Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Azungumza na Balozi wa Marekani Nchini Tanzania

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Balozi wa Marekani Nchini Tanzania Mhe.Michael Mattle,alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwa katika picha ya pa moja na Mgeni wake Balozi wa Marekani Nchini Tanzania Mhe.Michael Mattle,baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwa na mgeni wake Balozi wa Marekani Nchini Tanzania Mhe.Michael Mattle, akimshindikia baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema imeweka kipaumbele zaidi kuimaisha miundombinu ikiwemo barabara safi zenye kiwango cha lami kwa mji miji yote ya Zanzibar ili kurahisisha sekta ya biashara na kuwavutia wawekezaji zaidi nchini.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Michael Battle, aliefika kujitambulisha.

Dk. Mwinyi, pia ameikaribisha Marekani kuangalia fursa za biashara na uwekezaji katika kuimarisha uhusiano wao mwema utakaofungua milango ya fursa nyinyi za ajira kwa wananchi wa Zanzibar.

Akizungumzia sera ya Uchumi wa Buluu, Rais Dk. Mwinyi alimueleza Balozi Battle kwamba Zanzibar imejaaliwa bahari nyenye fursa nyingi za uwekezaji na biashara kupitia sekta ya utalii endelevu, uvuvi pamoja kilimo cha mwani.

Alisema sekta ya Uchumi wa buluu pia ina fursa za utalii wa ufukweni, utalii wa michezo ambako pia aliikaribisha Marekani kuangalia maeneo hayo kwaajili ya uwekezaji na kuimarisha uhusiano wao utakaolenga kukuza uchumi kwa watu wa pande mbili hizo.

Alisema, uhisusiano wa diplomasia baina ya Tanzania na Marekani ni wa muda mrefu pia alieleza Zanzibar ikiwa sehemu ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, imefaidika na uhusiano huo hasa kupitia sekta za Afya na Elimu.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Balozi Michael Battle ameisifu Zanzibar kwa kubarikiwa visiwa vyenye rasilimali nyingi za Uchumi.

Balozi Battle alimueleza Rais Dk. Mwinyi, dhamira ya Marekani kuwekeza kwenye biashara kwani wanajivunia kuwa na raia wengi, Tanzania.

Pia, alisema fursa ya kuwekeza Zanzibar, itafungua ajira nyingi kwa Wazanzibari na Wamareakani waliopo, kuongeza mitaji na kuboresha ustawi wa watu wa Tanzania na Marekani waliopo Zanzibar.

Hata hivyo, Balozi Battle alitumia fursa hiyo, kuipongeza Tanzania kwa kutimiza miaka 59 ya Muungano baina ya Zanzibar na Tanganyika, alisifu ni Muungano wa Mfano kwa dunia ya sasa.

Uhusiano wa Diplomasia baina ya Tanzania na Marekani ulianza zaidi ya miaka 50 iliyopita kwa mataifa mawili hayo kushirikina kwenye masuala mbalimbali ya maendeleo, jamii na uchumi.

Tanzania ina ubalozi wake nchini Marekani kwenye mji mkuu wa nchini hiyo, Washington DC, ambapo Balozi, Elsie Sia Kanza ni Balozi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania anaeiwakilisha Tanzania kwa Marekani na Mexico.

Marekani iko Kaskazini mwa bara Amerika, inapakana na nchi ya Canada kwa upande wa Kaskazini na Kusini ipo jirani na Mexico.

Taifa la Marekani lina idadi ya watu milioni 333, ni nchi ya tatu kwa ukubwa duniani, inashirikiana mipaka ya bahari na visiwa vya Bahamas, Cuba, nchi ya Urusi na mataifa mengine. New York ni jiji kubwa la biashara nchini humo.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.