Habari za Punde

Ipo Haja kwa Wasaidizi wa Sheria wa Wilaya Kupatiwa Mafunzo ya kuondosha Vitendo vya ukatili wa Jinsia kwa Wazee na Watoto

Na Maulid Yussuf WMJJWW  Zanzibar

Mkurugenzi  wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto Bi Siti  Abbas Ali amesema  ipo  haja  kwa  Wasaidizi  wa   Sheria  wa Wilaya  zote kupatiwa  Mafunzo ya  kuondosha  Vitendo  vya ukatili wa Jinsia  kwa Wazee  na watoto ili kusaidia kupunguza vitendo hivyo nchini.

Bi Siti ameyasema hayo wakati akifungua   mkutano wa  siku moja wa mrejesho  wa vikundi kazi  vya Wasaidizi wa Sheria  vya Wilaya  zote  za Unguja katika kupambana na vitendo vya ukatili na udhalilishaji kijinsia, katika ukumbi wa Bima uliopo  Mpirani Unguja.

Amesema wananchi wengi  wamepata uwelewa  juu ya masuala ya  Vitendo  vya udhalilishaji  wa kijinsia na wamekuwa na mwamko wa kuviripoti katika sehemu  mbalimbali,  kutokana na juhudi  za Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na watoto katika kutoa elimu pamoja na kutoa  msaada wa kisheria.

Amesema Wananchi wanahaki  ya kupewa  elimu ya kujikinga  na  vitendo  hivyo  vya udhalilishaji  na kuwataka  Wazee kukaa pamoja na  watoto wao kuwaelimisha na kufatilia nyendo   za  watoto wao ili kuwatambua pale watakapopatwa na tatizo lolote ikiwemo la udhalilishaji.

Aidha Mkurugenzi Siti amesifu kazi nzuri inyofanywa na wasaidizi wa sheria wa Wilaya zote na kuwaahidi kulipatia ufunmbuzi tatizo lao ya posho ili liweze kuwasaidia katika kujikimu kimaisha.

Pia ameitaka Wizara kuhakikisha inawapatia Elimu ya kisheria katika vipengele muhimu ili viweze kuwasaidia katika utendaji mzuri wa kazi zao.

Wakiwasilisha ripoti ya mpango kazi katika kipindi cha mwezi wa Octoba hadi disemba, baadhi ya wasaidizi wa sheria wa Wilaya mbalimbali wamesema pamoja na mipango waliyojiwekea kafika utekelezaji wao, wameona kuwepo mizozo katika ndoa hali inayopelekea talaka za kiholela na kupelekea watoto kusambaratika.

Hivyo wameshauri elimu ya ndoa izidi kutolewa kwa wale wanojiandaa kufunga ndoa ili kupunguza talaka za kiholela pamoja na udhalilishaji wa wanawake na watoto. 

Nao  wasaidizi wa Sheria wameomba kupatiwa posho kwa wakati pamoja na kuwataka masheha kusimamia suala la kupiga miziki hadi usiku wa manane kwani ni miongoni mwa  vichocheo  vva  vitendo vya udhalishaji.

Wamesema mafanikio mengi yamepatikana kupitia taluma wanayoitoa katika Skuli, mikutanoni, na sehemu za mikusanyiko ya watu lakini changamoto nyingi zimekuwa zikijitokeza ikiwemo  badhi ya Wazee  kukosa muda wa kuzungumza na watoto wao majumbani jambo ambalo linarejesha nyuma jitihada  zao.

Pia uelewa  mdogo juu ya utaratibu wa kesi za Mahakamani namna ya kuripotiwa  kesi hizo pamoja na kuoneana  muhali katika  kutoa  ushahidi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.