Habari za Punde

Tabora Kuwa Kinara wa Programu ya BBT Mifugo Nchini - ULEGA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akiongea na Wanakijiji cha Uganza (hawapo pichani) alifanya mkutano wa hadhara katika Kijiji hicho Wilayani Kaliua, mkoani Tabora.

Sehemu ya Wanakijiji cha Uganza wakimsikiliza Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega(hayupo pichani) wakati akihutubia hadhara hiyo katika mkutano aliyoufanya katika Kijiji cha Uganza, Wilayani Kaliua, mkoani Tabora. 
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega akimsikiliza mkazi wa Kijiji cha Uganza, Wilayani Kaliua, Bw. Dogan Budeba alipofanya ziara ya kikazi Wilayani Kaliua, Mkoani Tabora

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema kufuatia Mkoa wa Tabora kuongoza kwa  kuwa na idadi kubwa ya mifugo hapa nchini wamepanga kuanzisha programu kabambe ya BBT Mifugo itakayowawezesha vijana kunenepesha mifugo na  kuufanya mkoa huo kuwa kinara na lango kuu la kuuza nyama bora ndani na nje ya nchi.

Waziri Ulega aliyasema hayo katika mkutano wa hadhara aliyoufanya Wilayani Kaliua mkoani Tabora Mei 31, 2023. 

Alisema Tabora ni mkoa uliobarikiwa kuwa na eneo kubwa la ardhi na rasilimali nyingi ya mifugo hivyo anaona mkoa huo una kila sababu ya kuwa kinara wa kufanya biashara ya mifugo.

"Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, tunataka kuufanya mkoa wa Tabora kuwa ndio lango la kuvunia mifugo, vijana wawekeze kwenye mnyororo wa thamani wa uzalishaji wa mifugo na mazao yake ili waweze kuuza nyama  ndani na nje ya nchi, na wakiweza kufanya hivyo watakuza kipato chao na Taifa kwa ujumla", alisema

"Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa, sisi tupo tayari kuanzisha programu ya BBT hapa Tabora  kwa sababu rasilimali ipo ya kutosha hivyo ni rahisi kupata matokeo kwa haraka, muhimu ni kuifungamanisha rasilimali hiyo katika mnyororo wa thamani kuanzia uzalishaji mpaka katika masoko", alifafanua

Alisema kwa kuwa programu hiyo walishaianzisha katika Mikoa ya Mwanza, Kagera na Tanga hivyo ni rahisi kuanzisha pia mkoani Tabora, na mipango ni kuifanya BBT Mifugo ya Tabora kuwa ya kwanza katika ufugaji bora na uuzaji wa nyama.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Balozi. Dkt. Batilda Burian alimshukuru Waziri Ulega kwa mipango hiyo, huku akimuhakikishia kuwa tayari wana eneo la hekari 6000 lililopo Wilayani Kaliua  ambalo watalitumia kwa ajili ya programu hiyo ya BBT Mifugo.

Aidha, alisema pia kuna hekari nyingine 40,000 ambazo zipo Wilayani Nzega ambazo watazitumia pia kufanya ufugaji wa kisasa ikiwemo kulima malisho kwa ajili ya mifugo yao na kuuza ndani na nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.