote zinazowakabili ikiwemo skuli na hospitali.

Pia ameitaka Wizara ya Afya kuajiri madaktari wataalamu ili kuweza kufanya kazi za kitaalamu kwenye mahospitali ambayo yanatarajiwa kufunguliwa hivi karibuni

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.