Habari za Punde

Mgogoro mpya Ziwa Nyasa Malawi yatangaza kujiondoa kwenye mazungumzo



 LILONGWE, Malawi

 RAIS wa Malawi, Joyce Banda, ameiondoa nchi yake katika mazungumzo ya mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa na Tanzania, kutokana na kile anachodai kuwa uchokozi, ubabe  na vitisho vinavyofanywa na serikali ya Tanzania dhidi ya raia wake.

Rais Banda alisema Malawi sasa itaufikisha mgogoro huo katika mahakama ya kimataifa.

Nchi hizo mbili ziliingia katika mvutano mkubwa wa Ziwa hilo, ambalo linaaminika kuwa na rasilimali kubwa ya mafuta na gesi.

Rais Banda alisema amemuagiza Waziri wake wa Mambo ya Nje,kuvunja kabisa mazungumzo na Tanzania baada ya nchi hiyo kutangaza rasmi uzinduzi wa ramani mpya katika eneo la Ziwa hilo.

Aidha alisema nchi yake haitavumilia unyanyasaji unaofanywa na Tanzania dhidi ya raia wake wanaofanya shughuli za uvuvi katika Ziwa hilo.

Banda alitoa kauli hiyo wakati alipowasili mjini Lilongwe akitokea mjini New York, Marekani alikokwenda kuhudhuria mkutano wa Baraza kuu la Umoja wa Mataifa.


“Wakati naondoka kwenda New York, nilifikiria kuwa mgogoro huu ungemalizwa kwa njia ya mazungumzo,” alisema.

“Lakini wakati nipo njiani, Tanzania walizindua ramani mpya, wamewadhalilisha, kuwatisha  na kuwabugudhi wavuvi wetu na wanatembea na boti zao katika Ziwa letu,” alisema kwa uchungu mama huyo.

“Suala limekuwa tete sasa na tunalichukua katika hatua nyengine. Tanzania imetishia kushambulia boti za Malawi zitakazoonekana katika Ziwa Nyasa,” alisema Banda.

Kiongozi huyo wa Malawi alisema alifanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-moon na kumjulisha juu ya nia ya Malawi ya kulifikisha suala hilo katika mahakama ya kimataifa ya usuluhisi wa migogoro.

Banda alisema katika mazungumzo yake na Rais Kikwete walipokutana katika mkutano wa SADC walikubaliana kumaliza mgogoro huo kwa njia ya mazungumzo.

Hali katika mpaka wa nchi hizo mbili bado uko swahari, lakini uamuzi huo wa Banda huenda unaashiria kuwa mgogoro huo umeingia katika sura mpya.
Wakati huo huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki Moon amepongeza msimamo wa Tanzania kutafuta majawabu ya amani na ya kujadiliana kuhusu mzozo wa mpaka kati yake na Malawi kwenye Ziwa Nyasa.

Ki Moon alisema uamuzi wa Tanzania ndiyo njia sahihi na inayokubaliwa kimataifa kutafuta na kupata suluhisho la migogoro ya namna hiyo.

 “Majuzi nilikutana na Rais Joyce Banda wa Malawi na akanielezea mzozo wa mpaka kati ya Tanzania na Malawi kwenye Ziwa Nyasa na mazungumzo ambayo nchi zenu mbili zinafanya ili kupata ufumbuzi wa amani. Hii ndiyo njia sahihi na Umoja wa Mataifa unaunga mkono njia hiyo,” alisema.
Rais Kikwete amemweleza Katibu Mkuu huyo wa UN kuwa Tanzania bado inaamini kuwa njia sahihi na maelewano zaidi ni kutafuta ufumbuzi wa mvutano huo wa mpaka kwa njia ya mazungumzo.

 “Wazo la awali la kutafuta ufumbuzi wa tatizo hili la miaka mingi sana lilitokana na Rais wa Malawi, marehemu Bingu wa Mutharika ambaye aliniandikia barua ya kutaka nchi zetu zianze mazungumzo kuhusu mzozo huo. Nasi tulikubali. Hivyo, ndivyo tulivyoanza kuzungumza,”
alisema Rais Kikwete.

Alisema Tanzania inaongozwa na msingi mkuu wa mipaka inayopita kwenye maeneo ya maji ambako mipaka hiyo inakuwa katikati.

“Mpaka kati ya Malawi na Msumbiji kwenye ziwa hilo hilo, umekuwa katikati ya Ziwa tokea mwaka 1954 wakati nchi hizo zilipokubaliana kusahihisha makosa ya kuuweka mpaka huo nje ya Ziwa. Mpaka wa Tanzania na Malawi kwenye mto mkubwa zaidi unaoingiza maji katika Ziwa Nyasa uko katikati ya mto wenyewe,” alisema Kikwete.

 “Kila mahali ambako nchi zinatengenishwa na maji, mpaka unakuwa katikati ya nchi. Sisi tunadhani hata kwenye mpaka wetu wa Malawi kwenye Ziwa Nyasa ni lazima uwe katikati ya Ziwa,” alisema.

Lakini alisema katika hali ya sasa wananchi wa Tanzania wanapokunywa maji ya Ziwa Nyasa wanaambiwa wanakunywa maji ya Malawi, kila wanaposafiri ndani ya Ziwa kufanya shughuli zao wanaambiwa wanasafiri kwenye maji ya Malawi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.