Habari za Punde

Serikali kuzipa ulinzi nyumba za ibada.

Dk. Shein asisitiza wahalifu kusakwa.

Padri Mushi kuzikwa kesho

Na Waandishi wetu

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imetangaza kuzipa ulinzi nyumba zote za ibada na kusakwa mtandao mzima wa mauaji ya Padri  Evaristus Gabriel Mushi baada ya serikali kuikabidhi kazi hiyo kwa wapelelezi wa ndani na wa kimataifa.

Imesema kuwa tangu timu hiyo kuanza kazi tayari idadi ya washukiwa waliokamatwa kutokana na mauaji hayo imeongezeka ambapo hivi sasa wanahojiwa.

Hatua hiyo ya serikali imetangazwa jana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohammed, ofisini kwake Vuga mjini Zanzibar.

Padri Mushi, aliuawa kwa risasi  juzi asubuhi wakati akijitayarisha kwenda kuendesha misa katika kanisa Katoliki, Parokia ya Mtakatifu St. Joseph, Beir El Ras.

Waziri Aboud  alisema serikali imepokea kwa masikitiko makubwa muendelezo wa matukio ya mauaji ya viongozi wa dini, na kuwataka viongozi makanisa, waumini wa dini ya kikristo na wananchi kuwa watulivu kwani serikali itatumia wapelelezi wa kimataifa kuunasa mtandao wote uliohusika na mauaji hayo. 

Alisema serikali imeamua kutumia wataalamu hao kwa vile kiwango chao cha upelelezi ni cha hali ya juu katika matukio ya mauaji.


Alisema wapelelezi hao wanatarajiwa kuendesha uchunguzi huo katika maeneo mbali mbali ya visiwa vya Zanzibar zikiwemo bandari bubu baada ya kuonekana ni moja ya maeneo ambayo hupenda kutumiwa na wahalifu wa matukio hayo.

Hata hivyo, alifahamisha kuwa serikali haitataja wapelezi hao walipotoka lakini tayari wameanza kukamata watu zaidi ambao wanaendelea kufanyiwa mahojiano.

Alisema serikali imedhamiria kuzika mtandao huo baada ya kuonekana vitendo hivyo vinaongezeka na kuenea katika jamii jambo ambalo limekuwa likiwatia hofu wananchi na viongozi wa dini.

 Akifafanua zaidi alisema vipo vikundi vya watu ambavyo lengo lao kubwa kuona kwamba wananchi wa Zanzibar wanaingia katika chuki za kidini.

Alisema chuki hizo ni pamoja na kuchoma makanisa na kuwaua viongozi wa dini na kuifanya Zanzibar kuwa haitawaliki tena katika misingi ya sheria na imani za dini.


Alisema wakati serikali ikilifanyia kazi suala hilo ni vyema kwa waumini wa dini kuona wanakuwa watulivu ili kuhakikisha amani ya nchi inaendelea kudumishwa.

Aidha, aliwataka wageni na wawekezaji kuendelea kuja nchini kwani mazingira ya Zanzibar bado yako salama na hakuna mtu ataeweza kudhuriwa.

Alisema tayari kuna watu wamekamatwa wakiwa na silaha katika bandari bubu ya Nungwi wilaya ya Kaskazini ‘A’ Unguja.

 Wakati huo huo akizungumza na waandishi wa habari, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki jimbo la Zanzibar, Mhashamu Augostino Shao amesema Padri Mushi  atazikwa kesho  katika makaburi ya Kitope.

Alisema ibada ya mazishi  itafanyika katika kanisa katoliki la Minara miwili Shangani mjini Zanzibar.

Alisema Padri Mushi analazimika kuzikwa Zanzibar kwa mujibu wa sheria za kanisa zinavyoelekeza.

Shao alisema sheria hizo zinaelekeza kuwa Padri na mali zake ni mali ya kanisa  na sio familia hivyo ndio sababu ya marehemu Padri Mushi kuzikwa Zanzibar na sio Moshi nyumbani kwao.

“ Padri Mushi amekaa Zanzibar tangu ana miaka 18, Upadri kapewa katika Jimbo la Zanzibar ambalo lina madaraka kamili halitegemei jimbo jengine hivyo anapaswa kuzikwa hapa alipokuwa akiwatumikia waumini wake na si pengine popote,” alifafanua.

Alisema Kanisa tayari limeshajitayarisha kwa maziko hayo ambayo yatahudhuriwa na  waumini wa kanisa hilo na makanisa mengine, viongozi mbali mbali wa ndani na nje ya nchi huku likizingatia suala zima la usalama kwa kushirikiana na vyombo husika.

Akizungumzia kuhusu hali iliyopo hivi sasa visiwani Zanzibar, Askofu Shao alisema matukio ya kihalifu yanayotokea anaamini kuwa ni mbinu zinazopangwa nje ya Zanzibar kwa vile Wakristo na Waislamu wa Zanzibar kwa miaka mingi wamekua wakiishi kwa kusikilizana na kusaidiana bila ya kujua tofauti za dini zao.

“ Haya yanayotokea ni dhahiri kuwa yamepangwa nje ya nchi kwani wenzetu hawafurahi kusikia Tanzania ni nchi ya amani ndio maana wanaamua kufanya kila jambo kuhakikisha kuwa tunaingia katika mfarakano wa wenyewe kwa wenyewe,” alieleza Shao.

Alisema ni vyema vyombo husika vikawajibika ipasavyo katika majukumu yao ya kazi kwa lengo la kuliondoa tatizo hilo.

Aidha alisema tatizo sio uislamu wala ukristo tatizo ni suala la kuwadhibiti wahalifu kwani katika dini yoyote wapo wahalifu hivyo ni vyema vyombo husika vikaacha kufanya kazi kwa kujuana.

Askofu Shao akizungumzia suala la kuletwa wataalamu wa masuala ya uchunguzi kutoka nje ya nchi alisema suala hilo haliafiki kwa sababu nchi inapofikia hatua ya kutaka msaada kutoka nje ni dhahiri kuwa haina usalama jambo ambalo linaweza kusababisha kuwekewa vikwazo mbali mbali ikiwemo misaada na vikwazo vya kiuchumi.

Aidha aliitaka serikali kuhakikisha wahalifu wa matukio mbali mbali wanakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria bila ya kujali nani alihusika katika matukio hayo.

Alikielezea kifo cha marehemu Mushi, alisema ni pengo kubwa katika kanisa hilo ambapo yeye alikuwa akijishungulisha zaidi na masuala ya kukuza maendeleo elimu katika kanisa hilo.


Akielezea jinsi alivyopokea taarifa ya kifo cha msaidizi wake mkuu,Shao alisema wakati alipokuwa akiendesha ibada ya kawaida ya Jumapili hapo kanisa la minara miwili akiwa katikati ya ibada hiyo alipokea taarifa ya kifo cha marehemu Mushi.

 “Unajuwa mimi nilikuwa naongoza ibada lakini wenzangu tayari walikuwa wamepata taarifa ya kifo cha marehemu Mushi,ambaye nilikuwa naye asubuhi saa 12:00  tukiagana yeye akielekea kuongoza misa huko Mtoni katika kanisa liliopo eneo la Beit-el-Ras,” alisema.

Askofu Shao akifafanua matukio ya hujuma kwa viongozi wa dini ya kikristo alisema hivi sasa uvumilivu wa kidini Zanzibar umeanza kutoweka kidogo kidogo, tofauti na miaka ya nyuma ambapo Zanzibar ilikuwa ikisifika kuwa kisiwa chenye watu wenye dini tofauti wanaoishi pamoja kama ndugu huku wakipendana.

Alisema wapo watu wenye dhana kwamba  Zanzibar iwe nchi ya kiislamu na kuongeza kwamba watu hao wanakosea sana kwa sababu hata huo mji mtakatifu wa  makka  wapo waumini wa madhehebu mbali mbali ambao wanaishi kwa kuheshimiwa kwa mujibu wa imani zao.
Aliwataka wananchi kutumia mchakato wa mabadiliko ya katiba kutoa maoni yao kwa uwazi na uhuru huku wakibainisha mambo ambayo wanaona ni kero kwao.

Aidha, Shao, alivitaka vyombo vya ulinzi kufanya kazi za kuwasaka wahalifu kwani jamii wa wakristo tayari wameanza kupoteza imani kwa taasisi hizo.
Kwa upande wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameelezea kupokea kwa mshtuko mkunwa mauaji ya Padri Evaristitus Mushi  na kutoa pole kwa  waumini, ndugu jamaa, marafiki na wananchi wote wa Zanzibar kufuatia kifo hicho.
Katika taarifa yake kupitia Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud, Dk. Shein alisema   serikali kwa kushirikiana na jeshi la polisi itawasaka hadi kuwatia mikononi na hatimaye kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wale wote waliohusika na mauaji hayo.

Hapo jana Dk. Shein alikutana na Askofu Shao katika Ikulu ndogo Migombani na kueleza masikitiko yake kutokana na kifo hicho cha ghafla cha Padri Mushi na kuelezea haja ya kuwepo kwa uvumilivu katika kipindi hichi cha msiba.
 
Habari hii imeandikwa na Mwantanga Ame, Haroub Hussein na Rajab Mkasaba, Ikulu

2 comments:

  1. Naomba kama kuna mwenye taarifa atueleze ivi imekuwaje wale waliompiga risasi yule liongozi wa kanisa siku za nyuma na wale waliomwagia tindikali Ust Soraga? Nakumbuka kulitumwa kikosi maalum kuchunguza matukio yale.Au ilikuwa danganya toto?

    ReplyDelete
  2. Katika kesi ya padri aliyepigwa risasi mpendae, kuna watu tuliambiwa wamekamatwa na wanahojiwa. Hofu yetu ni kuwa hatujui kama bado wapo ndani au la. Ni bora serikali na vyombo vya sheria vikawa wazi katika maswala haya. kesi ziwe open na kila hatua ijulikane. serikali na vyombo vyake hatuviamini vizuri wanaweza wakadhalilisha watu kwa visingizio vya uongo.

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.