Mke
wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Mama Asha Suleiman Iddi
akizungumza na Vijana wanaobadilishwa tabia katika Nyumba ya Kubadilisha Tabia
iliyopo Mkorosoni Chake Chake Pemba.
Mke
wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi akikabidhi
magodoro kwa Vijana wa Soba House katika Nyumba yaoi liyopo Mkoroshoni chake
chake Kisiwani Pemba.
Mama Asha amefanya ziara ya
kuwatembelea Vijana hao akiambatana na Ujumbe wa Umoja wa Wake wa Wawakilishi
na Wabunge wa CCM ulio chini ya Uenyekiti wa
Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwena Shein.
Mama Asha Suleiman Iddi akiwakabidhi
Viongozi wa Soba House Chakula na Vifaa vya Michezo Vikiwemo Viti baada ya kuwatembelea Vijana hao kwenye
nyumba yao ya kubadilisha tabia iliyopo Mkoroshoni Chake chake Pemba.
Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi amewanasihi Vijana wanaoishi katika Nyumba za
kubadilisha tabia { Soba House } kuwa walimu kwa Vijana wenzao wakati wanaporejea katika
maisha yao ya kawaida ili kusaidia Jamii hasa Vijana kuepuka kujiingiza katika
vitendo viovu.
Mama
Asha alieleza hayo wakati akizungumza na Vijana hao waliopo katika nyumba ya
kubadilisha tabia iliyopo Mtaa wa Mkoroshoni Chake Chake Kisiwani Pemba.
Ziara
ya Mama Asha iliyojumuisha pia Wake wa Wawakilishi na Wabunge wa CCM unaounda
Umoja wa Wake wa Viongozi unaoongozwa na Mke wa Rais wa Zanzibar Mama
Mwanamwema Sheni ilienda sambamba na kukabidhi
zawadi za Magodoro, Vyakula,
Mafuta ya kupikia pamoja na Viti kwa Vijana hao hapo Soba House Mkoroshoni
Chake Chake Pemba.
Mama Asha alisema matatizo ya
Dawa za kulevya yanayopelekea maambukizi ya Virusi vya Ukimwi yanauma na kuleta
uchungu mkubwa ndani ya Jamii.
Alisema mapenzi kwa Familia hupungua au kutoweka kabisa inapotokea
Kijana wao amejiingiza katika janga la dawa za kulevya.
“ Mzazi anapata furaha na faraja pale anapotoa mafunzo na malezi kwa Mtoto wake na yakatekelezwa vizuri katika misingi ya
maadili”. Alisisitiza Mama Asha Suleiman Iddi.
Alifahamisha kwamba Serikali kupitia Taasisi zake pamoja na Jumuiya za
Kiraia bado zinathamini Vijana hao kwa vile wao ni sehemu ya Jamii.
Mama Asha aliwataka Vijana wote Nchini hasa wale wanaotumia dawa za
kulevya kuachana na anasa hiyo mbaya kwa kuwasusia wauzaji wa Biashara
hiyo.
“Mkifanya
mgomo baridi kwa kutotumia dawa za kulevya wauzaji wa bidhaa hiyo watashindwa
kuendeleza biashara hiyo. Na hiyo ndio kampeni pekee ya kupambana na mchezo huo
mchafu katika Nchi yetu”. Alifafanua Mama Asha.
Katika risala yao Vijana hao wa Nyumba ya kubadilisha Tabia Chake Chake
Pemba wameelezea faraja yao kutokana na Vituo vyao kumtabulika Kitaifa na
Kimataifa.
Walisema yapo mabadiliko makubwa kwa Vijana wanaopitia Nyumba za kubadilisha
Tabia.
Hata hivyo bado wamekuwa wakikabiliwa na Changamoto nyingi ikiwemo fedha
kwa ajili ya huduma pamoja na maeneo ya Michezo.
Wameiomba Serikali kuandaa Mipango madhubuti ya kuwajengea mazingira
bora ya mafunzo ya Amali kwa ajili ya kujiajiri wenyewe jambo ambalo
litawanyima muda wa kujiingiza tena katika janga la Matumizi ya Dawa za
kulevya.
Akipokea msaada wa vyakula na Vifaa hivyo msimamizi wa Nyumba za
kurekebisha Tabia Pemba Bwana Abdull Wahid alisema msaada huo ni chachu ya
kupunguza matatizo yanayozikabili nyumba
hizo.
Bwana Abdull Wahid alimshukuru Mama Asha
pamoja na Wanachama wa Umoja wao kwa msaada huo ambao utatumika kwa
lengo lililokusudiwa.
Msaada huo wenye
thamani ya Shilingi Milioni mbili {2,000,000/- } umejumuisha Mchele, Mafuta ya
Kupikia, Sabuni, Magodoro pamoja na Viti kwa ajili ya matumizi ya Ofisi.
HOW TO JOIN SOBA HOUSE
ReplyDelete