Habari za Punde

WAZIRI NDUMBARO ATETA NA UONGOZI WA FIFA NA CAF


Na Shamimu Nyaki

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amekutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA ) katika Ukanda wa CECAFA, Andrea Silva na Katibu Mkuu  wa  Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), Veron Mosengo - Omba  ambao wamewasili nchini Tanzania kwa ajili ya mechi ya Ufunguzi wa michuano ya African Football League kati ya Timu ya Simba  ya Tanzania na Al Alhy ya nchini Misri,  utakaochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, Oktoba 20,2023 .

Katika kikao hicho viongozi hao pamoja na mambo mengine wamejadili maendeleo ya Michezo nchini ambapo kwa sasa Tanzania inafanya vizuri katika michezo hususani mchezo wa soka, kwa Timu za Taifa za  wanaume na Wanawake pamoja na Ligi mbalimbali na mashindano ya Kimataifa.


Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bw. Gerson Msigwa, Katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT) Bi. Neema Msitha, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)  Ndg. Wallace Karia na viongozi  wengine wa Serikali na TFF.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.