HOTUBA YA MWENYEKITI WA KAMATI YA KATIBA,
SHERIA NA UTAWALA YA BARAZA LA WAWAKILISHI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA WIZARA YA NCHI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA IDARA MAALUM ZA SMZ
2014/2015
UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu kwa
kunijaalia afya njema na uzima wa kuweza kusimama mbele ya Baraza lako tukufu
katika kutekeleza majukumu ya kulijenga
taifa letu. Aidha napenda kwa moyo wa dhati nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa
nafasi hii muhimu ya kutoa maoni ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala kuhusu
makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za
Mikoa na Idara Maalum za SMZ kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
Mheshimiwa Spika, Napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa
Waziri wa Wizara hii, Mheshimiwa Haji Omar Kheir mwakilishi wa wananchi wa
Jimbo la Tumbatu pamoja na watendaji wake wote kwa juhudi zake anazozichukua na
hatimae katika muda mfupi tu tokea ateuliwe
matunda ya juhudi zake yameanza kuonekana.
Mheshimiwa Spika, Kamati katika kipindi cha
utekelezaji wa majukumu yake ilifanya kazi nzuri ya kuzipitia bajeti za Wizara
husika na kutoa maelekezo yenye lengo la kuleta ufanisi wa majukumu ya kila
siku ambapo Wajumbe wote walitoa ushirikiano wa hali ya juu katika kutekeleza
wajibu wao wa kuikosoa Serikali pale panapohitajika.
Mheshimiwa Spika, naomba
nichukue nafasi hii kuwashukuru Wajumbe wote wa Kamati kwa umakini wao wakati wa Kazi za Kamati. Shukurani hizo pekee
hazitatosha iwapo sitowataja wajumbe wa Kamati hii kwa majina yao, Pai naomba
kuchukua nafasi hii kumkaribisha rasmi Mjumbe mpya wa Baraza la Wawakilishi wa
Jimbo la Kiembesamaki ambae ameletwa katika Kamati hii.
Mheshimiwa Spika, Wajumbe
wa Kamati hii naomba kuwataja kama ifuatavyo:
- Mhe. Ussi Jecha
SImai Mwenyekiti
- Mhe. Abdalla Juma
Abdalla Makamo Mwenyekiti
- Bikame Yussuf
Hamad Mjumbe
- Mhe. Mahmoud Thabit
Kombo Mjumbe
- Nassor Salum Ali
Mjumbe
- Mhe. Suleiman Hemed
Khamis Mjumbe
- Mhe. Wanu Hafidh
Ameir Mjumbe
- Ndg. Aziza Wazir
Kheir
Katibu
- Ndg. Khamis Hamad
Haji Katibu
Mheshimiwa Spika, Wizara
ya Nchi (OR) Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ ni miongoni mwa Wizara za
Serikali ambazo zina majukumu mazito ya kutoa huduma kwa wananchi ambao wana
mahitaji mengi ya msingi yanayohitaji kutekelezwa kwa ufanisi wa hali ya juu.
Mheshimiwa Spika, Wananchi
waliowengi kipato chao ni duni na hivyo mahitaji yaio mengi ya msingi
wanategemea kuyapata kupitia huduma zinazotolewa na baadhi ya taasisi za
Serikali ambazo zinahusika na utoaji wa huduma hizo ambapo watumishi9 wa
Serikali wanapaswa kutumia utaalamu na ujuzi wao wote kwa lengo la kuisaidia
Serikali kufikisha huduma hizo kwa wananchi.
IDARA YA MIPANGO, SERA NA UTAFITI
Mheshimiwa Spika, Pamoja
na majukumu mengine ya msingi, kazi kubwa ya Idara hii katika mwaka huu wa fedha
ni kuandaa na kuhakikisha kuwa mpango wa kupunguza umaskini unatekelezeka.
Aidha Idara ina wajibu wa kusimamia utekelezaji wa sera na sheria mbali mbali
zilizo chini ya Wizara hii kwa lengo la kuhakikisha kuwa wananchi wananufaika
na huduma zinazotolewa na Serikali.
Mheshimiwa Spika, Mpango
wa kuendeleza miradi mikubwa na midogo midogo ya maendelea katika ngazi za
Serikali za mitaa ni mizuri, hata hivyo Kamati inaishauri Wizara kutekeleza
mipango hiyo kwa kasi zaidi na kwa wale wananchi ambao wanakiuka amri halali za
Serikali katika utekelezaji huo wachukuliwe hatua za kisheria.
Mheshimiwa Spika, Malengo
makubwa kwa mwaka ujao wa fedha ni kuanzisha na kuzindua kamati ya uratibu wa
shughuli za mipango katika ofisi. Kamati inakubaliana na wazo hilo la kuanzisha
kamati amabyo itakuwa na wajibu wa kuhakikisha kuwa shughuli zote za Wizara
zinatekelezwa kama zilivyopangwa jambo amablo litasaidia kuondoa baadhi ya kero
zinazowakabili wananchi hivi sasa. Aidha Kamati inazidi kusisitiza kuwa Idara
ina wajibu wa kuhakikisha kuwa inafuatilia utekelezaji wa kila robo mwaka wa
Bajeti kwa upande wa Pemba ili malengo yaliyopangwa kwa kila mwaka yaweze
kutekelezeka.
IDARA YA UENDESHAJI NA UTUMISHI
Mheshimiwa Spika, Idara
hii ina jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa Wizara inaimarisha mipango yake ya
upatikanaji wa rasilmali watu ambao watakua na ujuzi wa kutosha ambao
wataisaidia Wizara kutekeleza mipango yake iliyojipangia kwa ufanisi mkubwa.
Aidha Idara inawajibu wa kuhakikisha inatoa mafunzo ya muda mfupi
yanayowajengea uwezo katika utekelezaji wa majukumu yao. Aidha, Kamati
inaishauri Idara kuweka mazingira mazuri ya kiutawala ambayo yatasaidia kuwa na
maelewano baina ya wafanyakazi.
IDARA YA URATIBU TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA
Mheshimiwa Spika, Suala
kubwa ambalo kamati inataka kusisitiza hapa ni ushirikiano baina ya viongozi wa
Mikoa na Wilaya ambao ni kiungo kikubwa katika maeneo yetu. Aidha Kamati
imekubaliana na mpango wa Wizara uliowekwa kwa mwaka ujao wa fedha wa kuandaa
vikao baina ya viongozi hao. Vikao hivyo vitasaidia kujua changamoto zilizopo
baina ya viongozi hao ambao ni chachu ya maendeleo katika Serikali zetu za
Mitaa.
Mheshimiwa Spika,
kumekua na changamoto kubwa hivi sasa ya kuibuka kwa bandari bubu katika baadhi
ya maeneo mbali mbali ya Mikoa yetu. Hivi sasa kumekuwa na tabia ya baadhi ya
wananchi kuzitumia bandari hizo kwa kuwasafirisha wananchi kutoak sehemu moja
kwenda nyuengine kwa kutumia majahazi na maboti ambayo hayajasajiliwa kuoakia
abiria kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, jambo hili limekuwa ni chanzo cha
kusafirishia silaha na magendo mbali mbali wakiwemo wanyama kutoka bara kuja
hapa Zanzibar. Hali hiyo pia inahatarisha usalama wa afya za wananchi wetu
kutokana na hao wanyama wanaosafirishwa kutofanyiwa uchunguzi wa kina hatimae
kuingiza maradhi mbali mbali hapa nchini. Hivyo Kamati inaitaka Serikali
kupitia Wizara kuzifunga shughuli zote zisizoruhusiwa katika bandari hizo,
Kamati inaona kufanya hivyo kutaepusha mambo mengi ya kihalifu ambayo yamekuwa
yakijitokeza hivi sasa hapa nchini likiwemo tukio la hivi karibuni la kukamatwa
kwa silaha iliyoingizwa katika bandari ya Mkokotoni Wilaya ya Kaskazini A.
Mheshimiwa Spika, Baadhi
ya vipaumbele na mipango ya utekelezaji tunayoipanga na kuamua katika chombo
hiki haitekelezeki siyo kwa sababu ya ufinyu wa bajeti peke yake, bali mengine
inakwamishwa kutokana na aidha utendaji kazi uliochini ya kiwango na kutojali kwa
baadhi ya watumishi wa umma katika utekelezaji wa majukumu yao ya msingi na
ukaidi wa baadhi ya wananchi ambao mara nyingi wanapopewa amri na Serikali
hukataa kuitii amri hizo.
Mheshimwa Spika, Uporomokaji
huu wa maadili kwa baadhi ya watumishi wa Serikali umechangiwa sana na mifumo
yetu mibovu ya uajiri huko nyuma na baadhi ya wananchi kutegemea viongozi
wanaowajua ambao mara nyingi huwatetea Serikalini. Kamati inashauri Wizara
kupitia bajeti ya mwaka huu kufanya kampeni maalumu na kuchukua hatua za lazima
inapobidi kwa mujibu wa sheria, kuwashughulikia watumishi wa umma wasiozingatia
maadili ya utumishi na wananchi wote wanaokataa kutii mari ya Serikali.
Mheshimiwa Spika,
Sera na Kanuni za Serikali za mitaa ndio miongozo inayotumika katika
utekelezaji wa mipango yote inayopangwa katika Taasisi hizo, hivyo ni wajibu wa
Idara kuhakikisha kua inatoa mafunzo maalum kwa wananchi na taasisi
zinazohusika kuhusiana na sera na kanuni hizo, kwa lengo la kuhakikisha kuwa
mipango inayopangwa kwa wananchi inatekeleza bila kikwazo cha aina yoyote.
Aidha Kamati inachukua nafasi hii kuipongeza Wizara kwa taarifa iliyoipatia
Kamati kuwa wanategemea kuleta Mswada wa dharura wa marekebishio ya Sheria za
Serikali za mitaa ambazo ni Mswada wa
Sheria ya Tawala za Mikoa, Mswada wa Sheria ya Serikali za Mitaa na Mswada wa
kuanzisha Shirika la Ulinzi la JKU. Kabla ya hapo kumekua na kilio cha muda
mrefu ambacho Kamati kila Wilaya na Mkoa inaoupita inapewa malalamiko ya kuwepo
kwa mgongano wa tafsiri za Kisheria ambazo zimekuwa ni kikwazo cha utekelezaji
wa baadhi ya mipango ya Mikoa na Wilaya. Hivyo kuletwa kwa Miswada hiyo ya
kisheria Kamati inaamini kuwa itaondosha migongano ya kisheria iliyokuwepo
TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA
Mheshimiwa Spika, Kamati
yetu kabla ya kupitia bajeti ya Wizara na kuipitisha ilipata nafasi ya kufanya
kazi zake za kawaida na ilipata nafasi ya kukagua baadhi ya Wilaya na Mikoa ya
kisiwa cha Unguja ukiwemo Mkoa na Wilaya ya Kusini Unguja, Hlmashauri ya Wilaya
ya Kaskazinia “A”, Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini “B” , na Halmashauri ya
Wilaya ya Kati . Katika ziara hizo Kamati ilipata nafasi ya kupokea taarifa ya
utekelezaji wa Bajeti na kuelezwa mambo mbali mbali zikiwemo changamoto ambazo
nyingi kati ya hizo changamoto zinasababishwa na ufinyu wa bajeti. Kamati
ilielezwa kuwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja inakabiliwa na changamoto
ya ukosefu wa usafiri wa uhakika kwa wafanyakazi, hali hiyo inasababishwa na
bajeti finyu inayopelekwa ambayo haikidhi haja na hatimae wanashindwa kununua
hata gari ya Ofisi.
Mheshimiwa Spika,
Kamati pia ilipata changamoto ya malipo madogo ya wazee wanayolipwa kupitia
Mikoa yao kila mwisho wa mwezi, Kamati ilielezwa kuwa posho la wazee hao ni
shilingi elfu tano kwa mwezi wanayopatiwa ambayo Kamati inahisi kuwa kimo hicho
ni kidogo na inaishauri Serikali ifanye utaratibu wa kuwaongezea wazee hao
wanaoishi katika mazingira magumu angalau fehda hizo ziwe shilingi elfu hamsini
kwa mwezi.
Mheshimiwa Spika, Kamati
pia ilipata taarifa katika kila Mkoa na Wilaya iliyokua inakaguliwa kuwa Sheria
nyingi zilizopo hivi sasa za Serikali za Mitaa zimepitwa na wakati, aidha
sheria hizo hizo pia zinagongana na sheria za taasisi nyengine jambo ambalo
limekua linazikosesha mapato Halmashauri zetu. Hivyo Kamati inapenda kuchukua
nafasi hii kuipongeza Wizara kwa uamuzi wake huo wa busara ambao utasaidia kuondoa
changamoto zilizopo kama tulivyoeleza mwanzo katika hotuba hii.
Mheshimiwa Spika,
Kamati inazipongeza Wilaya na Mikoa yote katika jitihada zao za kuhakikisha
kuwa suala la ulinzi na usalama linaimarika kwa pia inazidi kusisitiza kuwa
ulizni shirikishi ni suala la msingi ni vyema likazidi kuekewa mkazo kwa
kuwashirikisha wananchi kila panapohitajika.
Mheshimiwa Spika, katika
ziara za Kamati ilipotembelea Baraza la Manispa ilipatiwa changamoto mbali
mbali zinazolikabili Baraza hilo ikiwemo changamoto ya uchache wa wafanyakazi
jambo ambalo linapunguza kasi ya utendaji kazi hasa kazi ya uzoaji wa taka
taka. Aidha Katika suala zima la kuweka mazingira ya maeneo yetu katika hali ya
usafi, Kamati ilisikitishwa sana na taarifa kuwa kuna baadhi ya wananchi wamekua
na tabia ya kukaidi amri ya kuzihifadhi taka taka katika maeneo ya kuwekea taka
hizo. Hali hiyo imekua ikizorotesha juhudi zinazofanywa na Baraza hilo na
kusababisha kuzagaa ovyo kwa taka hizo. Kutokana na hali hiyo Kamati inaishauri
Wizara na Serikali kwa ujumla kuweka utaratibu maalum wa kuizuia hali hiyo na
ikiwezekana mtu yeyote atakayevunja amri ya kuzihifadhi taka zake atozwe faini
au adhabu yoyote itakayofaa ichukuliwe dhidi yake. Kamati inaipongeza Serikali
kwa uwamuzi wake wa kuwaingiza wafanyakazi wa Baraza la Manispaa katika “Vote”
ya mishahara ya Serikali jambo amablo litasaidia fedha wanazozikusanya
kutoakana na vyanzo mbali mbali vya mapato kununulia vitendea kazi. Aidha Kamati inapenda kuchuku nafasi hii
kuipongeza Serikali kwa mpango wake wa kutaka kuliendeleza eneo la Darajani kwa
kujenga maduka ya kisasa ambayo yatakuwa ni chachu ya maendeleo katika nchi
yetu.
AFISI YA USAJILI NA KADI ZA UTAMBULISHO
Mheshimiwa Spika, Bado
kuna umuhimu mkubwa wa Idara kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusiana na
umuhimu wa Vitambulisho ambapo baadhi ya wananchi hadi hii leo hawana
vitambulisho hivyo. Hali hii inatokana na uelewa mdogo wa baadhi ya wananchi
ambao baadhi yao vitambulisho vyao hadi hii leo kwa taarifa za awali hawajaenda
kuvichukua. Aidha Kamati inapenda kuchukua nafasi hii kuwahamasisha wananchi
wale ambao hawana vitambulisho kufuata taratibu na kwenda kuchukua vitambulisho
ambavyo ni utambulisho wa Taifa. Aidha katika kikao cha kupitisha Bajeti Kamati
ilipewa taarifa kuwa Idara haikukadiriwa mapato yake kutokana na mjadala
uliokuwepo hivi sasa juu ya suala la ada ya vitambulisho vya wageni ambapo
suala hilo hivi sasa kutokana na Kanuni zake kutokamilika hivyo suala hilo
litakaa sawa hapo mjadala wa Kanuni hizo utakapokamilika. Vile vile Idara
inakusanya ada ya wanaopoteza vitambulisho ambapo Kamati ilipotaka maelezo juu
ya suala hilo ilipewa taarifa hiyo na Kamati iliridhika.
IDARA MAALUM ZA SMZ
Mheshimiwa Spika, Kamati
yangu inapenda kuchukua nafasi hii kuzipongeza Idara Maalum zote za SMZ kwa
juhudi wanazozichukua katika kutimiza wajibu wao pamoja na changamoto nyingi
wanazokabiliana nazo. Aidha Kamati wakati inafanya ziara zake katika baadhi ya
Idara hizo ilijionea changamoto ya ukosefu wa makaazi ya kudumu ya watumishi
hao ambapo baadhi ya nyumba wanazoishi hazifai kwa makaazi ya binaadamu,
kutokana na hali hiyo Kamati inaishauri Wizara kuliangalia suala hilo kwa
umakini mkubwa kwa kuhakikisha kuwa makaazi ya watumishi hao yanajengwa ili
waweze kutimiza wajibu wao kwa umakini zaidi.
Mheshimiwa Spika,
Suala la ubunifu kwa Idara Maalum ni suala la kupigiwa mfano kutokana na miradi
mingi ya maendeleo inayobuniwa na Idara hizo ambapo mingi ya miradi hiyo endapo
itatengewa bajeti za kutosha itaimarika na kuziimarisha Idara hizo kutokana na
fedha zitakazopatikana katika miradi hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati ilipokua katika ziara zake za kikazi katika Kikosi cha Valantia,
ilikagua kiwanda cha kutengenezea viatu ambacho kinatengeneza viatu hivyo kwa
uimara wa hali ya juu pamoja na hali ngumu iliyopo kiwandani hapo. Hivyo Kamati
inaiomba Wizara ifanye mpango wa kukiendeleza kiwanda hicho kwa kuhakikisha
kuwa anaajiriwa mtaalamu mwenye uwezo wa hali ya juu kutokana na mtaalamu anayetumika
hivi sasa kutoajariwa na Idara hiyo na anafanya kazi ya kuwafundisha vijana
waliopo pale kwa makubaliano maalum, aidha Kamati inaishauri Wizara kuwatafuta
wafadhili hata nje ya nchi kwa ajilia ya kuwaendeleza vijana waliopo katika
kiwanda hicho ili wakajifunze mbinu nyengine nzuri zaidi ambazo zitawezesha
kukiendeleza kiwanda hicho.
Mheshimiwa Spika, Kamati
ilipata nafasi ya kukagua mradi wa ujenzi wa skuli ya ufundi ya JKU iliyopo
Mtoni ambayo ujenzi wake umefikia hatua nzuri hadi hivi sasa. Kukamilika kwa
mradi huo kutaisaidia jamii yetu kupunguza tatizo kubwa liliopo hivi sasa la
ukosefu wa ajira kwa vijana wetu ambao wengi wao hawana ajira za kudumu, hata
hivyo katika bajeti ya mwaka huu fedha za maendeleo katika Idara hii
zilizotengwa ni kwa ajili ya kilimo cha mboga mboga, pamoja na umuhimu wake
kilimo hicho suala la ujenzi wa skuli hiyo pia ni muhimu zaidi, hivyo Kamati
inatoa ushauri kuwa Serikali ifanye juhudi zake zote kuhakikisha kuwa skuli
hiyo inakamilishwa hasa tukizingatia kuwa ujenzi wa mnara wa miaka 50 ya
Mapinduzi ya Zanzibar fedha zake zilipatikana japokuwa hazikuainishwa katika
bajeti iliyopita.
Mheshimiwa Spika,
Chuo cha Mafunzo ni miongoni mwa Idara zinazokumbwa na changamoto kubwa ya
kutoa huduma kwa wananchi hasa wale wanowekwa katika magereza yetu, hivyo
Kamati inaishauri Serikali inapopanga bajeti za kila Wizara ihakikishe kuwa inatoa
kipaumbele kwa Idara hii kutokana na huduma za msingi zinazohitajika katika
Idara hii ikiwemo ya malazi, makaazi na chakula. Kamati inazidi kusisitiza kuwa
ujenzi wa gereza jipya la Hanyegwa Mchana ni wa lazima na Serikali haina budi
kuhakikisha kuwa inatafuta wafadhili watakaoweza kutusaidia kukamilisha ujenzi
wake.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inapenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Idara ya Chuo cha Mafunzo
kwa juhudi zake za kuanzisha mradi wa ujenzi wa maduka ambayo kukamilika kwake
na mapato yake yataisaidia Idara hiyo kukwamua baadhi ya changamoto zilizopo.
Mheshimiwa Spika, Wito
wa Kamati yangu kwa Serikali katika mwaka huu wa fedha ni kuitaka ihakikishe
inatekeleza malengo waliyojipangia, ikiwa ni pamoja na kukamilisha mapitio ya
huduma za sheria ya Idara Maalum, Sheria Namba 6 ya 2007 na Kanuni zake. Aidha
Kamati inasisitiza kuwa Idara Maalum zote ikiwemo Idara ya Zimamoto na Uokozi,
Kikosi cha Kuzuia Magendo, ni muhimu sana katika ustawi wa taifa letu hivyo Serikali
ina wajibu wa kuwawekea mazingira mazuri ya kazi ili vijana wetu waweze kufanya
kazi kwa ufanisi zaidi.
Mheshimiwa Spika, Kamati
yangu inaendelea kusisitiza suala la kuwalipa mishahara mizuri watendaji wa
Idara Maalum zote kutokana na kazi nzito wanazozifanya na zinazolingana na
wenzao wa Taasisi za Muungano ambao wanalipwa vizuri zaidi ukilinganisha na
wao. Aidha Kamati haijaridhishwa na hali hii ya watumishi wa Idara Maalum kulipwa
kiwango kidogo cha mishahara na inapendekeza hatua za haraka zichukuliwe na
Serikali kukaa tena na Uongozi wa Wizara kujadiliana tena viwango vipya vya
Mishahara inayolingana na wenzao wa Tanzania bara.
TUME YA UTUMISHI YA IDARA MAALUM
Mheshimiwa Spika, Tume
hii ina jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa Idara Maalum za SMZ zinafanya zoezi la
uajiri pamoja na kuweka mazingira bora yatakayoimarisha mazingira ya Utumishi kwa
watendaji wa Idara hizo.
Kamati yangu inazidi kuisisitiza Tume
kusimamia zoezi zima la uajiri kwa haki ili kuepusha malalamiko yanayotolewa na
baadhi ya wananchi kipindi cha uajiri kinapofika. Kumekuwa na taarifa
zisizoridhisha kinapofika kipindi cha uajiri ambapo kumekua na baadhi ya
maafisa wasiokuwa waaminifu kuwalaghai wananchi kuwa watawapatia ajira kwa
urahisi na kinachotakiwa ni wananchi hao kutoa fedha kwa ajili ya kuwafanyia
mipango hiyo, malalamiko hayo yamekuwa ni mengi sana, hivyo Kamati inatoa agizo
kwa Afisa yeyote atakayepatikana na kadhia ya kufanya kitendo hicho achukuliwe
hatua kali za kisheria ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hizo
ambazo zimekuwa ni kikwazo na zinachafua jina la taasisi zetu.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Wizara kupitia Tume ya Utumishi
ya Idara Maalum za SMZ kwa uamuzi wake wa kuwafundisha wapiganaji pamoja na
maofisa wake Sheria mbali mbali za nchi ikiwemo Sheria ya Utumishi wa Umma
pamoja na masuala ya Utawala na Uongozi ili kuhakikisha kuwa wanatekeleza
majukumu yao kwa ufanisi mkubwa.
HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, Mwisho
naomba nichukue fursa hii kukushukuru wewe pamoja na Wajumbe wako wote wa
Baraza hili tukufu kwa kunisikiliza kwa utulivu na umakini mkubwa.
Mheshimiwa Spika, Nawaomba
wajumbe wako waichangie bajeti hii, watoe mapendekezo yao panapohitajika na
hatimaye kuipitisha baada ya kuafikiana kwa hoja mbali mbali watakazoibua
wakati wa mjadala.
Mheshimiwa Spika, naomba
kuwasilisha.
………………………………………..
Ussi
Jesha Simai,
Mwenyekiti,
Kamati
ya Katiba, Sheria na Utawala,
Baraza
la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment