Habari za Punde

Baba Amjeruhi Mtoto Wake kwa Kipigo.

Madina Issa na Khamisuu Abdallah
MTOTO wa kiume  anaekisiwa kuwa na umri wa miaka sita mkaazi wa Bambi, amepigwa na baba yake kwa kitu kizito na kumsababishia maumivu makali.

Akizungumza na waandishi wa habari hizi, Daktari wa kitengo cha mkono kwa mkono cha hospitali kuu ya Mnazimmoja, Salum Omar Mbarouk, alithibitisha kumpokea mtoto huyo na kusema dalili zinaonesha alivunjika.

Alisema baada ya kumpokea alimpima na kugundua kuwa mtoto huyo alipigwa na kitu kizito kilichomsababishia kuvunjika.

Aidha alisema mtoto huyo baada ya kupelekwa katika mashine ya kuchunguza mifupa (x-ray) ilionesha mtoto alivunjika na tayari ameshaanza kupatiwa matibabu.

Hivyo alitoa wito kwa wazazi na walezi kuwa makini na watoto wao kwani hao ndio tegemeo la baadae.

Aliitaka jamii inapowaokota watoto kama hao wanaofanyiwa udhalilishaji kuripoti kituo cha polisi ili sheria iweze kuchukua hatua zaidi.


“Baba yake ana tabia ya kumuacha mtoto wake nyumbani ambapo huondoka na mtoto wake wa kike sasa huyu huondoka na kwenda kiambo cha juu kwa ajili ya kucheza lakini akirudi huchezea kipigo,” alisema Mratibu wa wanawake na watoto, Mashavu Ramadhan Abdallah,.

Alisema mtoto huyo alimuona kwa bibi ambae alimuhifadhi baada ya kumuona anapigwa.

Sambamba na hayo Mratibu huyo alisema baba huyo ni mzoefu wa matukio ya udhalilishaji kwani alimtahiri mtoto Gumba kwa kutumia kisu huku dawa ikiwa pombe ya kienyeji.

“Baba yake huyu mtoto anaonesha kuwa ni katili sana kwani alimtahiri kwa kisu na pombe ya kienyeji kufanywa ndio dawa,” alisema.

Alisema  kwa sasa baba mzazi wa mtoto huyo yupo chini ya ulinzi katika kituo cha polisi Dunga huku mama yake hajulikani alipo.

Nae mtoto  Gumba  alisema baba yake huwa anampiga  mara kwa mara  baada ya kutoka kiamboni kucheza na wenzake.

1 comment:

  1. Binafsi namuonea huruma huyo mtoto inanikumbusha mie mwenye nikiwa Mdogo Baba yangu alikuwa hajuwi kuelimisha yeyey ukifanya kosa ujuwe ni fimbo alikuwa akinipiga mfano wa pweza wakati huo mie bado ni mtoto akili yangu inahitaji Baba kunielimisha na kunieleza ubaya na uzuri wa mambo lakini yeye hakuwa hivyo Baba yangu alikuwa ni mtu wa sala Tano ,nakumbuka ipo siku nikiwa nacheza na wezangu kifungo cha chati kikakatika na kwa kuwa siku hizo unambiwa usiende tumbo wazi mie nikatafuta nijiwe kidogo nikatia ili kuweka kiwe kama kifungo kufika nyumbani hakukuwa na msalie mtumi kiao kule ,nilifika mahali nikawa nipo tayari nimwagie petrol nimuwashe moto lakini sikuwa na uwezo wakuipata hadi hii leo mapenzi yangu kwake ni ile tu Mmungu anatutaka tuwaenzi wazazi na kila nikikumbuka inakuwa najihisi kama jana na kama ingekuwa kipigo chake ni elimu basi sasa ningekuwa namimi na kwenda mwezini

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.