RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameiagiza kamati ya kuzuia udhalilishaji wa kijinsia Zanzibar, iangalie suala la matumizi na athari za mitandao kwa vijana ili serikali
ijipange vyema na kwenye mwelekeo wa uhuru wa matumizi hayo kwa Zanzibar.
Dk. Mwinyi aliyasema hayo kwenye hafla ya uzinduzi wa kamati ya kuzuia udhalilishaji wa kijinsia
Zanzibar huko ukumbi wa Sheikh Idriss Abdul Wakili, Kikwajuni Wilaya ya mjini.
Alisema, mitandao inapotumiwa vibaya ni kishawishi kimojawapo cha mmong’onyoko
wa maadili na vitendo vya udhalilishaji.
“Naiagiza Kamati hii ifanye kazi
ya kuchunguza athari za matumizi ya mitandao ya kijamii na ongezeko la kesi za
udhalilishaji, baada ya kufanya kazi hiyo, itoe ushauri na mapendekezo
Serikalini ili tuwe na muelekeo bora zaidi juu ya uhuru na matumizi ya mitandao
hapa Zanzibar”. Aliagiza Dk. Mwinyi.
Alieleza furaha yake kuona Kamati hio imeundwa ikiwa na lengo la kuzuia
matukio ya udhalilishaji kabla ya kutokea, badala ya kupambana nayo yakiwa
yameshaathiri jamii.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi aliitaka Kamati hiyo iangalie mapungufu ya
Kisera, Sheria na Kanuni yaliopo ili watoe mapendekezo sambamba na kuweka malengo
ya kimkakati yatakayowawezesha kufanya kazi kwa kasi na haraka zaidi.
“Kwa vile ndani ya Kamati hii, wamo viongozi na wajumbe kutoka taasisi
za elimu ya sekula na elimu ya dini, ninayo matumaini kwamba kamati hii itakuja
na mapendekezo yatakayohusisha mitaala pamoja na uendeshaji na usimamizi mzuri
wa skuli, madrasa na maeneo mengine yanayotoa mafunzo ya dini” alitanabahisha
Dk. Mwinyi.
Katika hatua nyengine Rais Dk. Mwinyi alisema Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar inafarijika kuona jamii imesimama pamoja kuungamkono juhudi za Serikali
kivitendo.
“Sote tunasimama pamoja kupiga vita janga la udhalilishaji wa watoto na
unyanyasaji wa kijinsia. Hii ni ishara kwamba sote tunaguswa na uzito wa janga
hili kwa kuzingatia madhara yake. Endapo vitendo hivi tutashindwa kuwa na mbinu
mwafaka za kuvikabili, jamii yetu itakuwa na idadi kubwa ya washtakiwa wa
makosa ya udhalilishaji”. Alitanabahisha Dk. Mwinyi.
Aliongeza kuwepo kwa tatizo la idadi kubwa ya watu wanaofungwa kwa kesi
za udhalilishaji inaifanya jamii yetu kuwa na familia zinazokosa matunzo, hali
aliyoieleza kusababisha mifarakano na kusalia kuwepo kwa kundi kubwa la watoto
wanaokosa usimamizi wa familia zilizo madhubuti.
Hivyo, aliwataka wazazi na walezi wajitahidi kusimamia vyema maadili, hulka
na silka za vijana wao na kuhakikisha wanawalinda na kuwawekea mipaka sahihi
kwa kutowapa uhuru sana pamoja na kufuatilia
mabadiliko ya tabia na mienendo yao ya kila siku kwani kesi nyingi za
udhalilishaji wa kijinsia zilizopo kwenye vyombo vya sheria zinawahusisha
vijana.
Alisema watoto na vijana wanaofanyiwa udhalilishaji huathirika kiafya
na kisaikolojia, hali aliyoieleza kuchangia kuharibu mipango na muelekeo wao wa
maisha.
Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar, Mwl.
Haroun Ali Suleiman alisema kazi ilio mbele yao kamati aliyoizundua Rais Dk.
Mwinyi ni utekelezaji wa vitendo katika juhudi za kumuungamono Rais katika
mapambano dhidi ya udhalilishaji Zanzibar.
Naye, Mkurugenzi wa Mashitaka Zanzibar, (DPP)
Mgeni Jailani Jecha alisema vitendo vya udhalilishaji wa kijinsini vinazidi
kuongezeka nchini badala ya kupungua.
Alieleza kwamba vinaweza kuimaliza jamii, jambo
ambalo linazidi kuleta hofu na kutia dosari taifa
IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment