Habari za Punde

Jimbo la Nanjing kujenga kituo cha uchunguzi ya magonjwa ya njia ya chakula, hospitali kuu ya Mnazimmoja


Na Said Ameir, Nanjing China
Serikali ya Jimbo la Jiangsu nchini China itajenga katika hospitali ya Mnazi Mmoja mjini Unguja kituo cha uchunguzi wa magonjwa ya njia ya chakula na kitengo cha huduma kwa wagonjwa wanaopata ajali katika hospitali ya Abdalla Mzee huko Pemba.

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Idara ya Afya ya Serikali ya jimbo hilo Bwana Shi Zhiyu alieleza kuwa ujenzi wa vituo hivyo unatarajiwa kukamilika mwezi Oktaba mwaka huu.

Bwana Shi ameeleza hayo wakati alipokuwa akimkaribisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alipotembelea Hospitali ya Drum Tower mjini Nanjing makamo makuu ya jimbo hilo.

Akiwa katika hospitali hiyo Dk. Shein alitembelea vitengo mbalimbali na sehemu za kutolea huduma kwa wagonjwa na pia alizungumza na madaktari wa kichina waliowahi kufanya kazi Zanzibar.


“Tumefurahishwa na ujio wako hapa. Tunajua upo hapa kuimarisha uhusiano wa China na Zanzibar. Umetimiza nia yako ya kututembelea na hiyo inaonyesha jinsi unavyotuthamini ”alieleza Li.

Alibainisha kuwa hospitali hiyo imekuwa ikitoa wataalamu wengi wanaokwenda kufanya kazi Zanzibar na timu inayokwenda sasa ni ya 25.

“Kwa hakika ushirikiano wa nchi yetu na nchi zinazoendelea katika sekta ya afya ulibuniwa tangu Uhuru hali ya kuwa sisi wenyewe tulikuwa na hatujapiga hatua kubwa lakini tumeweza kutekeleza kwa kuwa ilikuwa ni dhamira yetu” Li alisema.

Aliongeza kuwa maadhimisho ya miaka 50 ya ushirikiano huo yatakayofanyika  mwaka ujao usiwe tu ni wa kuonyesha historia ya mafanikio yaliyopatikana bali kujenga mustakabala nzuri wa ushirikiano wetu kwa miaka mingi ijayo.

“maadhimisho ya miaka 50 ya Jiangsu kupeleka wataalamu wa afya Zanzibar tunayachukulia kama changamoto na fursa kwetu kupanua ushirikiano huo” Li alisisitiza.

Ujenzi wa vituo hivyo utaimarisha utoaji huduma za uchunguzi na tiba kwa wagonjwa wenye matatizo ya njia ya chakula na kutaimarisha huduma kwa watu wanaoumia katika ajali.

Bwana Li aliongeza kuwa baada ya kukamilika upanuzi wa hospitali ya Abdalla Mzee huko Pemba serikali ya jimbo hilo litapeleka wataalamu zaidi kusaidia kutoa huduma katika hospitali hiyo.

Akizungumza baada ya mkutano huo Dk. Ding Yibo ambaye alifanyakazi katika hospitali ya Abdalla Mzee huko Pemba kati ya mwaka 1997 hadi 1999 alisema kuwa mara kwa mara wanapokutana na watumishi wenzake wa kichina waliokuwa nao Pemba kuzungumzia jinsi walivyoishi na kufanya kazi huko.

“Ni kipindi chenye kumbukumbu nyingi katika utumishi wetu kila tunapokutana na wenzagu tuliofanya kazi pamoja Pemba huzungumzia maisha yetu yalivyokuwa na kuwakumbuka marafiki zetu huko”alieleza Dk. Ding.

Anasema sio siri kuwa kila mmoja wao ana hamu kupata fursa ya kurudi tena kwa sababu walipokelewa na kuishi vizuri na wenyeji wao na kuwa nao walirejesha upendo kwao kwa kufanyakazi kwa bidii.

Wakati huo huo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amekutana na Gavana wa Jimbo la Jiangsu Bwana Li Xueyong   na kuzungumzia kuimarisha ushusiano kati  ya Zanzibar na Jimbo la Jiangsu.

Katika mazungumzo hayo Bwana Li alisema mbali ya ushirikiano katika sekta ya afya sasa ni muda muafaka wa kuangalia maeneo mapya ya ushirikiano kati ya Jimbo hilo na Zanzibar ikiwemo sekta ya utalii.

Alipendekeza safari za kitalii zinazofanywa na wananchi wa jimbo hilo nchini Tanzania zijumuishe pia matembezi katika visiwa vya Unguja na Pemba.

Kwa upande wake Dk. Shein pamoja na kukubalina na pendekezo hilo amesema eneo jingine la ushirikiano ni kwa makampuni ya kati ya jimbo hilo kuwekeza Zanzibar katika sekta mbalimbali ikiwemo ya tekinolojia ya mawasiliano ya habari ikiwa ni njia ya kuingia katika masoko ya Afrika.

Jimbo la Jiangsu lina makampuni mengi yakiwemo makubwa ya eletroniki na tekinolojia ya habari na mawasiliano.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.