Habari za Punde

M/RAIS AZINDUA UUZAJI WA HATIFUNGANI KWAAJILI MRADI WA MAJI TANGA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akizindua Uuzaji wa Hatifungani kwaajili ya Fedha za Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Maji Tanga hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Regal Naivera Jijini Tanga 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akizindua Uuzaji wa Hatifungani kwaajili ya Fedha za Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Maji Tanga hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Regal Naivera Jijini Tanga

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akionesha kitabu cha muongozo wa Hatifungani ya Kijani ya Mamlaka ya Maji Tanga wakati wa uzinduzi wa Uuzaji wa Hatifungani kwaajili ya Fedha za Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Maji Tanga uliyofanyika katika Ukumbi wa Regal Naivera Jijini Tanga.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akishuhudia makabidhiano ya idhini ya uuzaji wa Hatifungani iliyotolewa na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) kwa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Tanga wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Uuzaji wa Hatifungani kwaajili ya Fedha za Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Maji Tanga.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Uuzaji wa Hatifungani kwaajili ya Fedha za Mradi wa Kuboresha Miundombinu ya Maji Tanga uliyofanyika katika Ukumbi wa Regal Naivera Jijini Tanga 



 Jamhuri ya Muungano wa Tanzania …

  

1.     Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha sisi sote kukutana hapa Tanga leo ili kuzindua uuzaji wa Hatifungani ya kijani kwa ajili ya kupata fedha za mradi wa kuboresha miundombinu ya maji katika Jiji la Tanga na Wilaya za Muheza, Pangani na Mkinga. Nawashukuru na kuwapongeza washiriki  wa hafla hii muhimu sana. Naipongeza Kamati ya Maandalizi na wote waliofanikisha  tukio hili.

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

2.     Mnamo tarehe 25 Oktoba 2021, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokutana na ujumbe wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UN Capital Development Fund-UNCDF), Ikulu ya Dar es Salaam, aliridhia na kuelekeza kutumika kwa Hatifungani katika ngazi ya Serikali za Mitaa na Taasisi nchini kama njia mbadala ya kibunifu ya kuongeza wigo wa upatikanaji wa fedha za miradi ya maendeleo. Kufuatia hatua hiyo, Kamati ya Kitaifa ya wadau kuhusu uuzaji wa hatifungani kwa Taasisi za Serikali (National Municipal  and Sub National Bond Stakeholders Taskforce) iliundwa. Wizara ya Fedha nayo iliunda na kuzindua Timu ya Kitaifa ya Uwezeshaji (National Facilitation Team (NFT)) mnamo tarehe 24 Februari 2022

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

3.     Uamuzi huu wa Serikali unatokana na ukweli kwamba Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22-2025/26)– 2025/26 una mahitaji makubwa ya rasilimali fedha ikilinganishwa na ukomo wa vyanzo vilivyozoeleka vya kupata fedha za maendeleo. Vilevile, uwekezaji katika kuendeleza miundombinu ya huduma ya Maji unahitaji rasilimali fedha nyingi ili kumaliza kero ya upatikanaji wa maji safi na salama.

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

 

4.     Natambua kwamba, Tanga UWASA  imekidhi vigezo na kupata idhini ya kuuza Hatifungani hii kutoka  kwenye mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana na Wizara ya Fedha.  Nawapongeza kwa dhati Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Wizara ya Maji, Wizara ya Fedha na Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Msajili wa Hazina na Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) kwa kufanikisha mpango huu. Vilevile, nalishukuru Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo na Mitaji (UNCDF) kwa kufadhili na kuratibu mchakato mzima wa jambo hili.

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

5.     Kama mlivyoeleza  kwenye taarifa yenu, Hatifungani hii itasaidia kuongeza kiasi cha maji yanayozalishwa kutoka lita milioni 42 hadi milioni 60, kuongeza upatikanaji wa maji katika jiji la Tanga kutoka asilimia 96 hadi takriban asilimia 100 ifikapo Juni 2025. Kuongeza mtandao wa maji katika miji ya Muheza na Pangani kutoka asilimia 70 hadi zaidi ya asilimia 95 ifikapo Juni 2025. Mradi huu utanufaisha zaidi ya wananchi 458,365 waliopo katika jiji la Tanga na miji ya Pangani na Muheza. Pia kupata maji ya kutosha kwa ajili ya wananchi wapatao 74,124 wa wilaya ya Mkinga.

 

6.     Nimefurahi kuona utekelezaji umeanza, maana kabla ya kufika ukumbini nilipata fursa ya kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Mradi huu kwenye eneo la Mtambo wa Kusafisha na Kutibu Maji wa Mowe, Kata ya Kiyomoni. Nawapongeza sana Tanga UWASA kwa kuweza kuanza utekelezaji wa sehemu ya mradi huu kwa  fedha za mkopo wa Shilingi bilioni 7.6 kutoka Benki ya TIB kupitia Mpango wa Investment Facility Financing - Output Based Aid (IFF-OBA) ambao ulibuniwa kwa kushirikiana na Shirika la KfW la Serikali ya Ujerumani.

 

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

7.     Njia hii ya matumizi ya Hatifungani ni nzuri  kwa kuwa inaruhusu ukopaji wa muda mrefu na uwezekano wa kupata fedha nyingi zaidi kwa wakati mmoja, hivyo kuzisaidia Taasisi zetu kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wakati na kuboresha huduma kwa wananchi. Napenda kutumia fursa hii tena kuwapongeza sana Bodi ya Wakurugenzi, Menejimenti na Wafanyakazi wote wa Tanga UWASA kwa kuwa na uthubutu na kutufungulia njia hii mbadala ya kupata fedha za kugharamia miradi ya maendeleo. Ni imani yangu kuwa hamtashawishika kuwekeza fedha za hatifungani hii yenye riba ndogo katika fursa nyingine (arbitrage profit). Mkifanya hivyo, kuna hatari ya kupoteza imani ya wadau kutumia njia hii kama malengo yake hayatafikiwa (reputational risk).

 

8.     Napenda kuhitimisha kwa kutoa maelekezo juu ya mambo ya kuzingatia, kama ifuatavyo:

 

Kwanza, Hatifungani tunayozindua leo iwe ni chachu na motisha kwa Halmashauri na taasisi nyingine zikiwemo Halmashauri kutumia njia hii ya kupata fedha za miradi ya maendeleo. Hivyo naielekeza Ofisi ya Msajili wa Hazina kama msimamizi wa Taasisi na Mashirika ya Umma nchini na Waziri wa OR-TAMISEMI kama msimamizi wa Halmashauri, kuona namna Taasisi, Mashirika na baadhi ya Halmashauri  zinavyoweza kutumia dirisha hili la Hatifungani kuharakisha utekelezaji wa miradi na kutoa nafasi kwa Serikali kujikita kwenye maeneo mengine ya kipaumbele ambako hakuna uwezeshaji wa aina hii.

 

Pili, naitaka Bodi ya Wakurugenzi, Menejimenti na Wafanyakazi wote wa Tanga UWASA, kusimamia vizuri matumizi ya fedha zitakazopatikana kupitia Hatifungani tunayoizidua leo na mapato mengine mtakayokusanya baada ya kukamilisha mradi huu. Nidhamu ya fedha na usimamizi thabiti ndiyo utakaowawezesha kurejesha kwa wakati fedha za wawekezaji wa Hatifungani hii. Serikali haitavumilia uzembe wa aina yoyote utakaoonekana kukwamisha jitihada hizi za Mheshimiwa Rais.

 

Tatu, natambua kwamba Mamlaka zetu za Maji kwa kiwango kikubwa zinafanya vizuri. Napenda kuwakumbusha Tanga UWASA kuongeza ufanisi katika uendeshaji wenu ili urejeshaji wa Hatifungani hii usiwe sababu ya kuzorota kwa huduma au ongezeko la bei za maji.

 

Nne, Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji na Wizara ya Maji, iweke utaratitu na mfumo wa tahadhari (early warning system) ili kufuatilia na kubaini mapema vihatarishi vinavyoweza kujitokeza.

 

Tano, kwa kuwa urejeshaji wa fedha hizo ni kwa mkupuo baada ya kuiva kwa Hatifungani, inaweza kuleta changamoto wakati wa malipo. Hivyo, ni vyema kujipanga mapema, ikiwezekana kufungua mfuko maalum wa kukusanya kidogokidogo fedha za marejesho (sinking fund). Lakini napenda nikiri kuwa nimefurahishwa na wazo la kibunifu la matumizi ya dira za malipo ya awali (pre-paid meters), naamini litasaidia kuongeza ufanisi wa ukusanyaji mapato na hivyo kuwajengea uwezo wa kulipa.

 

Wahe. Viongozi na Ndugu Washiriki;

 

9.    Ninapofikia tamati ya hotuba yangu napenda kutumia jukwaa hili kuwaalika na kuwahamasisha wawekezaji wote wa ndani na nje ya nchi, mifuko ya hifadhi za jamii, mifuko ya bima, taasisi mbalimbali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na wananchi kwa ujumla kushiriki katika ununuzi wa hatifungani hii ili kupata faida na wakati huo huo kuwekeza katika maendeleo ya jamii nzima.

 

10. Baada ya kusema hayo, sasa ninayo heshima kutangaza kuwa uuzaji wa hatifungani ya kijani kwa ajili ya kupata fedha za mradi wa kuboresha miundombinu ya maji Tanga, umezinduliwa rasmi.

 

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.