Habari za Punde

Rais Dk Hussein Mwinyi ahimiza tafiti kwenye elimu

 

                                                                                                       21 Julai, 2023

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, amehimiza jamii kufanya utafiti kwenye nyanja mbalimbali ili kutanua wigo na kukuza elimu kupitia sekta za maendeleo.

Al hajj Dk. Mwinyi alitoa nasaha hizo kwenye Masjid Abuu Ubayda, Fuoni Meli Saba, Mkoa wa Mjini Magharibi, alikojumuika na waumini wa dini ya Kiislamu kwenye ibada ya sala ya Ijumaa.

Alisema, mataifa makubwa yaliyoendelea yamewekeza mtaji mkubwa kwenye elimu, ambao hutumia fedha nyingi kushajihisha elimu.

Al hajj Mwinyi alieleza kadri ya mataifa hayo yanavyotumia pesa nyingi kwenye elimu, ndivyo wanavyopiga hatua zaidi za maendeleo.

“Ukisikia kuna nchi inafanya maendeleo makubwa basi ujue ndani yake watu wamejikita mno katika masuala mazima ya elimu, suala la Utafiti maana elimu inaletwa na utafiti” 

Alisema, elimu ndio inayoleta mabadiliko makubwa kwenye jamii maendeleo yote yanatokana na elimu watu kujifunza elimu ya dini na dunia.

Kwaupande mwengine Al hajj Dk. Mwinyi alieleza elimu ya dini huwapandisha darja waumini wake kwa kuendelea kumcha Mwenyezi Mungu kikweli katika kutekeleza ibada ya haki kama inavyotakiwa.

Pia, Alhaj, Dk. Mwinyi amewasihi wazazi/ walezi kuendelea kuwahimiza watoto wao kusoma elimu zote mbili ya dini na dunia, ili kukuza taifa lenye vijana wenye maadili na busara ya kukimbilia maendeleo kwa ajili ya familia zao na taifa kwa ujumla.

Alieleza, miongoni mwa sababu zinazochangia mmong’onyoko wa maadili kwenye jamii ni ukosefu wa elimu zote mbili, hivyo aliiasa jamii kuweka mkazo zaidi kwenye elimu na kulinda maadili ya uislamu.

Hata hivyo, Al hajj Dk. Mwinyi aliitaka jamii kuendelea kutekeleza maamrisho ya Mwenyezi Mungu kwa kufuata mafundisho ya Mtume (SAW) kwa kufanya yaliyo mema na kuacha mabaya yanayomchukiza Allah (S.W).

Naye, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Sheikh Khalid Ali Mfaume, ameisisitiza jamii ya waislam kuendelea kukithirisha ibada hasa kwenye mwezi mtukufu wa Muharram.

Alisema, Mwezi wa Mfunguo nne (Muharami) ni miongoni mwa miezi mitukufu ya Mwenyezi Mungu baada ya Ramadhan. Pia alisisitiza mwezi 10 Muharam ni Sunna kufunga kwa waumini wa dini ya kiislam, funga ya  Ashura, aliyoieleza ni funga bora baada ya Ramadhani ambayo Mtume (SAW) aliifunga mara baada ya kuhamia Madina.

Naye, Khatibu wa sala hiyo ya Ijumaa, Sheikh Sultan Nassor, aliwahimiza waislam kuendelea kuwa wachamungu kwa kumcha Allah (S.W) kwa haki ili kujiepusha na yote aliyoyakataza.

Akizungumza kwenye msikiti huo wa Abuu Ubayda, Fuoni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mahad Istiqama, Sheikh Said Khalfan aliisihi jamiii kuendelea kushirikiana na Ofisi ya Muft katika kutatua changamoto zao.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.