Habari za Punde

SERIKALI KUENDELEA KUDHIBITI ATHARI ZA MICHEZO YA KUBAHATISHA

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), akijibu swali bungeni jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Fedha, Dodoma)

Na Farida Ramadhani, WF – Dodoma.

Serikali kupitia Bodi ya Michezo ya Kubahatisha nchini inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuzuia na kudhibiti athari za michezo ya kubahatisha ili kuhakikisha jamii inakuwa salama.

Hayo yameelezwa Bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mlola, Mhe. Abdallah Shangazi aliyetaka kuwajua iwapo Serikali inatambua athari hasi kwa Jamii ya Watanzania zinazotokana na ongezeko kubwa la michezo ya kubahatisha.

Mhe. Chande alisema kuwa kwa mujibu wa Kifungu cha 7(2)(i) cha Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, Sura 41, mamlaka ya udhibiti ina jukumu la kuhakikisha kuwa jamii inalindwa ipasavyo dhidi ya athari hasi za michezo ya kubahatisha.

“Katika kutekeleza jukumu hilo, Bodi ya Michezo ya 

Kubahatisha imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali ya 

kuzuia na kudhibiti athari hasi zitokanazo na uwepo wa 

michezo ya kubahatisha, mikakati hiyo ni pamoja na 

kuimarisha udhibiti na uratibu wa sekta kwa kufanya ukaguzi 

wa mara kwa mara na matumizi ya mifumo ya 

TEHAMA,’’alisema Mhe. Chande.

Alifafanua kuwa Bodi inaendelea kutoa elimu kwa jamii 

kuhusu athari za michezo ya kubahatisha, kufanya mapitio ya 

mara kwa mara ya mifumo ya usimamizi wa michezo ya kubahatisha pamoja na kufanya kazi ya udhibiti kwa 

kushirikisha wadau na mamlaka nyingine kama vile Jeshi la 

Polisi, TCRA na TRA.

Mhe. Chande alisema pamoja na faida za kiuchumi na kijamii zinazotokana na michezo ya kubahatisha, Serikali inatambua athari zake katika jamii endapo haitaendeshwa kwa weledi ikiwemo uraibu na kugeuza michezo ya kubahatisha kuwa mbadala wa ajira, ushiriki wa watoto katika michezo ya kubahatisha na uwepo wa michezo haramu isiyo na usajili wa mamlaka ya udhibiti.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.