Habari za Punde

Uamsho wasomewa mashtaka mapya

Na Mwandishi wetu
 
MAHAKAMA Kuu ya Zanzibar, imewasomea upya mashtaka katika kesi ya jinai namba 9 ya mwaka 2012, viongozi wa Jumuiya ya Mihadhara ya Kislamu (Uamsho).
Akiwasomea mashtaka yao, Mwendesaha Mashtaka wa Serikali, Ramadhan Nasibu, aliwataja washtakiwa kuwa ni Farid Hadi Ahmed (41) mkaazi wa Mbuyuni, Mselem Ali Mselem (52) mkaazi wa Kwamtipura, Mussa Juma Mussa (47) mkaazi wa Makadara na Azan Khalid (48) mkaazi wa Mfenesini.
Wengine ni Suleiman Juma Suleiman (66) mkazi wa Makadara; Khamis Ali Suleiman (59) (Mwanakwerekwe); Hassan Bakar Suleiman (39) (Tomondo); Ghalib Ahmada Juma (39) (Mwanakwerekwe); na Abdallah Saidi (48) (Misufini).

Mashtaka waliyosomewa ni kuharibu mali, uchochezi, ushawishi na kuhamasisha fujo na kula njama ya kufanya kosa.
Kosa la nne linamkabili mshtakiwa namba nne pekee, Azan Khalid, ambaye anadaiwa kutoa maneno ya matusi kwa Kamishna wa Polisi, kitendo kinachoweza kusababisha uvunjifu wa amani.
Vitendo hivyo vinadaiwa kufanyika kati ya Oktoba 17 hadi 19 katika maeneo tofauti katika manispaa ya mji wa Zanzibar ambapo washtakiwa wote walikana makosa yote.
Mara baada ya kuwasomea mashtaka yao, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, alidai kuwa upelelezi wa shauri hilo tayari umekamilika.
Hata hivyo aliiomba mahakama hiyo kusubiri kwa kuwa upande wa mashtaka umekata rufaa katika Mahkama ya Rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu ya Zanzibzar.
Alidai kuwa iwapo mahakama itaendelea na kesi hiyo inaweza kuifanya Mahakama ya Rufaa kutoa uamuzi ambao unaweza kuathiri uamuzi wa mahakama hiyo.
Mapema upande wa utetezi ukiongozwa na Salum Taufiq, uliiomba mahakama hiyo kuwapatia dhamana wateja wao hasa ikiangaliwa kuwa tayari wameshakaa ndani kwa muda mrefu sasa.
Jaji Fatma Hamid Mahmoud anayesikiliza kesi hiyo alisema kuwa atayachukuwa maombi ya pande zote mbili na kuyapitia kwa umakini ili baadaye aweze kutoa uamuzi ulio sahihi.
Kesi hiyo iliahirishwa na watuhumiwa kurudi rumande hadi Machi 27 ambapo uamuzi wa washtakiwa kupatiwa dhamana au la utatolewa.

Chanzo - Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.