Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akihutubia wakati wa Ufunguzi wa Kongamano la
Kuhamasisha Uwekezaji katika Bustani za Kijani Nchini kwa Maendeleo Endelevu
linalofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa St. Gaspar mkoani Dodoma tarehe 15
Aprili 2024.
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…
Awali ya yote napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kushiriki Kongamano hili muhimu. Aidha, naishukuru Taasisi ya UONGOZI, Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwa kuandaa Kongamano hili. Nawashukuru pia waandaaji kwa kunialika tena kuwa mgeni rasmi kwenye mwendelezo wa makongamano ya Jukwaa la maendeleo endelevu, ambapo hili ni kongamano la nane mahsusi kwa ajili ya kuhamasisha uwekezaji katika Bustani za Kijani. Asanteni sana!
Kama mnavyofahamu, Bustani za Kijani (Green Parks) ni muhimu kwa ajili ya upatikanaji wa hewa safi, utunzaji wa vyanzo vya maji na utunzaji wa maliasili za nchi. Aidha, Bustani za Kijani zinasaidia kukabiliana na baadhi ya athari za mabadiliko ya tabianchi ikiwa ni pamoja na ongezeko la joto hasa maeneo ya mijini, kupunguza vifo vinavyotokana magonjwa yanayosababishwa na ongezeko la joto na kusaidia kupunguza ongezeko la hewa ya Kaboni. Vilevile, Bustani za Kijani zinawezesha kuwepo maeneo ya kupumzika, kufanya mazoezi na michezo mbalimbali na hivyo kusaidia kuboresha afya. Bustani za Kijani zikitunzwa vizuri zinaweza kuwa vivutio vya utalii na hivyo kuchangia pato la Taifa. Hata hivyo, pamoja na umuhimu mkubwa wa Bustani za Kijani, bado kuna mwamko mdogo wa uanzishaji, utunzaji na uendelezaji wa Bustani za Kijani. Maeneo mengi yaliyotengwa kwa ajili ya Bustani za Kijani hapa nchini hayatunzwi vizuri na baadhi yamebadilishwa matumizi, tofauti na ilivyokusudiwa awali.
Ndugu Washiriki;
Miaka iliyopita miji mingi hapa nchini ilifanya jitihada
kubwa za kutenga maeneo na kuanzisha Bustani za Kijani. Baadhi ya bustani hizo za kijani ni pamoja na
iliyo mkabala na ukumbi wa Karimjee (Dar es Salaam); iliyo mkabala na Ofisi ya
CCM Mkoa (Mwanza); Nyerere Square, Chinangali Park na Medeli zilizopo Dodoma pamoja
na ile ya mjini Iringa iliyo nyuma ya hospitali ya Rufaa. Pamoja na msisitizo
wa kuhakikisha miji na majiji yetu nchini yanatenga maeneo kwa ajili ya Bustani
za Kijani, kama nilivyosema hapo awali, uwekezaji na utunzaji wa maeneo hayo
bado siyo wa kuridhisha. Nchi yetu, hususan katika miji mikubwa, bado kuna
uhaba wa Bustani za Kijani. Nafahamu kwamba kumekuwepo na mipango na jitihada
za hapa na pale za kuanzisha na kuendeleza bustani hizi, lakini utekelezaji
wake umekuwa siyo endelevu.
Ni wazi kuwa jitihada kubwa zaidi zinahitajika ili
kuhakikisha kunakuwa na mwamko wa kutosha katika kuanzisha, kuendeleza na
kutunza maeneo ya Bustani za Kijani hapa nchini. Hivyo, napongeza uchaguzi wa
kaulimbiu ya kongamano la mwaka huu isemayo
“Kuhamasisha Uwekezaji katika Bustani za Kijani kwa Maendeleo
Endelevu Tanzania (Promoting Investments in Green Parks for Sustainable
Development in Tanzania).
Changamoto kubwa inayokabili uanzishaji na uendelezaji wa Bustani za Kijani nchini ni pamoja na usimamizi dhaifu wa maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya Bustani za Kijani, kubadili matumizi ya maeneo yaliyotengwa mahsusi kwa ajili Bustani za Kijani, mwamko hafifu wa viongozi na wananchi kulinda, kutunza na kuendeleza maeneo hayo na kutopewa kipaumbele katika bajeti za halmashauri za Miji na Majiji. Sekta binafsi nayo kwa kiasi kikubwa haijachangamkia fursa ya kuwekeza katika uendelezaji wa Bustani za Kijani. Hata hivyo, napenda kuwapongeza kwa dhati vijana na akina mama wajasiriamali wanaojihusisha na utunzaji wa vitalu vya miti na maua katika Miji na Majiji hapa nchini. Kwa hapa Dodoma, wajasiriamali hao ni pamoja na wale waliojiajiri katika bustani ya miti ya CDA (maili mbili), Kikundi cha Chapa Kazi kilicho pembeni ya kipita shoto (round about) cha barabara ya Iringa – Kikuyu magorofani, na Chinangali Park. Vilevile, napenda kuzipongeza taasisi za dini ambazo zimeendelea kutunza bustani ndogondogo za kijani katika maeneo yao, likiwemo eneo hili tulipo la St. Gasper na Martin Luther lililo upande wa pili wa barabara kuu ya kwenda Dar es Salaam.
Ndugu Washiriki;
Zipo nchi nyingi zilizopiga hatua kubwa katika uwekezaji
kwenye Bustani za Kijani na kunufaika sana na uwekezaji huo. Baadhi ya maeneo
ambayo uwekezaji mkubwa umefanywa ni kama vile Singapore, Bustani katika Mji wa
Sejong (Korea Kusini), Central Park (New York), Summer Palace
(Beijing), Boboli (Florence), Hampstead Heath (London), Al Azhar Park (Cairo) na
bustani zilizopo Abu Dhabi na Dubai (Umoja wa Falme za Kiarabu). Umaarufu wa bustani
hizi za kijani unatokana na uwekezaji, usimamizi na utunzaji mzuri wa maeneo
hayo. Hivi sasa, maeneo hayo yamekuwa
kivutio kikubwa cha utalii kwa wageni mbalimbali wanaotembelea nchi hizo.
Vilevile, katika baadhi ya nchi, maeneo ya Bustani za Kijani yamekuwa
yakitumika kutunza mitidawa (natural herbs) au viumbe vilivyo hatarini
kutoweka. Ni wajibu wetu kuiga mifano ya nchi zilizofanikiwa katika uwekezaji wa
Bustani za Kijani, ili kuwezesha uwekezaji kama huo hapa nchini kwa maendeleo
endelevu. Lakini, haitoshi kusifia tu bustani nzuri za kijani katika nchi
nyingine. Wakati sasa umefika tutengeneze Bustani za Kijani za hapa kwetu. Tena
ziwe za kiwango bora zaidi. Mimi na wenzangu tunaamini kwa dhati kabisa kwamba
vijana wa kitanzania wanao uwezo mkubwa na ubunifu wa kufanya miujiza katika
maeneo mengi, ikiwemo hili la Bustani za Kijani kama fursa ya ajira na chanzo
cha kipato kizuri na cha uhakika. Ninafahamu
tunao vijana wazuri sana katika tasnia ya kutumia na kuboresha sura ya nchi
iliyopo (landscaping). Aidha, tunao
vijana wenye vipaji vya hali ya juu vya kubuni na kutengeneza aina mbalimbali
za mapambo yanayoweza kutumika kwenye Bustani za Kijani na kuvutia watu wengi
wakiwemo watalii kuja kuona au kununua maua, mitungi/vyombo vya kufinyanga,
miti na wanyama wa kubumba n.k. yatayowekwa katika sehemu za kuingilia na ndani
ya bustani hizo za kijani.
Ndugu Washiriki;
Uanzishwaji na uendelezaji
wa Bustani za Kijani ni suala linalohitaji ushirikishwaji wa taasisi na wadau mbalimbali
wenye utaalam au uzoefu stahiki ili kuhakikisha uendelevu wa bustani hizi na
thamani ya fedha itakayowekezwa. Baadhi ya mambo yanayopaswa kuangaliwa kabla
ya kuwekeza ni utambuzi na uchambuzi wa mazingira ya bustani; usanifu wa ardhi
na bustani yenyewe; aina ya miti na maua yanayofaa katika eneo hilo; kubainisha
vifaa vitakavyotumika; sehemu za huduma mbalimbali kama vile kupumzika, michezo
na mazoezi; ukusanyaji wa rasilimali pamoja na mpango kazi wa utekelezaji. Katika
muktadha huu, natoa tena pongezi za dhati kwa Taasisi ya UONGOZI, kwa kuandaa
Kongamano hili ili kujadili namna ya kuvutia uwekezaji katika Bustani za Kijani,
kwa ushirikiano kati ya sekta binafsi na Serikali. Ni matumani yangu kuwa
kupitia Kongamano hili, masuala mbalimbali muhimu yahusuyo uwekezaji na uendelezaji
wa Bustani za Kijani nchini Tanzania yatajadiliwa na kuja na mkakati wa
utekelezaji ili tupige hatua katika suala hili.
Ndugu Washiriki;
Ningependa kuona mijadala
katika Kongamano hili ikiangazia mbinu mbalimbali za kuwekeza na kuendesha Bustani
za Kijani na jinsi tunavyoweza kujifunza kutokana na uzoefu na ubunifu wa
vijana wa kitanzania na ikibidi kuasili maarifa kutoka nchi nyingine; fursa na
changamoto za uanzishaji, uendelezaji na uendeshaji wa Bustani za Kijani, na
namna ya kukabiliana nazo; na
ushirikiano na wadau muhimu. Hivyo, matarajio yangu ni kuwa haya yote na mengine muhimu kuhusu
uwekezaji katika Bustani za Kijani yatajadiliwa kwa kina. Aidha, nitapenda kupata taarifa ya Kongamano hili na
mapendekezo ya hatua za kuchukua za muda mfupi na muda wa kati katika
kuendekeleza Bustani za Kijani kote nchini.
Ndugu Washiriki;
Hapo awali nilieleza kuhusu changamoto mbalimbali katika
uanzishaji, utunzaji na uendelezaji wa Bustani za Kijani hapa nchini. Hivyo,
kabla ya kuhitimisha hotuba yangu napenda kutoa msisitizo na maelekezo kama
ifuatavyo :
(i) Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Mamlaka za Miji, Halmashauri na Majiji wachukue hatua za makusudi kulinda maeneo yote yaliyotengwa kwa ajili ya Bustani za Kijani na kuhakikisha hayavamiwi au kubadilishwa matumizi. Maeneo hayo yapimwe na kuwekewa alama za kudumu kuonesha mipaka yake. Aidha, naagiza Mamlaka za Serikali za Mitaa zitunge sheria ndogo (by-laws) na kusimamia utekelezaji wake ili kuhakikisha maeneo ya Bustani za Kijani yanalindwa na kutumika kama ilivyokusudiwa;
(ii) Mamlaka
zote za Miji, Halmashauri za Wilaya na Majiji, washindanishe vijana wa
kitanzania kubuni bustani bora ya kijani katika Makao Makuu ya Wilaya, Mkoa,
Mji au Jiji iweje;
Mwisho, napenda
kueleza shauku niliyonayo ya kuona walau Bustani tatu mpya za Kijani
zinaanzishwa hapa Dodoma kabla ya mwisho wa mwaka 2025 na mojawapo iwe
Botanical Garden. Ninafahamu kuwa Mamlaka ya Jiji la Dodoma, imetenga maeneo
kwa ajili ya kuanzisha bustani hizo. Ninapenda kulishawishi Jiji la Dodoma
lichukue hatua ya kutangaza sasa fursa ya kuwekeza katika Bustani hizi
tangulizi (pioneer green parks). Hivyo, natoa wito kwa sekta binafsi
kujitokeza kuwekeza katika kuanzisha bustani hizo hapa Dodoma ili pamoja na
kutunza mazingira tulifanye Jiji letu kupendeza zaidi. Uzoefu kutoka nchi
mbalimbali zilizopiga hatua katika eneo hili, unathibitisha kuwa uwekezaji
katika kuanzisha na kutunza bustani
nzuri za kijani unalipa (profitable investment). Mkuu
Baada ya kusema hayo, ninayo heshima kutamka kuwa Kongamano la Kuhamasisha Uwekezaji katika Uendelezaji wa Bustani za Kijani nchini kwa Maendeleo Endelevu limefunguliwa rasmi. Nawatakia majadiliano mema.
ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA.
No comments:
Post a Comment