WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa leo Oktoba 04, 2025 amemwakilisha Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye uapisho wa Rais Mteule wa Malawi, Peter Mutharika uliofanyika katika uwanja wa Kamuzu, Blantyre nchini humo.
Mheshimiwa Rais Mutharika wa Chama cha Democratic Progressive (DPP) alimshinda mpinzani wake Rais Mstaafu Lazarus Chakwera wa The Malawi Congress Party (MCP) kwa asilimia 56.8.
Mutharika aliwahi kuwa Rais wa nchi hiyo kati ya mwaka 2014 hadi 2020 alipoangushwa na Mheshimiwa Chakwera, hivyo Mheshimiwa Rais Mutharika anarudi tena katika kiti hicho cha Urais baada ya miaka mitano.
Akizungumza baada ya kuapishwa Mheshimiwa Rais Mutharika amesema nchi ya Malawi ni kwa ajili ya Wamalawi wote, hivyo amewataka viongozi wajitokeze na washirikiane katika kuwatumikia watu na si matumbo yao, watoto wao au marafiki zao.
“Sote tunahitaji mabadiliko na ninawaahidi mabadiliko na kama nchi hii tunataka kuibadilisha ni lazima yatoke kwetu sisi Wamalawi. Ameongeza kuwa Serikali yake itahakikisha wananchi wanahudumiwa katika nyanja zote za kimaendeleo na kwa pamoja tutaijenga Malawi.”
(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAMOSI, OKTOBA 4, 2025
No comments:
Post a Comment