Habari za Punde

Mhe Waziri Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Akiwasilisha Bajeti ya Ofisi Yake

 

UTANGULIZI
1.      Mheshimiwa Spika,  kwa ruhusa yako naomba  kutoa hoja  kwamba Baraza lako tukufu sasa likae kama Kamati ya matumizi ili liweze kupokea, kuzingatia, kujadili, kuchangia na hatimae liweze kuidhinisha  Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa mwaka wa Fedha 2012/2013.

2.      Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana leo hii katika Baraza hili tukufu, kwa lengo la kujadili masuala muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu.


3.      Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya viongozi na wafanyakazi wote wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, napenda kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk. Ali Mohammed Shein kwa   kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya kazi ya kuwahudumia wananchi. Utaratibu aliouanzisha wa kukutana na taasisi za Serikali na kupokea taarifa za utekelezaji wa kila robo mwaka una madhumuni ya kukuza ufanisi katika utendaji wa shughuli za Serikali ili kuweza kuwatumikia wananchi vizuri zaidi.

4.      Mheshimiwa Spika, vile vile  sina budi kuwapongeza  viongozi  wetu wa kitaifa Makamu wa Kwanza wa Rais Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi kwa jitihada zao za kumsaidia Mheshimiwa Rais kuwatumikia wananchi wa Zanzibar. Mwaka mmoja wa utekelezaji wa bajeti umeonesha dhahiri umahiri na umakini walionao viongozi wetu hao.

5.      Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukurani za pekee kwa Mhe, Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye ndiye msimamizi mkuu wa Ofisi hii, kwa ushauri wake na miongozo anayonipatia katika utekelezaji wa majukumu yangu ya kila siku. Kwa hakika busara, hekima na uwezo wake wa kusimamia majukumu yake, yananipa muongozo juu ya namna bora ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu yangu. Naendelea kumuhakikishia kuwa nitajitahidi kadri Mwenyezi Mungu atakavyoniwezesha kusimamia vizuri majukumu yaliyo chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.

6.      Mheshimiwa Spika, napenda pia uniruhusu kukupongeza wewe binafsi na wasaidizi wako kwa kuliongoza Baraza hili tukufu kufuatana na sheria na kanuni za Baraza zikichangiwa na hekima na uadilifu mulionao. Umahiri wa utendaji kazi wenu unadhihirisha wazi pale inapotokea mijadala mizito na ikafikia maamuzi muwafaka.


7.      Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuipongeza Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa inayoongozwa na Mheshimiwa Hamza Hassan Juma Mwakilishi wa Wananchi wa Jimbo la Kwamtipura kwa kufanya nao kazi kwa mashirikiano makubwa. Kwa hakika Ofisi yetu inathamini sana michango, ushauri na maelekezo mbali mbali wanayotupa ambayo sio tu husaidia kutupatia mafanikio katika utekelezaji wa majukumu ya ofisi yetu lakini pia hutuwezesha kukabiliana na changamoto zinazotukabili.

8.      Mheshimiwa Spika, pia napenda kuwashukuru wajumbe wenzangu wa Baraza hili Tukufu la Wawakilishi, kwa kutoa ushirikiano wao wa dhati kwangu mimi binafsi pamoja na watendaji wa Ofisi yetu tukiwa ndani ya Baraza na hata katika majimbo yao.

9.      Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa mashirikiano makubwa wanayonipa katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi yetu. Vilevile, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Wakurugenzi pamoja na wafanyakazi wote wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa juhudi, bidii na ustahamilivu katika kutekeleza majukumu yao ya kazi na kuleta ufanisi na tija kwa Taifa.

10.  Mheshimiwa Spika, kwa  namna  ya  pekee napenda kuishukuru familia yangu kwa ustahamilivu wao na msaada mkubwa wanaonipa katika kunijengea utulivu ili niweze  kutekeleza majukumu yangu, nawaombea heri na baraka katika maisha yao.

11.  Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais napenda kutoa mkono wa  pole kwa ndugu na jamaa wa marehemu na kwa wale wote waliookolewa  au kupoteza mali zao katika ajali ya meli ya MV. Spice Islander iliyotokea tarehe 11/09/2011. Tutaendelea kuzikumbuka roho za ndugu zetu waliotangulia mbele ya haki. Mwenyezi Mungu azilaze roho za Marehemu mahala pema peponi Amin.

12.  Mheshimiwa Spika, vile vile kwa niaba ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais napenda kutoa mkono wa pole kwa familia pamoja na wananchi wa Jimbo la Uzini na Bububu kwa kuwapoteza wawakilishi wao wapendwa, marehemu Mussa Khamis Silima Mwakilishi wa Jimbo la Uzini na Salum Amour Mtondoo Mwakilishi wa Jimbo la Bububu, tutawakumbuka kwa michango yao mikubwa katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahala pema peponi Amin.

MALENGO MAKUU YA OFISI YA MAKAMU WA KWANZA WA RAIS

13.  Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ina jukumu la kusimamia na kuratibu masuala ya mazingira, watu wenye ulemavu, udhibiti wa dawa za kulevya na UKIMWI. Malengo makuu ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ni :
1.      Kuimarisha na kutetea uzingatiaji wa haki za binaadamu na fursa sawa kwa watu wenye ulemavu katika jamii.
2.      Kuongoza, kuratibu, kufuatilia na kutathmini muitiko wa kitaifa wa kupambana na UKIMWI.
3.      Kuimarisha usimamizi wa mazingira na matumizi endelevu ya maliasili.
4.      Kuratibu na kudhibiti usafirishaji na biashara haramu ya dawa za kulevya.
UTEKELEZAJI WA MALENGO YA OFISI YA MAKAMU WA KWANZA WA RAIS KWA MWAKA 2011/12 NA MALENGO 2012/13

14.  Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais imejipangia kutekeleza majukumu yake kupitia Idara na Tume zifuatazo.
1.      Ofisi ya Faragha
2.      Idara ya Mipango Sera na Utafiti
3.      Idara ya Uendeshaji na Utumishi
4.      Idara ya Mazingira
5.      Idara ya Watu Wenye Ulemavu
6.      Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya
7.      Tume ya UKIMWI
8.      Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Pemba

UTEKELEZAJI WA MALENGO KWA MWAKA 2011/2012

OFISI YA FARAGHA

15.  Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha ina majukumu ya kusimamia na kuratibu shughuli zote zinazofanywa na Makamu wa Kwanza wa Rais.

16.  Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilijipangia malengo yafuatayo:-

  1. Kusimamia na kuratibu shughuli zote za Makamu wa Kwanza wa Rais.
  2. Kukuza na kuimarisha mawasiliano ya habari za Makamu wa Kwanza wa   Rais.
  3. Kuimarisha huduma na mazingira mazuri ya utendaji kazi ofisini na nyumbani kwa Makamu wa Kwanza wa Rais.

17.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili 2011/2012 Ofisi ya Faragha imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

18.  Mheshimiwa Spika, katika kuratibu shughuli za Makamu wa Kwanza wa Rais, mambo mbalimbali yametekelezwa yakiwemo; kufanya ziara za kikazi ndani na nje ya nchi na kuandaliwa ripoti ambazo zimewasilishwa Serikalini. Aidha, vikao teule 19 vilivyojadili mada mbalimbali zikiwemo masuala ya kilimo, uvuvi, dawa za kulevya n.k. vimefanyika.

19.  Mheshimiwa Spika, Miongoni mwa ziara za ndani ni pamoja na kutembelea Wizara ya Kilimo na Maliasili, Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano pamoja na Idara na Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais. Pia ziara ya kufanya ukaguzi wa baadhi ya maeneo yaliyoharibiwa kimazingira kama vile, maeneo ya Uwanja wa Amani, njia kuu zinazopita umeme katika eneo la Kwarara, Uwandani, Kiwani, Wingwi n.k.

Aidha Mheshimiwa Makamu wa Kwanza wa Rais amefanya ziara katika Mikoa mitatu ya Tanzania Bara ikiwemo Tabora, Lindi na Dar es Salam ambapo alipata fursa ya kushiriki katika shughuli mbali mbali za kijamii, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbali mbali ya kimaendeleo.

20.  Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2011/2012 Mheshimiwa Makamu wa Kwanza wa Rais alifanya ziara moja ya kikazi nchini India. Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Makamu wa Kwanza alipata fursa ya kutembelea majimbo ya Hyderabad, Karnataka (Bangalore) na Kerala. Mheshimiwa Makamu wa Kwanza na ujumbe wake walipata fursa ya kukutana na Viongzi wa Serikali na taasisi mbali mbali pamoja na wawekezaji katika majimbo hayo matatu.
21.  Mheshimiwa Spika, Zanzibar inatarajiwa kufaidika na ziara hii katika Nyanja mbali mbali zikiwemo, teknolojia ya habari na mawasiliano, elimu, kilimo, biashara na uwekezaji. Ufuatiliaji wa mafanikio ya ziara hii kwa pande zote mbili unaendelea vizuri.
22.  Mheshimiwa Spika, zaidi ya wananchi 250 walifika ofisini kwa Makamu wa Kwanza wa Rais kwa ajili ya kuwasilisha malalamiko yao pamoja na kupatiwa ushauri na maelekezo katika kuyapatia ufumbuzi mambo yanayowakabili. Aidha mabalozi 12 wanaoziwakilisha nchi zao pamoja na wawakilishi wa  mashirika tisa ya kimataifa na ya kikanda walifika kwa Makamu kwa ajili ya kujitambulisha na kuzungumzia mambo mbali mbali ya kimaendeleo pamoja na kuimarisha mashirikiano.

23.  Mheshimiwa Spika, kuanzishwa kwa kitengo cha habari katika Ofisi ya Faragha, kumepelekea kurahisisha upatikanaji wa taarifa na matukio mbalimbali ambayo Makamu wa Kwanza wa Rais anayafanya. Kitengo kimeweza kuanzisha mtandao wake wa kijamii “weblog” ambao unaojulikana kwa jina la “Zanzibar ni njema” yenye anuani http://mkr1znz.wordpress.com. Mtandao huo wa kijamii hurusha hewani habari na taarifa mbalimbali za Mheshimiwa Makamu wa Kwanza wa Rais.

24.  Mheshimiwa Spika, Kitengo cha habari katika Ofisi ya Faragha pia kina mashirikiano na mawasiliano mazuri na vyombo vyengine mbali mbali vikiwemo vile vinavyotumia mtandao ambavyo pia huchapisha habari na matukio ya Mheshimiwa Makamu wa Kwanza wa Rais.

25.  Mheshimiwa Spika, Jumla ya vipindi vitano vimetayarishwa na kurushwa hewani kupitia TV na radio za Serikali na zile za binafsi. Zaidi ya makala 15, zimeandikwa na kuchapishwa katika magazeti mbali mbali na mitandao ya kijamii. Mikutano miwili na waandishi wa habari “Press conference” imefanyika. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 1).

26.  Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha mazingira mazuri ya utendaji kazi ofisini na upatikanaji wa huduma nyumbani kwa Makamu wa Kwanza wa Rais, samani na vitendea kazi mbalimbali vimenunuliwa.

27.  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 hadi kufikia Mei 2012 Ofisi ya Faragha imekwishatumia jumla ya Shilingi 99,100,000 kwa kuendeshea kazi.


MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
28.  Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-

1.       Kusimamia na kuratibu shughuli zote za Makamu wa Kwanza wa Rais.
2.       Kukuza na kuimarisha mawasiliano ya habari za Makamu wa Kwanza wa Rais.
3.       Kuimarisha mazingira ya kazi katika kuleta ufanisi.
4.       Kuimarisha huduma za Makamu wa Kwanza wa Rais.

29.  Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia, Ofisi ya Faragha  kwa mwaka fedha 2012/2013 inahitaji jumla ya Shilingi 511,324,000  kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo T.Shs. 300,000,000 kwa kuendeshea kazi na T.Shs. 211,324,000 ni kwa ajili ya mishahara.

IDARA YA MIPANGO SERA NA UTAFITI
30.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti ina majukumu ya kuandaa na kusimamia utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, kukusanya, kutunza takwimu, ufuatiliaji na tathmini pamoja na kuratibu shughuli za  utafiti kwa Idara zote zilizo  chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.

31.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilijipangia malengo yafuatayo:-
1.    Kusimamia na kuratibu shughuli zote za mipango, sera na utafiti katika Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
2.    Kuweka utaratibu utakaowezesha upatikanaji wa taarifa sahihi za shughuli za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ndani na nje ya nchi kwa wepesi.
3.    Kuratibu na kusimamia miradi ya maendeleo ya taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo.
4.    Kutafuta rasilimali ambazo zitasaidia katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
32.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

33.  Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kazi zake za kawaida za kuratibu, Idara hii imeandaa mipango ya utekelezaji, bajeti, pamoja na kuiwakilisha Ofisi  katika  kamati za kitaalamu na vikao mbali mbali ili kuhakikisha masuala yaliyo chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais yanazingatiwa katika mipango yote ya maendeleo.

34.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango imekamilisha uandaaji wa tovuti ya  Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa lengo la kutoa taarifa kiurahisi ndani na nje ya nchi, tovuti hii inatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika kurahisisha mawasiliano baina ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais na wadau wake (www.fvpo.go.tz).

35.  Mheshimiwa Spika, Idara imeendelea kuratibu na kusimamia utekelezaji wa miradi mitatu ya maendeleo ikiwemo mradi wa kuangamiza kunguru weusi, mradi wa usimamizi wa maji machafu Msingini - Kichungwani Pemba pamoja na mradi wa kuimarisha majengo ya viongozi.

36.  Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kuangamiza Kunguru Weusi umeanza rasmi mwezi wa Machi 2012.  Lengo Kuu la Mradi huu ni kuua kunguru weusi waliopo hapa Zanzibar kwa kutumia mitego na sumu.  Aidha lengo la mradi la mwaka 2011/2012 ni kuua kunguru 408,000. Mradi huu unatekelezwa kwa pamoja kati ya Idara ya Mazingira na Idara ya Misitu na Maliasili Zisizorejesheka.  Fedha za utekelezaji wa mradi huu zinatoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Finland kupitia Jumuiya isiyokuwa ya Kiserikali ya Uhifadhi wa Wanyama pori ya Tanzania (Wildlife Conservation Society – WCS).

37.  Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mchango wa Serikali, jumla ya Shillingi 50,000,000 zilipangwa kutumika na hadi kufikia mwezi wa Mei 2012 Shillingi 35,000,000 sawa na asilimia 70 zimetolewa.  Mambo yaliyofanyika kwa fedha hizo ni pamoja na kutengeneza mitego 30 na kusambazwa maeneo mbalimbali (tafadhali angalia kiambatanisho nam. 2), kununua sumu ya kuulia kunguru kilo mbili kutoka New Zealand, kununua vifaa mbalimbali vikiwemo mabesini, ndoo, sinia, vijiko, glavu, mapanga na majembe pamoja na kununua chambo cha kutumika kwenye sumu na mitego.

38.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi wa Mei 2012 jumla ya kunguru 11,596 wameshauliwa. Idadi hiyo ni ndogo kwa mujibu wa kiwango cha mwaka kilichowekwa, hii imetokana na kuchelewa kupatikana kwa fedha na muda mkubwa ulitumika kutengeneza mitego pamoja na kuagizishia sumu kutoka nje ya nchi.

39.  Mheshimiwa Spika, mradi wa ujenzi wa mtaro wa maji machafu Msingini na Kichungwani ulizinduliwa rasmi Julai 2009. Mradi unatekelezwa kwa pamoja kati ya Serikali kupitia Idara ya Mazingira na wananchi wa Shehia za Msingini na Kichungwani zilizopo katika Wilaya ya Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba kupitia mradi wa TASAF. Lengo kuu la mradi huu ni kulinda na kusimamia mazingira ya baharini na ukanda wa pwani wa magharibi ya bahari ya hindi kutokana na shughuli mbali mbali zinazofanywa kutoka nchi kavu ambazo zinasababisha uchafuzi wa mazingira. Jumla ya shilingi 440,000,000 zilitolewa na UNEP pamoja na Aqua- 4 All kwa ajili ya vifaa na kazi za mradi huu. Aidha jamii kupitia TASAF ilichangia jumla ya shillingi 69,000,000.

40.  Mheshimiwa Spika, Shughuli kubwa za mradi huu ambazo zimefanyika ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa mtaro wa maji ya mvua wenye urefu wa mita 1,610, ulazaji wa mabomba ya kupitishia maji machafu na ujenzi wa mabwawa matatu ya kukusanyia na kusafishia maji machafu. Kazi kubwa zilizobakia kukamilisha mradi huu ni uwekaji wa kokoto kwenye mabwawa hayo na matengenezo ya mtaro wa zamani wa maji ya mvua. Mkandarasi wa kutoa huduma za usambazaji wa kokoto, mchanga na saruji kwa ajili ya kumalizia kazi hizo ameshapatikana na anatarajiwa kuanza kazi hivi karibuni.

41.  Mheshimiwa Spika, mradi huu ulitarajiwa kukamilika tarehe 31 Machi 2011, lakini kutokana na ucheleweshwaji wa upatikanaji wa fedha kutoka UNEP, pamoja na ugumu uliojitokeza wakati wa mvua wa kufikisha vifaa vya kazi katika eneo lililochimbwa mabwawa umesababisha mradi huu kutomalizika kwa wakati uliopangwa. 

42.  Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa mradi wa kuimarisha nyumba za viongozi wa kitaifa, ununuzi wa vifaa na marekebisho ya makaazi mapya ya Makamu wa Kwanza wa Rais yamefanyika.

43.  Mheshimiwa Spika,   Idara ya Mipango iliendelea na juhudi zake za kutafuta rasilimali za  kusaidia katika utekelezaji  wa majukumu ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, kwa kuandika pendekezo la mradi wa kujenga uwezo kwa Ofisi na kuiwasilisha UNDP hali ambayo imepelekea kufanikiwa kuingizwa katika mradi wa miaka minne wa UNDAP. Aidha pendekezo jengine la mradi wa kujenga uwezo limeandikwa na kuwasilishwa Benki ya Dunia.

44.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango,Sera na Utafiti  kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikadiriwa kutumia Shilingi 170,010,000 kati ya hizo Shilingi 15,000,000 kwa kuendeshea kazi na Shilingi 155,000,000 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Hadi kufikia Mei 2012 Idara ilikwisha ingiziwa shilingi 15,000,000 sawa na asilimia100 kwa kazi za kawaida na Shilingi 140,000,000 sawa na asilimia 90 kwa kazi za maendeleo.

 MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
45.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-
  1. Kusimamia, kuratibu na kuandaa, shughuli zote za mipango, sera, utafiti pamoja na ufuatiliaji na tathmini kwa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
  2. Kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli mtambuka (UKIMWI, dawa za kulevya,  jinsia, mazingira, watu wenye ulemavu, utawala bora na idadi ya watu)
  3. Kuimarisha mazingira ya kazi na kujenga uwezo wa watendaji
46.  Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Miradi ya Maendeleo Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais inatarajia kutekeleza miradi mitano (5) kwa kupitia fedha za Serikali na mradi mmoja kwa fedha za wahisani. Miradi yenyewe ni:-
a)    Mradi wa kuendeleza elimu ya mazingira
b)   Mradi wa majaribio wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi
c)    Mradi wa kuangamiza kunguru weusi
d)   Mradi wa kuingiza masuala ya watu wenye ulemavu katika mipango ya maendeleo
e)    Mradi wa kujenga kituo cha Tiba na   Marekebisho ya Tabia kwa watumiaji wa dawa za kulevya huko Tunguu (Construction of Treatment and Rehabilitation Center)
f)    Na mradi wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi ambao utatumia fedha za wahisani.

47.  Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia Idara ya Mipango, Sera na Utafiti kwa mwaka wa fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 176,251,000 kwa kazi za kawaida. ambapo T.Shs. 115,000,000 kwa ajili ya kuendeshea kazi na T.Shs.  61,251,000 kwa ajili ya mishahara. Idara pia inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 255,000,000 kwa kazi za maendeleo ikiwa ni mchango wa serikali. Aidha Idara inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 705,600,000 kutoka kwa wahisani. Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais inaendelea kuwasiliana na Washirika wa Maendeleo kuhusu ongezeko la Fedha hizi za Mchango wa Wahisani katika Miradi ya Kimaendeleo.


IDARA YA UENDESHAJI NA UTUMISHI 
48.  Mheshimiwa Spika, Idara hii ina majukumu ya kusimamia rasilimali watu pamoja na undeshaji wa kazi za kila siku za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais. Katika kutekeleza majukumu hayo inasimamia utawala, ajira, maslahi na maendeleo ya watumishi pamoja na sheria, kanuni na taratibu za utumishi. Pia inasimamia masuala ya nidhamu, uwajibikaji, mafunzo na mafao ya wafanyakazi wanaostaafu.

49.  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 Idara ilijipangia malengo yafuatayo:
1.      Kuimarisha mazingira mazuri ya utendaji kazi.
2.      Kukuza uwezo wa wafanyakazi na viongozi na kuwapatia maslahi
3.      Kukuza na kuimarisha mawasiliano ya habari.
4.      Kuimarisha Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
5.      Kuimarisha huduma za usafiri katika Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
6.      Kuratibu safari za kikazi nje na ndani ya nchi.

50.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei, 2012 Idara ya Uendeshaji na Utumishi imeweza kutekeleza majukumu yafuatayo:

51.  Mheshimiwa Spika, Idara imeendelea na jitihada zake katika kuhakikisha kuwepo kwa mazingira mazuri ya kazi kwa kuwapatia wafanyakazi vifaa mbali mbali vikiwemo samani za Ofisi na vitendea kazi.  Hatua hiyo imetoa mwelekeo mzuri wa ufanisi hasa katika utekelezaji wa majukumu ya kazi.

52.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi   imeweza kuwapatia maposho wafanyakazi wanaostahiki na kufanya malipo ya fedha za likizo kwa wafanyakazi 18 waliokwenda likizo.

53.  Mheshimiwa Spika, Idara imeendelea kuwapatia mafunzo wafanyakazi ili kuleta ufanisi katika utendaji. Mfanyakazi mmoja anaendelea na mafunzo ya muda mrefu, watatu wamepatiwa mafunzo ya muda mfupi na wafanyakazi wawili wameweza kusaidiwa baadhi ya gharama za mafunzo kama vile usafiri na vifaa vya kuandikia. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 3)

54.  Mheshimiwa Spika, Idara kupitia Kitengo cha Habari na Mawasiliano kwa kushirikiana na taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais imeendelea kushajihisha wananchi na kutoa elimu ya mazingira, dawa za kulevya, UKIMWI na masuala ya watu wenye ulemavu kupitia Televisheni, Radio na Magazeti. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 4)

55.  Mheshimiwa Spika, Idara imefanya matengenezo makubwa ya jengo la Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ili liweze kuwa na hadhi inayolingana na Ofisi hii. Miongoni mwa matengenezo hayo ni pamoja na kubadilisha mfumo wa maji machafu na safi, kubadilisha sehemu za mikingo ya vigae vya paa, kupaka rangi na kujenga sehemu ya kupokelea wageni.

56.  Mheshimiwa Spika, Idara imeweza   kuhudumia safari sita  za nje na kumi na saba za ndani kwa viongozi na watendaji katika kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, safari hizo zimewawezesha kuhudhuria shughuli mbali mbali za kazi na mikutano ambayo imepelekea kuimarisha utendaji kazi, mahusiano na kubadilishana uzoefu.

57.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi kwa mwaka wa Fedha 2011/2012 imekadiria kutumia jumla ya shilingi 704,204,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo T.Shs. 388,770,000 kwa ajili ya kuendeshea kazi na T.Shs. 315,434,000 kwa ajili ya mishahara. Hadi kufikia Mei, 2012 ilikwisha kuingiziwa kiasi cha Shilingi 745,545,197 sawa na Asilimia 106. kati ya hizo shilingi 299,725,000 sawa na asilimia 77 kwa ajili ya kuendeshea kazi Shilingi 445,820,197 sawa na asilimia 141 kwa ajili ya mishahara. (Ongezeko hili limetokana na kuongezeka kwa mishahara)
MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
58.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi  imepanga  kutekeleza malengo yafuatayo:-
  1. Kusimamia majukumu na utendaji wa wafanyakazi.
  2. Kuimarisha mazingira ya utendaji kazi.
  3. Kuwajengea uwezo wafanyakazi na kuwapatia maslahi.
  4. Kukuza na kuimarisha mawasiliano ya habari
  5. Kusimamia utaratibu wa udhibiti wa matumizi ya fedha.
59.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi ili iweze kutekeleza malengo iliyojipangia kwa mwaka wa fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 616,444,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo T.Shs.254,749,00  kwa kuendeshea kazi  na T.Shs. 361,695,000 kwa ajili ya mishahara.

IDARA YA MAZINGIRA
60.  Mheshimiwa Spika, majukumu makuu ya Idara ya Mazingira kwa mujibu wa Sera ya Mazingira ni kukusanya na kuhifadhi taarifa za kimazingira, kutoa taarifa za kimazingira ili ziweze kusaidia katika kutayarisha na kutekeleza mipango na miradi ya kimaendeleo, kufuatilia mwenendo wa hali ya kimazingira, kukabiliana na matatizo ya kimazingira, kuhamasisha wadau kuchukua hatua za kuhifadhi mazingira pamoja na kutoa elimu ya mazingira kwa jamii.

61.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikuwa na malengo yafuatayo:-
1.      Kuongeza  uelewa wa elimu ya mazingira kwa jamii na wadau wengine.
2.      Kuhakikisha kwamba miradi ya maendeleo inazingatia vigezo vya utunzaji wa mazingira.
3.      Kudhibiti uingizaji wa bidhaa chakavu zinazoharibu na kuchafua mazingira.
4.      Kuendelea kuzuia uingizwaji na matumizi ya mifuko ya plasitiki.
5.      Kuandaa Mpango Mkakati wa utekelezaji wa Sera mpya ya Mazingira.
6.      Kutekeleza mradi wa kuangamiza kunguru weusi hapa Zanzibar.
7.      Kuandaa mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (climate change strategy).
8.      Kuweka utaratibu mzuri wa uvunaji wa maliasili zisizorejesheka.

62.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Idara ya Mazingira  imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

63.  Mheshimiwa Spika, Idara imeweza kutoa matangazo juu ya marufuku ya mifuko ya plastiki kwa siku za sikukuu kupitia Redio za ZBC, Hit FM na Zenji FM, pamoja na Televisheni za ZBC na Zanzibar Cable.  Vipindi 9 vya redio na vipindi 3 vya TV vinavyohusu usimamizi wa mazingira vimerushwa hewani (Tafadhali rejea kiambatanisho Nam. 4). Filamu fundishi (documentaries) tatu kuhusu athari za mifuko ya plastiki, uchimbaji holela wa mchanga, na bidhaa chakavu za umeme na elektroniki ziliandaliwa.  Semina kumi juu ya athari na udhibiti wa mifuko ya plastiki na uchafuzi wa mazingira zimefanywa skuli zote za msingi za Unguja na Pemba ambazo zina vilabu vya mazingira. Jumla ya skuli 146 (90 Unguja 56 Pemba) na wanafunzi 292 (180 Unguja 112 Pemba) walishiriki semina hizo. Mkakati wa mawasiliano kwa ajili ya elimu ya mazingira umetayarishwa.  Aidha, Idara ilifanya mikutano mitano ya jamii huko Pemba katika maeneo ya Uwandani, Kangagani na Muwambe na kuwahusisha wanajamii 157 (wanawake 30, wanaume 127).  Mikutano hiyo imepelekea kuundwa kwa kamati za jamii za usimamizi wenye uwiano wa ukanda wa pwani (Integrated Coastal Zone Management Committees – ICZM).

64.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira imefanya semina ya siku tatu kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako tukufu na wewe mwenyewe Mheshimiwa Spika ulitupa heshima ya kuiongoza semina hiyo. Semina hiyo iliyohusu masuala mbalimbali ya mabadiliko ya tabianchi ilikuwa na lengo la kuwapa uelewa wa mabadiliko ya tabianchi na mwelekeo wa Zanzibar katika kusimamia suala hilo.  Sambamba na hayo wafanyakazi 12 waliwezeshwa kufanya ziara ya kimasomo mjini Moshi na Arusha kujifunza na kupata uzoefu juu ya usimamizi wa taka, wafanyakazi hao ni kutoka Idara ya Mazingira, Manispaa, Halmashauri ya Wilaya ya Magharibi, Mabaraza ya Miji ya Chake Chake, Wete na Mkoani, Jumuiya ya Wakulima, Wafanyabiashara na Wenye Viwanda pamoja na jumuiya zisizokuwa za kiserikali ambazo zimewakilishwa na jumuiya ya CODECOZ.Aidha viongozi 10 wa Kamati ya machimbo ya Uwandani walishiriki ziara ya kimasomo Mjini Mombasa nchini Kenya kwa lengo la kujifunza namna bora ya shughuli za uchimbaji na urejeshwaji wa maeneo yaliyochimbwa.
65.  Mheshimiwa Spika, katika kujenga uwezo wa kiutendaji  Idara ya Mazingira ili kuweza kutekeleza majukumu ya kutoa elimu ya mazingira na kufanya tathmini ya athari za kimazingira, jumla ya wafanyakazi sita wamepatiwa mafunzo ya muda mfupi kuhusu uandishi wa habari na tathmini ya athari za kimazingira.  Aidha, wafanyakazi wawili wamepatiwa mafunzo ya muda mrefu katika fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
( ICT) na Uandishi wa habari. Wafanyakazi watatu wamelipiwa gharama za masomo kwa ngazi ya cheti katika fani za  kilimo, usimamizi wa kumbukumbu na Usimamizi rasilimali watu.  .

66.  Mheshimiwa Spika, Idara imefanyia mapitio ripoti 12 za Tathmini za Athari za Kimazingira na Kijamii na kutoa vyeti vya mazingira kwa taasisi husika kwa hatua za utekelezaji. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 5).  Jumla ya miradi ya hoteli 110 (80 Unguja na 30 Pemba) imefanyiwa ufuatiliaji katika maeneo mbali mbali ya Zanzibar ili kuona namna inavyozingatia masuala ya kimazingira katika uendeshaji wa shughuli zao (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 6). Katika ufuatiliaji huo, miradi iliyoonekana na kasoro za kimazingira ilitakiwa kuondoa kasoro hizo ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa kimazingira. (Environmental audit).

67.  Mheshimiwa Spika, miradi ambayo imejenga ndani ya mita 30 kuanzia alama inayofikiwa na maji ya bahari yanapojaa (high water mark) imetakiwa kubomoa sehemu ambayo imejengwa ndani ya eneo hilo.  Hadi sasa ni mradi mmoja tu wa Zanzibar Ocean View ndio umeripoti kutekeleza amri hiyo.  Kwa miradi ambayo imekaidi amri hiyo majina ya miradi hiyo yamewasilishwa Idara ya Mipango Miji na Vijiji kwa hatua za kisheria kwa mujibu wa Kanuni ya kudhibiti matumizi ya ardhi kwa ajili ya uekezaji ya mwaka 2006 (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 7). Sambamba na utekelezaji huo, Kanuni ya kufanya tathmini ya athari za kimazingira (Environemntal Impact and Social Assessment – EISA Regulations) imefanyiwa mapitio.

68.  Mheshimiwa Spika, rasimu ya kanuni ya kupiga marufuku uingizwaji wa bidhaa chakavu za umeme na elektroniki (e-waste) nchini imeandaliwa kwa kuwashirikisha wadau husika.  Hata hivyo, baada ya kanuni hiyo kupitiwa na Kamati ya Uongozi ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais na wadau wengine  imeonekana ipo haja ya kuandaa viwango vya bidhaa zitakazoruhusiwa kuingizwa nchini badala ya kupiga marufuku ya moja kwa moja kuingiza bidhaa hizo. Idara inaendelea kushauriana na Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko ili kuweka viwango vinavyohitajika vya bidhaa hizo chakavu.

69.  Mheshimiwa Spika,  kanuni ya kusimamia marufuku ya mifuko ya plastiki imefanyiwa marekebisho yaliyohitajika.  Kufuatia marekebisho hayo, matangazo kwa njia ya gari yametolewa kwa mikoa mitano ya Zanzibar.  Aidha, operesheni za kila siku zimefanyika ambazo zinasimamiwa na mkuu wa operesheni wa Jeshi la Polisi Zanzibar. Kwenye operesheni hizo hadi kufikia mwezi wa Mei 2012  jumla ya watu 192 (5 wanawake na 187 wanaume) wamekamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria na kutozwa faini jumla ya shilingi 7,650,000 (shilingi 6,350,000.Unguja na 1,300,000 Pemba). Fedha zote hizo zimeingizwa kwenye mfuko mkuu wa Serikali kupitia Mahakama husika. Aidha mafanikio makubwa yaliyopatikana kwenye operesheni hizo ni kupungua kwa kiwango kikubwa cha matumizi ya mifuko ya plastiki pamoja na kupungua kuzagaa kwa mifuko hiyo kwenye maeneo mbali mbali ya Zanzibar.

70.  Mheshimiwa Spika, rasimu ya Mpango Mkakati wa utekelezaji wa Sera mpya ya Mazingira imeandaliwa.  Hata hivyo, kukamilika kwa uandaaji wa Mpango Mkakati huo unategemea kukamilika kwa Sera mpya ya Mazingira ambayo itajadiliwa katika kikao cha Makatibu wakuu hivi karibuni. Sera hiyo imechelewa kukamilika kutokana na umuhimu wa kuingiza mambo mengine mapya ya kimazingira yakiwemo ya mabadiliko ya tabianchi ambayo utafiti wake ulikuwa haujakamilika. 

71.  Mheshimiwa Spika, katika hatua za kuandaa mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, utafiti juu ya athari za kiuchumi zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi umefanyika na ripoti yake imewasilishwa Serikalini baada ya kujadiliwa na wadau.  Kufuatia kupatikana kwa taarifa hizo, tayari hatua za kumpata mshauri mwelekezi wa kuandaa Mkakati huo zimeshaanza.  Katika hatua nyengine, maeneo 148 yanayoingia maji ya chumvi Unguja na Pemba yameorodheshwa, kati ya hayo 25 yapo Unguja   na 123 yapo Pemba  (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 8). Aidha kamati za uongozi na kitaalamu za kusimamia masuala ya mabadiliko ya tabianchi kwa Zanzibar zimeanzishwa. Kamati ya uongozi ina wajumbe 10 ambao ni Makatibu wakuu na kamati ya kitaalamu ina wajumbe 23 katika ngazi ya Wakurugenzi na Viongozi wa taasisi zisizo za kiserikali. 

72.  Mheshimiwa Spika, rasimu ya kanuni juu ya uchukuaji wa maliasili zisizorejesheka imeandaliwa na kujadiliwa na wadau mbalimbali. Hivi sasa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais  inaendelea kuyafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kabla ya kuchapishwa na kuanza utekelezaji.  Sambamba na kanuni hiyo, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais pia inaendelea na taratibu za kuandaa kanuni ya usimamizi wenye uwiano wa ukanda wa pwani (Integrated Coastal Zone Management {ICZM} Regulations).

73.  Mheshimiwa Spika, kutokana na kuwepo athari za mabadiliko ya tabianchi, Idara ya Mazingira ilibahatika kupata fedha za wahisani za kutekeleza mradi wa majaribio wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.  Kupitia mradi huu, Idara ya Mazingira ilipata jumla ya Shilingi 539,414,800 ili kutekeleza kazi mbalimbali za mradi huo wenye lengo la kufanikisha upatikanaji wa maji yasiyokuwa na chumvi kwa Wananchi wa Shehia ya Nungwi, Wilaya ya Kaskazini A, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

74.  Mheshimiwa Spika, kazi ambazo kwa sasa zimetekelezwa ni pamoja na kuchimba kisima katika eneo la Shehia Kilimani chenye uwezo wa kuzalisha maji lita 30,000 kwa saa, kuchimba msingi wa Kilomita 7.5 kutoka eneo la kisima hadi Nungwi, kununua mabomba na kuyalaza katika msingi uliochimbwa, kujenga kibanda cha pampu ya maji, kununua na kufunga pampu ya maji.  Aidha, kazi zinazoendelea ni kufunga tangi jipya lililonunuliwa kutoka Uingereza lenye uwezo wa kuhifadhi lita 150,000,  kununua na kufunga transfoma pamoja na kuunga umeme kwenye kibanda cha pampu ya maji.  Hivi sasa mradi huu uko katika hatua za mwisho za kukamilika.

75.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikadiriwa kutumia Shilingi 239,158,000 kwa kazi za kawaida, hadi kufikia Mei  2012 ilikwisha ingiziwa shilingi 261,426,046 sawa na asilimia 109.3 kati ya hizo shilingi 66,680,000 sawa na asilimia 66 kwa ajili ya kuendeshea kazi na Shilingi 194,746,046 sawa na asilimia 144 kwa ajili ya mishahara. Aidha katika kufanikisha kazi zilizotekelezwa jumla ya shilingi 118,105,066 zilitumika kutoka mradi wa MACEMP na SMOLE.

76.  Mheshimiwa spika, Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2011/2012, ilipangiwa kukusanya jumla ya shillingi 9,000,000. Aidha makusanyo hayo yamegawika katika  sehemu mbili ikiwa ni pamoja na ada ya hifadhi ya mazingira ambayo ilipangiwa jumla ya shilingi 4,000,000 na ada ya ukaguzi wa mazingira yenye jumla ya shilingi 5,000,000. Kwa mwaka huu, Idara ya Mazingira ilihusika na ukusanyaji wa ada ya hifadhi ya mazingira pekee kwa kuwa ada ya ukaguzi wa mazingira imehamishiwa kamisheni ya Utalii. Ada hii imehamishiwa kwenye taasisi hiyo kwa kuwa ilihusika na fomu za maombi ya leseni za biashara za Utalii ambazo hupitia kwenye taasisi mbali mbali kuridhia utoaji wa leseni hizo. Kwenye kifungu cha ada ya hifadhi ya mazingira hadi kufikia mwezi wa Mei 2012, Idara ya Mazingira  imeweza kukusanya Shilingi 5,978,000 sawa na asilimia 149 ya kifungu hicho.

MALENGO KWA MWAKA 2012/2013
77.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-

1.      Kudhibiti uchafuzi wa mazingira.
2.      Kusimamia uingizwaji wa masuala ya mazingira katika miradi ya maendeleo.
3.      Kuongeza uwezo na kuimarisha muundo wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
4.      Kuimarisha usimamizi endelevu wa maliasili.
5.      Kuongeza uelewa wa elimu ya mazingira kwa jamii na wadau wengine.
6.      Kuimarisha utekelezaji wa Sera, Sheria na Kanuni za mazingira.
7.      Kuimarisha mazingira ya kazi na kuwajengea uwezo wafanyakazi.

78.  Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shillingi 369,369,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo shilingi 112,373,000 ni kwaajili ya kuendeshea kazi na shilingi 257,296,000 ni kwaajili ya mishahara

79.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Mazingira kwa mwaka wa fedha 2012/2013, imepangiwa kukusanya jumla ya shillingi 10,800,000.00 ambazo zitatokana na ada ya hifadhi ya mazingira ikwa ni pamoja na vyeti vya Mazingira.

IDARA YA WATU WENYE ULEMAVU
80.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Watu Wenye Ulemavu ina majukumu ya kuratibu masuala mbali mbali ya watu wenye ulemavu, pia inafanya kazi na Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu ambalo linaishauri Serikali kuhusu maendeleo ya watu wenye ulemavu kwa mujibu wa Sheria No. 9 ya mwaka 2006.

81.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Watu Wenye Ulemavu kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilijipangia malengo yafuatayo:-

  1. Kuendeleza usajili wa Watu wenye Ulemavu kwa kupata taarifa zinazohitajika juu ya watu wenye ulemavu.
  2. Kuongeza uelewa wa jamii juu ya Sera, Sheria na Mikataba ya Kimataifa ya haki za watu wenye ulemavu.
  3. Kujenga uwezo wa Idara, Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu Zanzibar na Jumuiya za Watu wenye Ulemavu.
  4. Kuratibu Shughuli za Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu Zanzibar.

82.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Idara ya Watu Wenye Ulemavu imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

83.  Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza usajili wa Watu Wenye Ulemavu, Idara imeweza kusajili watu wenye ulemavu katika mikoa yote miwili ya Pemba. Jumla ya watu 6,445 wenye ulemavu tofauti wamesajiliwa. Kati ya hao wanaume 3,556 na wanawake 2,878. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 9). Kabla ya kufanya usajili, mafunzo yalitolewa kwa masheha 121, wakusanyaji taarifa 25 na wasimamizi wa usajili 4. Kwa ajili ya kushajihisha na kuwafichuwa watu wenye ulemavu.

84.  Mheshimiwa Spika, katika kuongeza uelewa wa jamii juu ya Sera, Sheria na Mikataba ya Kimatafa ya Haki za Watu wenye Ulemavu, Idara inaendelea kuifanyia mapitio Sheria ya Watu wenye Ulemavu. Vikao vitano vya awali vimefanyika vya kupitia Sheria No. 9  ya mwaka 2006 ya watu wenye ulemavu  ambavyo viliwashirikisha wadau mbali mbali wa Unguja na Pemba.

85.  Mheshimiwa Spika, katika kuhamasisha mambo mbali mbali ya Watu wenye Ulemavu na kwenda sambamba na utekelezaji wa Mikataba ya Kimataifa ya Watu Wenye Ulemavu, Idara imefanikiwa kuadhimisha siku ya Kimataifa ya Watu wenye Ulemavu, tarehe 3/12/2011 katika kiwanja cha Mahonda Wilaya ya Kaskazini “B”, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

86.   Mheshimiwa Spika, Idara imefanikiwa kushawishi uanzishwaji wa maafisa waratibu wa masuala ya watu wenye ulemavu ili kusaidia taasisi husika kuingiza masuala ya Watu wenye Ulemavu katika mipango ya taasisi za Serikali. Jumla ya maafisa waratibu 16 tayari wapo katika wizara zetu. Vile vile Idara ilitoa mafunzo juu ya uingizwaji wa masuala ya watu wenye ulemavu kwa maafisa hao. Aidha Idara kwa kushirikiana na “Save the Children” imetoa mafunzo juu ya haki na uhifadhi wa mtoto kwa watu 80 wakiwemo wazazi, walezi na watoto wenye ulemavu katika mikoa miwili ya Pemba. Idara imeweza kuandaa vipindi 15 vya Radio na viwili vya TV kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), Zenji FM na Radio Istiqama Pemba. (Tafadhali rejea kiambatanisho Nam. 4)

87.  Mheshimiwa Spika, katika kujenga uwezo wa Idara na Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu, Idara imeweza kununua vifaa vya ofisini kama vile samani za Ofisi na vifaa vya utendaji kwa wafanyakazi wake. Aidha Idara imemlipia mafunzo mfanyakazi mmoja katika ngazi ya Diploma ya kompyuta.

88.  Mheshimiwa Spika, kwa kutambua mchango wa Jumuiya za Watu wenye Ulemavu katika suala zima la kutetea haki na kuhakikisha Jumuiya za Watu wenye Ulemavu zinakuwa na nguvu kiutendaji na kiuwezo, Idara imeweza kutoa ruzuku kwa Jumuiya tisa (9) za Watu wenye Ulemavu  pamoja na kuwapatia visaidizi (viti vyenye magurudumu mawili) watu 31  Unguja na Pemba.  (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam.10a na b)

89.  Mheshimiwa Spika, katika kuratibu shughuli za Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu, Idara imefanya vikao vinne vya Baraza la Taifa la Watu Wenye Ulemavu na kujadili mambo mbali mbali yanayohusu maendeleo ya Watu wenye Ulemavu hapa Zanzibar.

90.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Watu Wenye Ulemavu kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikadiriwa kutumia Shilingi 177,995,000 kwa kazi za kawaida hadi kufikia Mei 2012 ilikwisha ingiziwa shilingi 139,424,888 sawa na asilimia 78.3 kati ya hizo shilingi 85,258,000 sawa na asilimia 62 kwa ajili ya kuendeshea kazi Shilingi 54,166,888 sawa na asilimia 127 kwa ajili ya mishahara.

MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
91.  Mheshimiwa Spika, Idara ya Watu Wenye Ulemavu kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-
  1. Kuratibu shughuli za Baraza la Taifa la Watu wenye Ulemavu.
  2. Kuwapatia visaidizi na kuimarisha juhudi za taasisi zinazoshughulikia masuala ya watu wenye ulemavu.
  3. Kuanzisha mfumo wa taarifa za Watu wenye Ulemavu.
  4. Kuandaa na kusimamia utekelezaji wa sera, sheria na kanuni za Watu wenye Ulemavu.
  5. Kuimarisha mazingira mazuri ya kazi na kujenga uwezo wa wafanyakazi katika kuleta ufanisi.

92.  Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia Idara ya Watu Wenye Ulemavu kwa mwaka fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 532,562,000 kwa kazi za kawaida. kati ya hizo 96,992,000 ni mishahara na 435,570,000 ni matumizi ya kuendeshea kazi.

TUME YA KURATIBU NA UDHIBITI WA DAWA ZA KULEVYA
93.  Mheshimiwa Spika, Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya  ina jukumu la kuratibu mapambano dhidi ya matumizi, biashara na usafirishaji wa  dawa za kulevya kwa  kushirikiana na wadau mbali mbali, kutoa taaluma kwa jamii juu ya athari ya dawa za kulevya na kutoa huduma za tiba na  ushauri nasaha kwa watumiaji wa dawa za kulevya.

94.  Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa Fedha 2011/2012 Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya ilijipangia malengo yafuatayo:-

1.    Kuwasilisha mswaada wa marekebisho ya Sheria ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya Zanzibar katika ngazi zinazo husika.
2.                Kuwajengea uwezo watendaji wa Sekta ya Dawa za Kulevya.
3.                Kuendeleza upigaji vita vya dawa za kulevya.
4.                Kuandaa Sera ya Dawa za Kulevya.
5.    Kupunguza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa watumiaji wa dawa za kulevya.
6.    Kuziendeleza juhudi za Taasisi zisizo za kiserikali (NGOs) zinazotoa huduma za makaazi na marekebisho kwa vijana wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya (Sober Houses).

95.  Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za kulevya imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

96.  Mheshimiwa Spika, Tume imeweza kufanya mapitio ya Sheria Nam.9 ya mwaka 2009 ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya Zanzibar. Rasimu ya Mswada wa Marekebisho ya Sheria hiyo ilipitiwa na wadau wa ngazi mbalimbali kabla ya kupitishwa na Baraza lako tukufu.

97.  Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha shughuli za uhamasishaji na ufuatiliaji wa mambo mbalimbali ya kikazi, jumla ya vespa nne (4) zimenunuliwa. Na kwa upande wa kujenga uwezo wa watendaji, wafanyakazi watatu wameweza kupata mafunzo ya muda mrefu juu ya dawa za kulevya ndani na nje ya nchi kwa ufadhili wa taasisi ya “Center for Disease Control” ya Marekani, Serikali ya Australia na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

98.  Mheshimiwa Spika, Tume iliweza kuandaa programu na ziara za uhamasishaji upigaji vita dawa za kuleva kupitia vyombo vya habari na kuzitembelea shehia mbalimbali za Unguja na Pemba. Jumla ya vipindi 41 vilirushwa hewani, vipindi 24 katika radio na 17 katika televisheni. Jumla ya shehia 17 zilifanyiwa ziara za uhamasishaji na taaluma juu ya athari ya dawa za kulevya, kati ya hizo tisa Unguja na nane Pemba zenye wastani wa watu 783. Aidha wanafunzi 5,422 katika Skuli 28 walipatiwa taaluma hiyo. Kati yao wasichana ni 2991 na wavulana 2431, wengi wao ni wenye umri kati ya miaka 12 hadi 18. Pia walimu 97 walifaidika na taaluma hiyo.
 
99.  Mheshimiwa Spika, Tume kwa kushirikiana na taasisi ya Umoja wa Mataifa ya Dawa za Kulevya na Uhalifu  kanda ya Afrika Mashariki ( United Nations Office on Drugs and Crime  Regional Office for Eastern Africa- UNODC-ROEA)   ilifanya semina maalum ya siku moja ya uhamasishaji upigaji vita biashara na matumizi ya dawa za kulevya kwa wajumbe wa Baraza lako Tukufu. Pia kwa kutambua umuhimu wa taasisi za kidini katika jamii, Tume kwa kushirikiana na taasisi ya “American International Health Alliance” (AIHA) iliandaa semina juu ya dawa za kulevya kwa mtandao wa taasisi za dini mbali mbali unaoratibiwa na Ofisi ya Mufti  Unguja na Pemba. Jumla ya washiriki 84 walinufaika na mafunzo hayo. Lengo hasa ni kuwapa mwamko zaidi na kusaidia kuendelea na juhudi zao za kila siku za kuwaasa vijana, waumini na jamii kwa jumla juu ya athari ya dawa za kulevya.

100. Mheshimiwa Spika, Uandaaji wa Sera ya Dawa za Kulevya haukuweza kukamilika kama ilivyotarajiwa kutokana na kuchelewa kupata fedha zilizoahidiwa na wafadhili. Hata hivyo shughuli hiyo imeshaanza na imo katika hatua za awali za ukusanyaji wa maoni ya wadau.

101. Mheshimiwa Spika, Tume kupitia kituo chake cha ushauri nasaha kilichopo mtaa wa Sogea kiliweza kutoa huduma kwa jamii na watumiaji wa dawa za kulevya wapatao 984 wakiwemo wanawake 510, na wanaume 474. Kati ya hao 97 walikuwa ni watumiaji wa dawa za kulevya (wanaume 82 na wanawake 15). Aidha, watu tisa (9) kati yao waligundulika na virusi vya UKIMWI, (w/ke 4, w/me 5). Kupitia huduma za kuwafikia wateja (outreach programme) katika maeneo yao (maskani), jumla ya wateja 125 (wanawake 20, wanaume 105) waliweza kufikiwa katika maeneo mbali mbali (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 11).

102. Mheshimiwa Spika, Kwa kutambua mchango wa taasisi zisizo za kiserikali katika suala zima la mapambano dhidi ya dawa za kulevya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kupitia Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya ilizipatia jumla ya shillingi 9,900,000 nyumba tisa (9) za makaazi ya vijana wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya (Sober Houses) pamoja na seti ya Televisheni na Radio Unguja na Pemba. Jumla ya vijana 501 walipata huduma katika makaazi hayo. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam.12a, b na c)

103. Mheshimiwa Spika, Tume kwa kushirikiana na taasisi ya AIHA iliweza kutoa mafunzo ya uongozi na uwekaji wa kumbukumbu za kifedha kwa taasisi zinazotoa huduma za makaazi ya vijana wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya (Sober Houses) Unguja na Pemba. Jumla vijana 45 (wanawake 6, wanaume 39) walifaidika na mafunzo hayo. Aidha mafunzo ya programu ya upataji nafuu (Recovery Oriented System of Care –ROSC) yalitolewa kwa wadau mbali mbali, wakiwemo watendaji wa Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Chuo cha Mafunzo, jumla ya washiriki 75 kutoka Unguja na Pemba walifaidika na mafunzo hayo.

104. Mheshimiwa Spika, Tume imekamilisha rasimu ya muongozo wa nyumba za marekebisho za makaazi ya vijana wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya. Aidha, Tume iliweza kuandaa mkutano wa mapitio ya Katiba ya Jumuiya ya vijana walioacha matumizi ya dawa za kulevya (Drug Free Zanzibar) na kusimamia uchaguzi wa taasisi hiyo. Tume kupitia programu yake ya Family Therapy  imekuwa ikikutana na wazee, familia na jamaa ili kubadilishana mawazo, kuwapa ushauri na kuzungumzia mafanikio na changamoto mbali mbali. Mikutano minne na wanafamilia iliyokuwa na wastani wa watu wapatao 3,022 ilifanyika.

105. Mheshimiwa Spika, Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikadiriwa kutumia shilingi 142,527,000 kwa kazi za kawaida, hadi kufikia Mei 2012 ilikwisha ingiziwa shilingi 138,965,297 sawa na asilimia 97.5 kati ya hizo shilingi 62,200,000 sawa na asilimia 73 kwa ajili ya kuendeshea kazi Shilingi 76,765,297 sawa na asilimia 134 kwa ajili ya mishahara.

MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013
106. Mheshimiwa Spika, Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo;
1.      Kuratibu na kuendeleza mapambano dhidi ya uingizaji na usafirishaji wa dawa za kulevya.
2.      Kuongeza mwamko wa jamii juu ya athari na udhibiti wa dawa za kulevya.
3.      Kuimarisha utoaji wa huduma za tiba kwa watumiaji wa dawa za kulevya.
4.      Kuanzisha mfumo wa taarifa za dawa za kulevya.
5.      Kuratibu na kuimarisha juhudi za taasisi katika kushughulikia mapambano dhidi ya dawa za kulevya.
6.       Kuimarisha mazingira mazuri ya kazi katika kuleta ufanisi.

107. Mheshimiwa Spika, Ili kutekeleza malengo iliyojipangia Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 247,091,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo Shilingi 146,607,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kuendeshea kazi na Shilingi 100,684,000 ni kwa ajili ya mishahara.

OFISI KUU PEMBA

108. Mheshimiwa Spika, Ofisi Kuu Pemba ina jukumu la kuratibu, kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa shughuli zote za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kwa upande wa Pemba.

109. Mheshimiwa Spika, Ofisi Kuu Pemba kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilijipangia malengo yafuatayo:-

  1. Kuratibu na Kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Pemba.
  2. Kuimarisha mazingira ya Utendaji kazi.
  3. Kujenga uwezo wa wafanyakazi.
110. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Ofisi Kuu Pemba imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

111. Mheshimiwa Spika, Ofisi Kuu Pemba imeweza kuratibu ziara mbali mbali za Viongozi zikiwemo ziara za Makamu wa Kwanza wa Rais, ziara za Kamati ya Baraza la Wawakilishi ya kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa na ziara za Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais. Pia Ofisi Kuu Pemba iliratibu ziara ya Mwakilishi wa Idara ya Maendeleo ya Kimataifa ya Uingereza (UK-Department for International Development -DFID) katika maeneo yanayoendeleza juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Aidha, Ofisi ilisimamia utekelezaji wa msaada uliotolewa kwa ajili ya kuendeleza huduma kwa vijana  wanaoendelea  kupata nafuu  ya kujikinga na matumizi ya dawa  za kulevya  katika nyumba za kurekebisha  tabia (Sober Houses).  Mikutano ya operesheni ‘Mifuko ya Plastiki’ kwa Mikoa ya Kusini na Kaskazini Pemba nayo pia iliratibiwa.

112. Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuimarisha mazingira ya utendaji kazi, Ofisi Kuu Pemba iliweza kununua vifaa mbali mbali kwa ajili ya matumizi ya Ofisi vikiwemo kompyuta na samani pamoja na kuunganisha mitandao ya mawasilisano. Pia Ofisi Kuu Pemba imeweza kuimarisha Ofisi ya Idara ya Watu Wenye Ulemavu kwa kuwapatia Ofisi yenye mazingira rafiki wanayoweza kuitumia bila usumbufu.

113. Mheshimiwa Spika, Ofisi Kuu Pemba kwa mwaka wa Fedha 2011/2012 ilikadiria kutumia jumla ya shilingi 214,115,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo Shilingi 135,875,000 kwa ajili ya kuendeshea kazi na Shilingi 78,240,000 kwa ajili ya mishahara Hadi kufikia Mei, 2012 ilikwisha kuingiziwa kiasi cha Shilingi 218,472,625 sawa na Asilimia 102 kati ya hizo shilingi 95,242,000 sawa na asilimia 70 kwa ajili ya kuendeshea kazi Shilingi 123,230,625 sawa na asilimia 158 kwa ajili ya mishahara.

MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013

114. Mheshimiwa Spika, Ofisi Kuu Pemba  kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-

  1. Kuratibu na Kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Pemba. 
  2. Kuimarisha mazingira ya kazi na kuwajengea uwezo wafanyakazi.
  3. Kukuza na kuimarisha mawasiliano ya habari.
  4. Kusimamia na kuratibu udhibiti wa matumizi ya fedha.

115. Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia Ofisi Kuu Pemba kwa mwaka fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shillingi 316,659,000 kwa kazi za kawaida. Kati ya hizo Shilingi 157,774,000 kwa ajili ya kuendeshea kazi na shilingi 158,596,000 kwa ajili ya mishahara.

TUME YA UKIMWI

116. Mheshimiwa Spika, majukumu makuu ya Tume ya UKIMWI ni kuhakikisha kwamba sera na mikakati ya taifa ya kupiga vita UKIMWI zinaundwa na kutekelezwa, kutafuta rasilimali zitakazotumika katika utekelezaji wa muitiko wa kitaifa wa kupambana na UKIMWI, kuimarisha uwezo wa wadau katika kufanyia kazi programu za UKIMWI na kuratibu shughuli zao, kushajihisha utoaji wa huduma za tiba na matunzo kwa watu walioathirika na kuathiriwa, kufuatilia na kutathmini umakini na ufanisi wa utekelezaji wa mikakati, sera na muitiko wa kitaifa na kutoa taarifa zote zinazohusiana na UKIMWI.

117. Mheshimiwa Spika, Tume ya UKIMWI kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilijipangia malengo yafuatayo:-

  1. Kutekeleza Mkakati wa Pili wa kitaifa wa kupambana na UKIMWI, kwa kuzishirikisha sekta za serikali, sekta binafsi na Asasi za kiraia katika ngazi zote.
  2. Kuimarisha utekelezaji wa programu za habari, utetezi na mawasiliano kwa ajili ya kuleta mabadiliko ya tabia kwa makundi yaliyo katika hatari zaidi ya kuambukizwa na jamii kwa ujumla.
  3. Kuimarisha mipango ya ufuatiliaji, tathmini na utafiti inayohusiana na shughuli za UKIMWI na maeneo yanayohusiana nayo.
  4. Kuongeza uwezo wa Tume na wadau katika kuratibu na kutekeleza shughuli za UKIMWI kwa mfuatano huo.

118. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mei 2012 Tume ya UKIMWI imeweza kutekeleza yafuatayo katika malengo iliyojipangia:-

119. Mheshimiwa  Spika,  Tume imeweza kuzindua Mkakati wa Pili wa kitaifa wa UKIMWI Siku ya UKIMWI Duniani tarehe 1 Disemba 2011, baada ya uzinduzi, Mkakati huo  ulisambazwa kwa wadau mbali mbali kwa kuanza kuufanyia kazi. Aidha Tume imetayarisha  Mpango wa Utekelezaji wa Mkakati wa kitaifa wa UKIMWI wa mwaka 2012/13 hadi 2013/14. Pamoja na uzinduzi huo wa mkakati Tume imezinduwa Tovuti yake www.zac.or.tz

120. Mheshimiwa Spika, Tume imeweza kuzisaidia Shehia 71 katika kuandaa  mipango ya Shehia dhidi ya udhalilishaji wa jinsia na UKIMWI  (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 13). Pia Tume imewapatia mafunzo juu ya usimamizi wa masuala ya UKIMWI Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi ili kuwawezesha kuongeza usimamizi wa uwajibikaji wa sekta za Serikali kwenye masuala ya UKIMWI.

121. Mheshimiwa Spika, Tume  ya UKIMWI imeweza  kuimarisha utekelezaji wa programu za habari, utetezi na mawasiliano kwa ajili ya kuleta mabadiliko ya tabia kwa makundi maalum na jamii kwa ujumla kwa kuufanyia mapitio Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano na Utetezi ambao unaendana na Mkakati wa Pili wa kitaifa wa UKIMWI. Mkakati huo kwa sasa uko tayari  kusambazwa kwa wadau kwa matumizi .

122. Mheshimiwa Spika, ili mapambano ya UKIMWI yaimarike ushiriki na ushirikishwaji wa Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI ni jambo la lazima. Kwa kulitambua hilo, mkutano wa kitaifa uliowashirikisha viongozi katika ngazi za maamuzi kutoka sekta mbalimbali ulifanyika. Mkutano huo ulilenga kuhamasisha umuhimu wa kuwashirikisha Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI katika mipango mbalimbali ya maendeleo. Jumla ya washiriki 55 (wanaume 35, wanawake 20) walihudhuria wakiwemo Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI. Aidha jumla ya shilingi milioni 15  walipatiwa ZAPHA+ kwa ajili ya kutekeleza shughuli zao mbali mbali zinazolenga   utekelezaji wa Mkakati wa Pili wa UKIMWI. Ni matumaini ya Tume kwamba jitihada zao zitasaidia kupunguza unyanyapaa wa Watu Wanaoishi na Virusi vya UKIMWI na hatimae  maambukizi ya VVU.

123. Mheshimiwa Spika, Taasisi za Kidini zina mchango  mkubwa katika kupiga vita suala la UKIMWI. Semina mbili  za mafunzo ya viongozi wa dini zimefanyika Unguja na Pemba. Jumla ya viongozi 58 (wanaume 34, wanawake 24) wamefikiwa. Aidha, kupitia Mtandao wa Taasisi za Dini Katika Mapambano Dhidi ya UKIMWI, miongozo mbali mbali ya UKIMWI  imechapishwa. Nakala 350 za miongozo ya  afya ya uzazi na jinsia zimetolewa kwa waumini wa kiislamu na kikristo.

124. Mheshimiwa Spika, Tume ya UKIMWI pia imeweza kuandaa mikutano ya utetezi wa makundi maalum pamoja na watu wenye ulemavu Unguja na Pemba kwa kuhamasisha taasisi mbalimbali kuzingatia mahitaji ya makundi hayo katika programu mbalimbali za UKIMWI na afya kwa ujumla.

125. Mheshimiwa Spika, Tume imeendelea kuchapisha jarida la Jihadhari. Hadi kufikia Januari, toleo nambari 15 limetoka kwa kuchapishwa nakala 5,000 ambazo zimesambazwa sehemu mbalimbali. Aidha, vipeperushi 3,000 kwa ajili ya makundi maalum vimetayarishwa na kuchapishwa.

126. Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na tatizo la UKIMWI Tume ya UKIMWI imeweza kuyafikia makundi maalum  (wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao, wanawake wanaojiuza na watu wanaotumia dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga sindano)  kwa kuwapatia huduma mbalimbali za kujikinga na  UKIMWI. Makundi haya yameweza kufikiwa kwa  kuwatumia waelimishaji rika ambao wanafanya kazi katika maeneo  ambayo makundi haya yanapatikana zaidi. (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 14).

127. Mheshimiwa Spika, katika masuala ya ufuatiliaji na tathmini, Tume ya UKIMWI imeweza    kufanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa program za UKIMWI. Jumla ya vikundi 24 vyenye miradi 36 ya kujiongezea mapato vilifuatiliwa. Vile vile Tume iliweza kuandaa ripoti ya mwaka ya ufuatiliaji na Tathmini kwa shughuli za UKIMWI na ripoti ya mkutano mkuu maalum wa Umoja wa Mataifa ”United Nation General Assembly Special Session” (UNGASS). Vile vile, Tume imeweza kukusanya, kuwasilisha, kuchambua na kuhakiki taarifa za fomu zinazotumiwa na wadau mbali mbali katika kukusanya taarifa za utekelezaji wa shughuli za UKIMWI (ZHAPMoS).
                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                               
128. Mheshimiwa Spika, katika kuongeza uwezo wa wadau, Tume ya UKIMWI  imeweza kutoa mafunzo kwa asasi za kiraia na wadau wengine. Jumla ya asasi 55 zilipatiwa mafunzo ya uongozi, utetezi, ushawishi, ubia, utatuzi wa migogoro na uandishi wa ripoti.  Washiriki 15 (wanaune 9, wanawake 6) kutoka ZANGOC walipatiwa mafunzo ya jinsia na UKIMWI, waandishi wa habari na wasanii 25 (wanaume 15, wanawake 10) walipatiwa mafunzo juu ya ubunifu wa kazi za mawasiliano na  waelimishaji rika 40 (wanaume 22, wanawake18) kutoka katika makundi maalum walipatiwa mafunzo ya namna ya  kuyafikia makundi maalum. Aidha Tume imeandaa warsha ya kuwahamasisha  waheshimiwa wawakilishi na makatibu wa kamati juu ya  muitiko wa kitaifa wa kupambana na UKIMWI ili kuongeza uelewa wao.

129. Mheshimiwa Spika, Tume ya UKIMWI  imeimarisha mazingira ya utendaji kazi kwa kufanya ukarabati wa jengo lake na kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa wafanyakazi ili kuongeza ufanisi katika kutimiza  majukumu yake. Katika kipindi cha mwaka wa 2011/12, jumla ya wafanyakazi 3 walipatiwa mafunzo ya muda mrefu na wafanyakazi  6 wamepata mafunzo ya muda mfupi. (Tafadhali rejea kiambatanisho Nam. 3)

130. Mheshimiwa Spika, Tume ya UKIMWI kwa mwaka wa fedha 2011/2012 ilikadiriwa kutumia Shilingi 472,000,000 kwa kazi za kawaida hadi kufikia Mei 2012 ilikwisha ingiziwa shilingi 439,648,862 sawa na asilimia 93. Aidha Tume iliidhinishiwa Shilingi. 90,000,000 kwa kazi za maendeleo na hadi kufikia Mei 2012, ilikwisha ingiziwa Shilingi 90,000,000 sawa na asilimia 100. Kwa upande wa fedha za wahisani walitarajiwa kuchangia Shilingi 1, 300,000,000 na hadi kufikia Mei 2012, wamechangia Shilingi 705,550,000 sawa na asilimia 54.3.

MALENGO KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013

131. Mheshimiwa Spika, Tume ya UKIMWI kwa mwaka wa fedha 2012/13 imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:-

  1. Kuimarisha uratibu na utekelezaji wa Sera, Sheria na Mkakati wa Pili wa kitaifa wa UKIMWI.
  2. Kuongeza uwezo wa programu za habari, utetezi na mawasiliano ili kuchochea mabadiliko ya tabia katika jamii na makundi maalum.
  3. Kuongeza utumiaji wa taarifa zinazotokana na ufuatiliaji, tathmini na utafiti katika programu za UKIMWI.
  4. Kuimarisha mazingira ya kazi ili kuleta ufanisi.
  5. Kusimamia utaratibu wa udhibiti wa matumizi ya fedha .

132. Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza malengo iliyojipangia Tume ya UKIMWI kwa mwaka fedha 2012/2013 inatarajia kutumia jumla ya Shilingi 739,000,000 kwa kazi za kawaida, kati ya hizo shilingi 500,838,000 kwaajili ya kuendeshea kazi na shilingi 238,162,000 kwaajili ya mishahara Aidha inatarajia kutumia Shilingi 50,000,000 kwa kazi za maendeleo na Shilingi 893,760,000 kutoka kwa wahisani.

SHUKURANI

133. Mheshimiwa Spika, kabla ya kumaliza hotuba yangu naomba kuwashukuru wote waliofanikisha ukamilishaji wa kazi hii. Pia napenda kuchukua fursa hii kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika kwa Uongozi wako makini wa kuliongoza Baraza hili tukufu katika awamu hii ya saba pamoja na Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wa Baraza. Aidha, bila ya kuwasahau naomba niwashukuru kwa dhati kabisa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako tukufu kwa kuwa wasikivu na wastahamilivu wakati wote nilipokuwa nikiwasilisha hotuba yangu. Ni matumaini yangu kwamba tutaendelea kushirikiana katika kutoa michango mbali mbali ambayo itasaidia Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kutatua matatizo yanayoathiri jamii. Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais inaahidi kuichukua michango yote itakayotolewa na Wajumbe wa Baraza hili na kuifanyia kazi kwa maslahi ya Jamii na Taifa kwa ujumla.

134. Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa nchi marafiki, mashirika ya Kimataifa na watu binafsi kwa kuendelea kutusaidia kuendeleza shughuli za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais. Nchi hizo ni pamoja na Marekani, Finland, Norway, Uingereza, Uholanzi, Australia, China, Brazil, India na Falme za nchi za Kiarabu na Oman. Pia mashirika ya kimataifa yakiwemo UNDP, UNICEF, UNFPA, UNAIDS, UNEP, UNODC, UNFCCC, WHO, World Bank, AIHA, CDC, ICAP, Save the Children na nchi na mashirika mengine ambayo sikuyataja, lakini kwa njia moja au nyengine yanatuunga mkono katika shughuli zetu za maendeleo. Juhudi na michango yao tunaithamini sana.

135. Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako tena natoa shukrani zangu kwa Viongozi wakuu wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa na Taasisi  mbali mbali  za Serikali  zikiwemo vyombo  vya ulinzi  na usalama   na taasisi zisizo za kiserikali zinazojishughulisha na masuala ya UKIMWI, mapambano dhidi ya dawa za kulevya, utunzaji na uhifadhi wa mazingira na kutetea haki na fursa za watu wenye ulemavu. Taasisi hizi zinatoa mchango mkubwa na mashirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, mashirikiano yao yanasaidia kuleta  ufanisi katika utekelezaji  wa  majukumu ya Ofisi yetu. Nawaomba waendelee kutupa mashirikiano hayo kwa lengo la  kuwatumikia  wananchi  wa Zanzibar na kufikia lengo kuu la kukuza uchumi na kupambana na umasikini.

136.Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais inatoa shukurani za dhati kwa vyombo vya habari vyote ambavyo tumekuwa tukishirikana navyo kuielemisha jamii juu ya athari za uharibivu wa mazingira, matumizi ya dawa za kulevya, namna ya kujikinga na VVU na UKIMWI na umuhimu wa kuwahudumia watu wenye ulemavu. Ni matumaini yetu kuwa tutaendeleza mashirikiano haya kwa faida ya jamii yetu sote.

137. Mheshimiwa Spika, shukurani za pekee ziwaendee wote walioshiriki kwa njia moja au nyengine katika kufanikisha utekelezaji wa kazi za Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais. Mwisho napenda kuwashukuru wananchi wote kwa ujumla kwa kufanikisha kazi za maendeleo ya nchi yetu.

HITIMISHO

138.Mheshimiwa Spika, kwa heshima nachukuwa nafasi hii kuwaomba Wajumbe wa Baraza lako tukufu waipokee, waijadili, watushauri, watuelekeze na hatimae kuidhinisha matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ya jumla ya shilingi bilioni mbili milioni mia saba na sabini (T.Shs. 2,770,000,000) kwa mwaka wa fedha 2012/2013. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni moja milioni mia tano kumi na tano (T.Shs. 1,515,000,000) kwa ajili kuendeshea kazi na shilingi bilioni moja milioni mia mbili hamsini na tano (TShs.1,255,000,000) kwa ajili ya mishahara. Aidha tunaliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya shilingi milioni mia mbili hamsini na tano (T.Shs. 255,000,000) kwa kazi za maendeleo ikiwa ni mchango wa Serikali na Shilingi milioni mia saba na tano na laki sita (T.Shs 705,600,000) fedha za wahisani (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 15 a na b).

139. Mheshimiwa Spika, aidha, naliomba Baraza lako tukufu liidhinishie Tume ya UKIMWI matumizi ya jumla ya shilingi milioni miasaba thelathini na tisa (T.Shs. 739,000,000) kwa kazi za kawaida, ambapo shilingi milioni mia tano laki nane thelathini na nane elfu (T.Shs. 500,838,000) kwa ajili ya kuendeshea kazi na shilingi milioni mia mbili thelathini na nane laki moja sitini na mbili elfu (TShs.238,162,000) kwa ajili ya mishahara. Aidha tunaliomba Baraza lako tukufu kuidhinisha jumla ya shilingi milioni hamsini (T.Shs. 50,000,000) kwa kazi za maendeleo ikiwa ni mchango wa Serikali na shilingi milioni mia nane tisini na tatu lakisaba sitini elfu (T.Shs 893,760,000) mchango wa wahisani (Tafadhali angalia kiambatanisho Nam. 15 c na d).

140. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.