MAKADIRIO
YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA
2014/2015
-
Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii,
Vijana, Wanawake na Watoto
UTANGULIZI:
1.
Mheshimiwa Spika, Naomba
kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu likae kama Kamati ya matumizi ili liweze kupokea,
kujadili na kuidhinisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya
Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto kwa mwaka wa fedha
2014/2015.
2.
Mheshimiwa Spika, Naomba
kuchukua fursa hii adhimu kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu na Mwingi wa Rehema
kwa kutujaalia kwa mara nyengine kukutana hapa leo, tukiwa wazima wa afya. Aidha, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia mimi mwenyewe afya njema
na uzima, nikaweza kusimama hapa leo kuwasilisha mbele ya Baraza lako Tukufu,
Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu kwa mwaka wa fedha
2014/2015.
3.
Mheshimiwa Spika, Kwa niaba yangu
na Wafanyakazi wa Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jami, Vijana, Wanawake na
Watoto, nachukua fursa hii adhimu kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kutuongoza vyema katika safari yetu ya kuleta
maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi yetu. Uongozi wake mahiri, thabiti
na makini umeendelea kuwa dira katika utendaji wa kazi zetu. Tunaomba Mwenyezi
Mungu azidi kumjaalia afya njema, maarifa na hekima katika kuiongoza nchi yetu,
ili tuweze kufikia matarajio na malengo tuliyojiwekea katika kufikia maendeleo
ya kiuchumi na kijamii.
4.
Mheshimiwa Spika, Pia napenda nichukue nafasi hii kuwapongeza
Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharrif Hamad na Makamu wa Pili wa Rais,
Balozi Seif Ali Iddi kwa kumshauri na kumsaidia kwa
karibu Mheshimiwa Rais wa Zanzibar katika utekelezaji wa majukumu yake.
Aidha, nachukua fursa hii kukushukuru wewe
binafsi Mheshimiwa Spika kwa kuendelea
kuliongoza Baraza hili Tukufu kwa hekima, busara na uadilifu. Umahiri wako
katika kuliendesha Baraza hili, umewezesha kuwepo kwa mijadala makini, ambayo
imesaidia sana kuimarisha utekelezaji wa majukumu yetu ndani ya Serikali.
5.
Mheshimiwa Spika, Napenda
kuchukuwa fursa hii kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wote
kwa kuadhimisha miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar. Sherehe za
maadhimisho haya zilitupa fursa ya kutathmini mafanikio tuliyoyapata kupitia
sekta mbali mbali katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi
yetu. Aidha, zilitupa fursa ya kutafakari changamoto tunazopaswa kuzifanyia
kazi, ili kuleta maendeleo endelevu kwa ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.
Napenda sana kumpongeza Mhe. Makamu wa Pili wa Rais na Wafanyakazi wake wote
kwa kuratibu Sherehe hizi kwa ufanisi mkubwa, na hivyo kuweza kudhihirisha
maendeleo ya kupigiwa mfano yaliyopatikana katika miaka hii 50 ya Mapinduzi.
6.
Mheshimiwa Spika, Napenda
pia kuzipongeza Serikali zote mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuandaa na kufanikisha
sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Aidha, sote
tunapaswa kujipongeza kwa kuweza kuudumisha Muungano huu hadi kufikia miaka 50
na huku tukiendeleza amani na mshikamano katika nchi yetu. Sherehe zilionesha
namna gani tumejizatiti kuendelea kuudumisha Muungano wetu, ambao ni wa kipekee
na wa mfano Barani Afrika. Napenda kuwapongeza viongozi wetu mahiri Dkt. Jakaya
Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa
Majeshi ya Ulinzi na Usalama na Dkt Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa mafanikio hayo.
7.
Mheshimiwa
Spika, Nachukua fursa hii kuishukuru Kamati ya Maendeleo ya
Wanawake na Ustawi wa Jamii ya Baraza lako Tukufu chini ya Uenyekiti wa
Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma, pamoja na wajumbe wake wote kwa ushirikiano, mawazo
na michango waliyotupa, ambayo imeisaidia Wizara kuimarisha utekelezaji wa majukumu
yake. Ni matarajio yangu kwamba tutaendelea kushirikiana kwa pamoja katika
kuimarisha utekelezaji wa majukumu yetu, ili kuleta
mabadiliko yanayotarajiwa ya hali za wanawake, vijana, watoto, wazee na jamii
kwa ujumla. Pia, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza lako tukufu
kwa miongozo na michango yao, iliyotuwezesha kutekeleza majukumu ya Wizara kwa
ufanisi. Aidha, napenda pia nichukue fursa hii kumpongeza Mhe. Mahmoud Thabit
Kombo kwa kuchaguliwa kuwa Mwakilishi wa jimbo la Kiembesamaki na kujiunga nasi
katika shughuli za Baraza hili.
8.
Mheshimiwa Spika, Utakumbuka
kwamba mwaka jana nilisoma mbele ya Baraza lako tukufu Hotuba ya Bajeti kwa Wizara
ya Ustawi wa Jamii, Maendeleo ya Vijana, Wanawake na Watoto. Mabadiliko ya
baadhi ya Wizara yaliyofanywa mwezi Agosti 2013, yalipelekea kuanzishwa kwa
Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto. Napenda kutoa
shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa kuniamini na kuniteua kuiongoza
Wizara hii.
MWELEKEO WA BAJETI KWA MWAKA 2014/2015
9.
Mheshimiwa Spika, Bajeti
na shughuli zilizopangwa kutekelezwa na Wizara
yangu kwa mwaka wa fedha 2014/2015 zimezingatia Mipango
Mikuu ya Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar ambayo ni Dira ya Maendeleo ya 2020, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Zanzibar (MKUZA
II – 2010-2015), Malengo ya Milenia 2015, Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha
Mapinduzi (CCM) kwa mwaka 2010-2015, Mwelekeo wa Sera za CCM 2010-2020, Mwelekeo
wa Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2014/2015, Sera za Kisekta
pamoja na Mpango Mkakati wa Wizara. Aidha, matumizi ya Wizara yataelekezwa
zaidi katika kuimarisha programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi, hifadhi ya
jamii kwa wazee na watu wanaoishi katika mazingira magumu zaidi, maendeleo ya
vijana, mapambano dhidi ya udhalilishaji wa wanawake na watoto, pamoja na
kushajiisha usawa na uwiano wa kijinsia.
10.
Mheshimiwa
Spika, Wizara kwa kipindi cha mwaka 2014/2015 imejipangia kutekeleza malengo makuu yafuatayo:
1. Kuimarisha
hali za kiuchumi na kijamii za Vijana, Wanawake, Watoto, Wazee, makundi yanayoishi
katika mazingira magumu na jamii kwa ujumla;
2. Kuhakikisha
kuwa mapungufu ya sera na sheria katika masuala ya uwezeshaji na yanayohusu
watoto, wanawake, vijana, wazee na makundi yanayoishi katika mazingira magumu yanafanyiwa
kazi;
3. Kuimarisha
ubora wa huduma na upatikanaji wa hifadhi ya jamii kwa watoto, wanawake, vijana,
wazee na makundi yanayoishi katika mazingira magumu;
4. Kuhakikisha
kuwa taarifa zinazohusu masuala ya wanawake, vijana, watoto, wazee, hifadhi ya
jamii na uwezeshaji wananchi kiuchumi zinakusanywa na kutumiwa katika kuandaa
na kuimarisha sera, mikakati na programu;
5. Kukuza
uwelewa wa jamii juu ya dhana, misingi na kanuni za Ushirika; na
6. Kuimarisha
uwezo wa Wizara kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
MUHTASARI WA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA
2013/2014
11.
Mheshimiwa Spika, Katika
mwaka 2013/2014,Wizara ilipangiwa kukusanya mapato ya jumla ya Shilingi Milioni
Kumi (Tshs. 10,000,000) kutokana na usajili na huduma za ukaguzi wa vyama vya
ushirika. Hadi kufikia mwezi wa Mei 2014, jumla ya Shilingi
Milioni Tano, laki Tisa na Elfu Thamanini na Tano (Tshs. 5,985,000/=) zilikuwa
zimekusanywa, sawa na asilimia 60 ya makadirio kwa mwaka 2013/2014.
12.
Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa
fedha wa 2013/2014, Wizara ilitengewa Shilingi
Bilioni Tatu, Milioni Mia Mbili Arobaini na Tisa, Laki Sita na Elfu Ishirini na
Mbili (Tshs. 3,249,622,000/=) kwa matumizi ya kazi za kawaida, ikiwa ni pamoja
na mishahara. Hadi kufikia mwezi wa Mei, 2014, fedha zilizotolewa ni Shilingi Bilioni
Mbili, Milioni Mia Nne na Tisini na Tano, Laki Tatu na Hamsini Elfu (Tshs.2,495,350,000/=) ambayo ni sawa na asilimia 77 ya fedha zilizotengwa. Aidha,
Wizara ilitengewa jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Nane na Themanini (Tshs.1,880,000,000/=)
kwa kazi za maendeleo. Fedha zilizotolewa kwa kazi hizo mpaka kufikia mwezi
Mei, 2014 ni Shilingi Milioni
Mia Tano Arobaini na Mbili, Laki Mbili na Elfu Tisini na Mbili (Tshs.542,292,000/=),
ambazo ni sawa na asilimia 29 ya fedha zilizotengwa (Angalia Kiambatanisho Namb. 1a
na 1b).
UTEKELEZAJI WA MALENGO YA WIZARA KWA MWAKA 2013/2014
13.
Mheshimiwa Spika, Majukumu ya Wizara hii yanatekelezwa kupitia Idara
zake nane na Ofisi kuu Pemba kama zifuatazo:
1. Idara ya Mipango, Sera na Utafiti;
2. Idara ya Uendeshaji na Utumishi;
3. Idara ya Uendelezaji na Uratibu wa Programu za
Kuwawezesha Wananchi Kiuchumi;
4. Idara ya Ushirika;
5. Idara ya Mikopo;
6. Idara ya Ustawi wa Jamii,
7. Idara ya Maendeleo ya Vijana; na
8. Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto.
9. Ofisi Kuu Pemba inasimamia shughuli zote za Wizara,
ikiwemo majukumu ya Idara hizi kwa Pemba.
Utekelezaji wa malengo ya
Wizara kupitia Idara hizi kwa mwaka 2013/2014 na malengo kwa mwaka 2014/2015 ni
kama ifuatavyo:
IDARA YA MIPANGO, SERA NA UTAFITI
14.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2013/2014, Idara hii ilijipangia kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kusimamia
uingizwaji wa masuala ya jinsia na mtambuka katika mipango, bajeti, programu/miradi
na sera za kisekta na Wizara;
2. Kusimamia
uandaaji wa tafiti mbili zinazohusu masuala ya jinsia na maendeleo ya vikundi
vya wanawake;
3. Kuimarisha
uratibu, uandaaji na ukusanyaji wa taarifa, ufuatiliaji na tathmini ya mipango,
programu na bajeti ya Wizara;
4. Kuimarisha
mashirikiano ya kitaifa, kikanda na kimataifa ili kuleta maendeleo na ustawi wa
wanawake, vijana, wazee na watoto; na
5.
Kusimamia utekelezaji wa
miradi ya Wizara.
Utekelezaji wa malengo ya
Idara ya Mipango, Sera na Utafiti kwa mwaka 2013/2014:
15.
Mheshimiwa Spika, Miongoni mwa majukumu ya Idara ya Mipango, Sera na
Utafiti ni kusimamia uandaaji wa sera, ili kujenga mfumo mzuri wa utekelezaji
wa shughuli inazozisimamia. Katika hili, Wizara tayari imekamilisha Sera ya Maendeleo
ya Ushirika na Sera ya Hifadhi ya Jamii, ambazo zimeshapitishwa rasmi na ziko
tayari kutumika. Sera hizi zitakuwa ndio dira na
miongozo katika uendeshaji wa vyama vya ushirika na usimamiaji wa mipango ya
hifadhi ya jamii Zanzibar.
16.
Mheshimiwa Spika, Wizara pia imeandaa rasimu ya Sera ya Jinsia ambayo
ipo tayari kujadiliwa katika kikao cha Kamati ya Makatibu Wakuu. Sambamba na hilo,
Wizara inaandaa Mpango wa utekelezaji wa Sera hiyo. Rasimu ya Sera ya Maendeleo
ya Vijana nayo imekamilika na matayarisho yanafanywa ili kuiwasilisha katika
vikao vya maamuzi. Pia Wizara imo katika hatua ya kutayarisha Sera ya
Uwezeshaji, ambapo rasimu ya mwanzo ipo tayari, inasubiri kujadiliwa katika
Kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wizara na hatimae kuwasilishwa katika ngazi
nyengine za maamuzi.
17.
Mheshimiwa Spika, Wizara imefanya mapitio ya Mpango Mkakati wake ili
uendane na mabadiliko yaliyofanywa kuhusiana na majukumu yake na kushughulikia
changamoto mpya zilizojitokeza. Mpango Mkakati huo umekamilika na umetumika
katika uandaaji wa Mpango wa Matumizi wa Muda wa Kati kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015.
18.
Mheshimiwa Spika, Wizara imetayarisha na kuwasilisha kunakohusika
ripoti mbali mbali zinazohusiana na utekelezaji wa majukumu yake. Taarifa hizo
ni pamoja na zinazohusu utekelezaji wa miradi inayosimamiwa na Wizara, utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM (2005) na utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Wizara.
Aidha, ziara za ufuatiliaji zimefanywa ili kuangalia utekelezaji wa
programu za Wizara.
19.
Mheshimiwa Spika, Wizara imo katika hatua ya kukusanya Taarifa za Hali
ya Kijinsia (Gender Profile) kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa
Serikali. Kuwepo kwa taarifa hizo kutasaidia uandaaji wa Sera na Mipango ya Kitaifa
inayozingatia masuala ya kijinsia.
20.
Mheshimiwa Spika, Ili kuimarisha uzingatiaji wa masuala mtambuka katika
sera, mipango na program za Wizara, mafunzo yametolewa kwa wajumbe wa Kamati ya
Wizara inayoshughulikia masuala mtambuka kwa upande wa Unguja. Mafunzo hayo ni
pamoja na yaliyohusu uzingatiaji wa masuala ya kijinsia katika bajeti, mipango,
sera na programu na masuala ya uwezeshaji na ujasiriamali. Kwa upande wa Pemba,
wafanyakazi
na familia zao wamepatiwa mafunzo ya kujikinga na maambukizo
ya virusi vya UKIMWI na
vifo vitokanavyo na UKIMWI, pamoja
na kuhimiza utendaji wa kazi kwa kuzingatia jinsia.
21.
Mheshimiwa Spika, Kamati 18 za Shehia Pemba na 10 Unguja za kupinga
vitendo vya udhalilishaji zimefuatiliwa ili kutathmini utekelezaji wa shughuli
zao na kupewa ushauri na maelekezo ya kuwasaidia kuimarisha kazi zao. Aidha,
jumla ya vijana 120 kutoka Mikoa 3 ya Unguja na 80 kutoka Mikoa miwili ya Pemba
walipatiwa mafunzo ya kupinga vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia na
kuepukana na mimba na ndoa za utotoni. Vile vile, Wizara imesimamia uundwaji wa
kamati kumi na moja (11) za Shehia za kupambana na udhalilishaji wa kijinsia katika
Wilaya ya Chake Chake, Pemba. Aidha, Kamati hizo zilipewa maelekezo na
kujengewa uwezo wa kusimamia shughuli zao kwa kushirikiana na Masheha na
Waratibu wa Wanawake na Watoto wa Shehia.
22.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea
kutoa taarifa mbali mbali kupitia vyombo vya habari ili kuielewesha jamii juu
ya shughuli inazozitekeleza. Jumla ya taarifa 17 za matukio mbali mbali ya
Wizara zilirushwa hewani kupitia vyombo vya habari. Pia vipindi vitatu (3) vya redio
na televisheni kwa ajili ya kushajiisha jamii kupinga vitendo vya udhalilishaji
wa kijinsia viliandaliwa na kurushwa hewani. Vile vile, makala mbili (2) zilizozungumzia
masuala ya haki za wanawake na kupinga vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia ziliandaliwa
na kutolewa katika Gazeti la “Zanzibar Leo”.
Utekelezaji wa Programu zinazosimamiwa na Idara ya Mipango Sera na
Utafiti
23.
Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Idara ya Mipango, Sera
na Utafiti katika kipindi cha mwaka 2013/2014 imesimamia utekelezaji wa
Programu mbili zifuatazo:
Programu ya Jinsia Zanzibar
24.
Mheshimiwa Spika, Programu hii inatekelezwa kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Idadi
ya Watu (UNFPA). Madhumuni ya programu hii ni kuisaidia Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kuzingatia masuala ya kijinsia katika sera, mipango na bajeti,
pamoja na kuzijengea uwezo taasisi mbalimbali na wananchi katika kupambana na
udhalilishaji wa kijinsia.
25.
Mheshimiwa Spika, Katika
mwaka 2013/2014, Wizara kupitia programu hii imetekeleza yafuatayo:
- Imetayarisha miongozo
kwa viongozi wa dini mbili kuu, ya Kiislamu na ya Kikristo, kwa ajili ya
kuwafundisha waumini wao juu ya masuala ya kupinga udhalilishaji wa
kijinsia. Miongozo hii imeshafanyiwa majaribio na marekebisho na ipo
tayari kwa kutumika.
·
Imeandaa Taarifa ya Utekelezaji
wa Mkataba wa Kimataifa wa Kuondoa Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya Wanawake
(CEDAW) kwa upande wa Zanzibar. Taarifa hiyo inayozungumzia
utekelezaji kwa kipindi cha miaka minne
kuanzia mwaka 2011 hadi 2014,
itajumuishwa na ile ya Tanzania Bara kwa ajili ya kuwasilishwa katika Mkutano
wa Umoja wa Mataifa utakaofanyika mwezi Septemba 2014.
·
Imezijengea
uwezo Kamati za kupinga vitendo vya
udhalilishaji wa kijinsia za Mkokotoni, Mahonda na Kinyasini Unguja na
Micheweni na Konde Pemba ili ziweze kufanya kazi zao kwa ufanisi. Jumla ya
Wajumbe 140 wa kamati hizo wamepatiwa mafunzo ya ushauri nasaha, Sheria na
taratibu za kukuza mwitiko dhidi ya vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia na
ufuatiliaji wa kesi.
·
Imefanya tathmini ya mapungufu yaliyopo
katika Sheria ya Usajili wa Ndoa ya
mwaka 1966 sura ya 91 na 92, ambapo tathmini
hiyo iligundua kwamba Sheria hii imejikita zaidi katika masuala ya usajili na
haikugusia masuala muhimu yanayohusu ndoa, ikiwemo suala la haki na wajibu wa
wanandoa, umri wa kuingia katika ndoa, tafsiri ya ndoa na suala la matunzo ya
watoto baada ya kuvunjika kwa ndoa. Aidha, ripoti ya tathmini hiyo ilieleza
kuwa kuna umuhimu wa kuandaliwa Sheria maalum ya ndoa, lakini itanguliwe na
uandaaji wa Sera ya Kuimarisha Familia.
·
Imeandaa Muhtasari
(Fact Sheet) juu ya hali halisi ya udhalilishaji wa kijinsia ambao utatumika kushajiisha jamii
kuchukua hatua dhidi ya vitendo vya udhalilishaji. Vile vile, Wizara imeandaa
mchezo wa kuigiza, wenye sehemu 25, kwa ajili ya kuelimisha jamii juu ya athari
ya ukatili wa kijinsia kupitia redio. Mbali na hayo, Wizara imetayarisha filamu
ya ushuhuda wa vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia Zanzibar, ambayo itatumika
katika programu za kuelimisha jamii juu ya athari za ukatili na udhalilishaji
wa kijinsia.
Programu ya Kukuza usawa wa Kijinsia na Kuwawezesha Wanawake
Kiuchumi
26.
Mheshimiwa Spika, Programu hii inatekelezwa kwa mashirikiano na
Shirika la UN- Women kwa
lengo la kusaidia jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuimarisha usawa wa kijinsia
na kuwawezesha wanawake kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Kupitia
programu hii, Wizara katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 imetekeleza yafuatayo:
·
Imefanya
utafiti wa kuvitambua vikundi vya uzalishaji na vya kiuchumi vya wanawake
katika Wilaya zote 10 za Unguja na Pemba. Utafiti huu utaweza kutambua aina ya
biashara zinazofanywa na kinamama, uimara wa vikundi vyao, mitaji waliyonayo ya
kuendesha biashara zao na maeneo vilipo vikundi hivyo,
·
Imetoa mafunzo ya kuvijengea
uwezo vikundi vya wanawake vya Mkoa wa Kaskazini Unguja, jumla ya wanawake 60
wamenufaika na mafunzo hayo na kwa
upande wa Pemba jumla ya wanawake 60 wa Wilaya ya Micheweni na Mkoani
wamenufaika na mafunzo hayo. Mafunzo hayo yalihusu utengenezaji wa bidhaa,
ufungashaji, ufugaji wa kuku wa kisasa na kienyeji, utengenezaji wa unga wa
lishe, ulimaji wa mboga mboga, utengenezaji wa sabuni na utafutaji wa masoko.
·
Pia
kupitia mradi huu, watendaji wawili wa Wizara
ilihudhuria mkutano wa 58 wa Tume ya Umoja wa Mataifa Juu ya Hadhi ya Wanawake,
uliofanyika New York, Marekani ambapo ujumbe wa mwaka huu ulikuwa ni ‘Changamoto na Mafanikio
katika Kutekeleza Malengo ya Milenia kwa Wanamke na Watoto wa Kike’. Mkutano huo
uliweka azimio la kuweka lengo mahsusi linalohusu usawa wa kijinsia katika
Agenda ya Maendeleo ya Baada ya Mwaka 2015, pamoja na mambo mengine mkazo
uliwekwa katika kumuwezesha mwanamke kiuchumi na kupiga vita vitendo vya
udhalilishaji wa kijinsia. Aidha, ilisisitizwa kuwa malengo mengine yote yaliyobaki
yazingatie usawa wa kijinsia.
27.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2014/2015 Idara ya Mipango,
Sera na Utafiti imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kusimamia
uingizaji wa masuala mtambuka, ikiwemo masuala ya jinsia katika sera, mipango, program
na bajeti za kisekta na Wizara;
2. Kusimamia
uandaaji wa utafiti wa kuangalia athari za utalii na mmonyoko wa maadili kwa
vijana;
3. Kusimamia
uandaaji wa Mpango wa Utekelezaji wa Sera ya Hifadhi ya Jamii, Sera ya Watoto,
Sera ya Uwezeshaji na Sera ya Maendeleo ya Vijana;
4. Kuimarisha
uandaaji, uratibu, ufuatiliaji na tathmini ya mipango na programu za Wizara;
5. Kuimarisha
mashirikiano ya kitaifa, kikanda na kimataifa ili kuleta maendeleo na ustawi wa
wanawake, vijana, wazee, watoto na wananchi wanaoishi katika mazingira magumu
zaidi; na
6.
Kuratibu utekelezaji wa programu
na miradi inayosimamiwa na Wizara.
28.
Mheshimiwa Spika, Ili Idara
ya Mipango, Sera na Utafiti iweze kutekeleza malengo yake iliyojiwekea kwa mwaka wa
fedha 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi
Milioni Mia Moja na Elfu Sitini na Tano (Tshs
165,000,000/=) kwa ajili ya matumizi ya Kazi za Kawaida na Shilingi Bilioni
Mbili, Milioni Mia Mbili na Nne, Laki saba na Elfu Thalathini na Tano (Tshs 2,204,735,000/=) kwa Kazi za Maendeleo.
IDARA YA UENDESHAJI NA UTUMISHI
29.
Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka 2013/14, Idara hii ilipanga kutekeleza malengo
yafuatayo:-
1. Kusimamia
shughuli za kila siku za Uendeshaji na Utumishi za Wizara, ikiwemo Sheria na Kanuni
za Utumishi Serikalini na kuhakikisha wafanyakazi wanafuata Sheria na Kanuni za
Usimamizi wa fedha na manunuzi ya Vifaa vya Ofisi;
2. Kuwajengea
uwezo wafanyakazi wa Wizara kwa kuwasaidia malipo ya ada ya masomo ya muda
mrefu na muda mfupi kwa kuzingatia mahitaji ya Wizara;
3. Kuimarisha
utendaji kazi kwa kusimamia ununuzi wa vifaa muhimu vya kutendea kazi;
4. Kuimarisha
Wizara kwa kuajiri wafanyakazi wapya kumi na nane (18) Unguja na wanane (8)
Pemba; na
5. Kuendelea
kuviimarisha vitengo vya manunuzi, uhasibu na ukaguzi wa ndani.
Utekelezaji wa malengo ya Idara ya Uendeshaji na
Utumishi kwa mwaka 2013/2014
30.
Mheshimiwa
Spika, Katika kusimamia uendeshaji wa shughuli za
kila siku, Wizara imeshughulikia upatikanaji na utunzaji wa vifaa mbali mbali vya
Ofisi, huduma za mawasiliano
na usafiri, pamoja na kuvifanyia matengenezo
vyombo ya usafiri na vifaa vya ofisi Unguja na Pemba. Aidha, Wizara imenunua vespa mbili (2) ili kuimarisha huduma za usafiri kwa ufuatiliaji wa
shughuli za kazi.
31.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imeajiri wafanyakazi wapya 13 (4 wanaume na 9 wanawake) katika fani za Uchumi, Utawala, Katibu Muhtasi,
Udereva, Ufundi, Ushoni na Upishi Unguja na Pemba. Nafasi
hizi zimejazwa kutokana na kuachwa wazi na wafanyakazi waliostaafu kazi
kisheria na wengine kufariki dunia. Aidha, Wizara imepokea wafanyakazi wawili
(2) kwa njia ya uhamisho kutoka taasisi nyengine za Serikali na wafanyakazi tisa (9) walipewa uhamisho
wa kwenda kuendelea na kazi katika Wizara nyengine. Pia, wafanyakazi kumi (10) walistaafu
kazi kisheria,
wafanyakazi wawili (2) waliacha kazi kwa hiari yao na wafanyakazi watatu (3)
walifariki dunia (Angalia Kiambatanisho Namb.2a)
32.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imewapatia mafunzo ya muda mfupi
wafanyakazi 4, (2 Unguja na 2 Pemba)
katika kada ya Ukaguzi wa Hesabu
za Ndani,
Uandishi
wa Kumbukumbu,
Habari
na Mawasiliano.
Pia, Wizara imewasaidia ada ya
masomo wafanyakazi 33
(Unguja 23 na
Pemba 10) wanaochukua masomo ya muda
mrefu katika vyuo mbali mbali nchini Tanzania. Wafanyakazi hao wanasomea fani
za Ustawi wa Jamii,
Uchumi, Sheria, Maendeleo ya Jamii,
Ushirika, Mipango na Uongozi, Uongozi wa Fedha na Ujasiriamali, Utunzaji Kumbukumbu na Ukatibu
Muhutasi
(Angalia Kiambatanisho
Namb. 2b).
33.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imefanya vikao kumi (10) vya Kamati
Tendaji na vikao vitatu (3) vya Kamati ya Uongozi. Miongoni mwa yaliyojadiliwa katika vikao vya
Kamati hizo ni
pamoja na rasimu za Sera
ya Hifadhi ya Jamii, Sera ya Maendeleo
ya Vijana na Sera
ya Maendeleo ya Ushirika, pamoja na taarifa za utekelezaji
wa programu mbali mbali
zinazosimamiwa na Wizara.
34.
Mheshimiwa
Spika, Ili
kuendana na mabadiliko yaliyofanywa katika muundo wa Wizara, Bodi ya
Zabuni na Kamati ya Ukaguzi wa Ndani
ya Wizara zimeundwa upya. Bodi
ya Zabuni imefanya vikao viwili (2) ambavyo, pamoja na mambo mengine, vilijadili na kupitisha Mpango
wa Manunuzi kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya mwaka 2005 na Ripoti za Manunuzi.
Kamati ya Ukaguzi wa Hesabu za Ndani pia imefanya vikao viwili (2) ambavyo
vilipitia na kujadili Ripoti za Ukaguzi wa Ndani zilizowasilishwa.
35.
Mheshimiwa
Spika, Wizara kupitia Kitengo cha Ukaguzi wa Hesabu
za Ndani ilifanya ukaguzi wa mahesabu na matumizi ya Wizara katika Idara, Miradi na Programu zake mbali mbali Unguja na Pemba. Lengo ni kuhakikisha kuwa fedha na mali nyengine za Wizara zinasimamiwa kwa mujibu wa Sheria ya
Fedha na Manunuzi za mwaka 2005.
36.
Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2014/2015 Idara ya Uendeshaji na
Utumishi imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kufanya
tathmini ya mahitaji ya uwezo wa rasilimali watu katika Wizara;
2. Kuimarisha
uwezo wa utendaji kwa kusimamia upatikanaji wa mafunzo ya muda mfupi na mrefu
kwa wafanyakazi 10 (Unguja 8 na Pemba 2) na kuajiri wafanyakazi wapya 76 (Unguja
55 na Pemba 21);
3. Kuimarisha
mfumo wa mawasiliano wa Wizara kwa kununua mtambo na vifaa muhimu vya
mawasiliano vitakavyowezesha kujiunga na mfumo wa Serikali wa mtandao
(E–government), pamoja na kuweka simu za mezani;
4. Kuimarisha
utendaji kazi kwa kusimamia ununuzi wa vifaa mbalimbali vya ofisi;
5. Kuendelea
kusimamia nidhamu, wajibu, na upatikanaji wa haki, maslahi, fursa, na motisha
kwa wafanyakazi wa Wizara Unguja na Pemba; na
6. Kuimarisha
Mfumo wa habari na uhusiano wa Wizara.
37.
Mheshimiwa
Spika, Ili Idara ya Uendeshaji na Utumishi iweze kutekeleza majukumu yake katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe
jumla ya Shilingi Milioni Mia Tatu na Sitini (Tshs. 360,000,000/=) kwa kazi za kawaida na jumla ya
Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Saba na Tano, Laki Moja na Elfu Sitini na
Nne (Tshs. 1,705,164,000/=) kwa
ajili ya Mishahara, Mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na Posho za
wafanyakazi Unguja.
IDARA YA UENDELEZAJI NA URATIBU WA PROGRAMU ZA UWEZESHAJI
WANANCHI KIUCHUMI
38.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 Idara hii
ilipanga kutekeleza malengo yafuatayo:
1.
Kujenga utamaduni wa ujasiriamali
na kuimarisha uwezo wa wajasiriamali, hususan vijana, katika wilaya 10 za
Zanzibar;
2.
Kuimarisha usimamizi,
huduma za ushauri, ufuatiliaji na tathmini shirikishi ya shughuli za uwezeshaji
wananchi kiuchumi;
3.
Kutanua soko la bidhaa za
wajasiriamali wadogo wadogo; na
4. Kuijengea uwezo wa kiutendaji Idara ya
Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi.
Utekelezaji wa malengo ya
Idara ya Uendelezaji na Uratibu wa Programu za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi
2013/2014:
39.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2013/2014, utekelezaji wa
malengo kwa Idara hii ulikuwa kama ifuatavyo:
·
Idara ilipanga
kutoa mafunzo kwa awamu sita juu ya ujasiriamali kwa watu 250 (150 Unguja na
100 Pemba) hususan vijana, lakini kutokana na uhaba wa fedha imeweza kutoa mafunzo
kwa vijana 50 kutoka Mikoa miwili ya Pemba. Mafunzo hayo yalikusudia kuimarisha
utamaduni wa ujasiriamali kwa vijana ili waweze kujiajiri kwa kuanzisha
biashara mbali mbali. Pamoja na mambo mengine, mafunzo hayo yamesaidia vijana
kubuni mipango ya biashara kulingana na fursa zilizopo katika maeneo yao. Kati
ya vijana waliopatiwa mafunzo, vijana 11 (7 wanawake na 4 wanaume) wameweza
kujiajiri kwa kuanzisha shughuli za biashara, kilimo, ufugaji na ushoni.
·
Idara imetoa mafunzo ya awamu 4 kwa wajasiriamali wadogo
wadogo 120 (90 Unguja na 30 Pemba) baada ya kufanya utafiti mdogo wa kubaini
mahitaji yao. Pia imewapatia mafunzo wanavikundi 30 wa Wilaya
ya Magharibi katika vijiji vya Maungani, Kisauni na Bweleo. Baada ya mafunzo
hayo, wanavikundi hao wameunganishwa na wataalamu mbali mbali kulingana na
mahitaji na changamoto zinazowakabili, kama vile masoko, upatikanaji wa vifaa
vya kilimo na upatikanaji wa mashine ya kutotolea vifaranga na mayai inayotengenezwa
kwa kutumia teknolojia rahisi na rasilimali zilizopo nchini.
·
Mafunzo
ya awamu 4 juu ya Uandishi wa Mpango wa Biashara (Business Plan) yalitolewa kwa
wajasiriamali 45 (30 Unguja na 15 Pemba). Kutokana na mafunzo hayo, jumla ya
Mipango ya Biashara 15 ya wajasiriamali
vijana kutoka Mikoa miwili ya Pemba imetayarishwa na kuwasilishwa katika Idara
ya Mikopo kwa ajili ya kufanyiwa tathmini juu ya uwezekano wa kupatiwa fedha za
mitaji kupitia njia ya mkopo. Pia Idara inatarajia kupokea Mipango ya Biashara
30 kutoka Mikoa mitatu ya Unguja kwa kuiwasilisha Idara ya Mikopo kama
ilivyofanywa kwa upande wa Pemba.
·
Jumla ya
wajasiriamali wadogo wadogo 100 (wanawake 70 na wanaume 30) wameshiriki katika
maonesho ya Wiki ya Uwezeshaji yaliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya
Wizara Mwanakwerekwe na Kisonge. Maonesho hayo yamebainisha kwamba wajasiriamali
wadogo wadogo wanahitaji kujengewa uwezo zaidi katika kuimarisha ubora wa
bidhaa zao, viwango na vifungashio ambayo ndiyo changamoto kubwa inayowakabili
katika kumudu ushindani wa soko la ndani na la Afrika ya Mashariki.
·
Kupitia makongano
(clusters), Idara imefanya uchanganuzi wa masoko ya ndani ya wajasiriamali
wadogo wadogo katika Mikoa mitatu ya Unguja, ili kubaini changamoto katika
uzalishaji na uuzaji wa mazao/bidhaa zao. Katika uchanganuzi huo, Idara imeweza
kujua aina mbali mbali za bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali wadogo wadogo,
ubora na wingi wa bidhaa hizo, mitaji na faida inayopatikana, maeneo ya
uzalishaji na uuzaji wa bidhaa hizo na changamoto zinazowakabili. Miongoni mwa
changamoto zilizobainika ni pamoja na uhaba wa bidhaa zinazozalishwa kulingana
na mahitaji ya soko, kutokuwepo kwa uendelevu katika uzalishaji, kukosekana kwa
vifungashio vya bidhaa za wajasiriamali na ubora unaokubalika wa bidhaa.
Changamoto hizo zinaendelea kufanyiwa kazi na Wizara.
·
Kwa kushirikiana
na Wizara ya Biashara na Viwanda, Wizara imeweza kuwasaidia wajasiriamali 50
kushiriki katika maonesho ya 14 ya Juakali/Nguvu kazi ambayo kwa mwaka
2013/2014 yalifanyika Nairobi, nchini Kenya.
·
Katika
kuratibu shughuli za uwezeshaji wananchi kiuchumi, Wizara imefanya mikutano
miwili ya Kamati za Uwezeshaji za Wilaya ya Kusini na Kaskazini A Unguja. Pia
imeandaa mikutano miwili na washirika wengine wa taasisi za Serikali
ili kujadili utekelezaji wa programu na
shughuli mbali mbali za uwezeshaji wananchi kiuchumi wanazozitekeleza. Mikutano
hiyo pia imewashirikisha Waratibu wa programu mbalimbali za uwezeshaji wananchi
kiuchumi, ikiwemo TASAF; Programu ya Miundo Mbinu ya Masoko, Uongezaji Thamani Bidhaa
na Huduma za Kifedha Vijijini (MIVARF); na Programu ya Kukuza Mazingira ya Biashara.
Aidha, mikutano hii imesaidia kubadilishana taarifa juu ya utekelezaji wa
programu hizo na kupeana uzoefu juu ya mikakati iliyoleta mafanikio.
·
Idara
imefanya ziara 3 (2 Unguja na 1 Pemba) za ufuatiliaji wa vikundi vya kiuchumi
na mjasiriamli mmoja mmoja, ambapo jumla ya vikundi 20 (10 Unguja na 10 Pemba)
na wajasiriamali 20 (kumi na tano Unguja na watano Pemba) walitembelewa na
kupatiwa huduma za ushauri, ili kukuza biashara zao (Angalia Kiambatanisho Namb. 3). Ziara
hizo zimesaidia kuona udhaifu na kubaini matatizo yanayovikabili vikundi na
wajasiriamali hao. Aidha, mafunzo ya papo kwa papo yalitolewa ili kutatua
baadhi ya changamoto zilizobainika.
·
Katika
kujenga uwezo wa Idara ili iweze kuyamudu vyema majukumu yake, Wizara
imemgharamia mfanyakazi mmoja wa Idara hiyo kutoka Pemba, kushiriki katika mafunzo ya wiki mbili juu ya masuala ya
uwezeshaji wananchi kiuchumi huko Tanzania Bara.
40.
Mheshimiwa Spika, Katika utekelezaji wa majukumu yake ya kuwawezesha
wananchi kiuchumi, Wizara pia imekuwa
ikishirikiana na taasisi mbali mbali za Serikali na zisizo za Serikali. Wizara
kwa kushirikiana na washirika wengine wa masuala haya imo katika maandalizi ya kuanzisha
Kituo cha Kulelea Wajasiriamali katika Chuo cha Karume cha Sayansi na
teknolojia, Mbweni. Kamati maalumu imeundwa kusimamia uanzishwaji wa kituo
hicho. Kamati hiyo inahusisha wawakilishi kutoka Chuo kikuuu cha Taifa (SUZA),
Jumuiya ya wafanya Biashara, Viwanda na Wakulima, Chuo cha Karume, Mamlaka ya
vyuo vya Amali, Benki ya Watu wa Zanzibar, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Amali, Wizara ya Habari, Wizara ya Mawasiliano, Wizara ya
Kilimo na Maliasili na Shirika la Kazi Duniani. Kituo hicho kitapokamilika kitatoa
taaluma kwa vijana juu ya masuala ya ujasiriamali,
ikiwemo kuwasaidia kuibua na kuendeleza mawazo yao ya biashara pamoja na
kuwaunganisha na huduma za fedha na masoko.
41.
Mheshimiwa Spika, Pia Wizara, kwa msaada wa Tume ya Sayansi na
Teknolojia ya Tanzania (COSTECH) imepata Mtaalaamu wa kujitolea kutoka nchini
Canada, ambaye atasaidia katika masuala ya uimarishaji wa makongano (clusters) ya
wajasiriamali. Mtaalamu huyo, kwa kushirikiana na Chuo cha Karume cha Sayansi
na Teknolojia, Mbweni ametengeneza mashine ya kukaushia mwani na matunda kwa
kutumia nguvu ya jua. Lengo ni kuwasaidia wajasiriamali wadogo wadogo kuweza
kutumia teknologia ya nishati ya jua kwa kuhifadhi bidhaa zao zisiharibike.
Malengo ya Idara ya Uendelezaji na Uratibu wa Programu za
Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kwa mwaka 2014/2015
42.
Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha mwaka 2014/2015, Idara hii
imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:
1.
Kuandaa mafunzo ya
ujasiriamali katika maeneo tofauti kwa vijana 200 wakiwemo wahitimu wa vyuo na
vikundi vya kiuchumi;
2.
Kuanzisha Mtandao wa Wajasiriamali
utakaohusisha taasisi zinazotoa huduma za kifedha na huduma za biashara;
3.
Kukuza mashirikiano na
taasisi nyengine zinazohusika ili kuhakikisha upatikanaji wa masoko kwa bidhaa
za wajasiriamali;
4.
Kuimarisha ufuatiliaji na tathmini
ya shughuli za uwezeshaji wananchi kiuchumi;
5.
Kukamilisha uanzishaji wa Kituo
cha Kutotoa Wajasiriamali (Incubation Center) Unguja; na
6.
Kutoa huduma za kibiashara
kwa wajasiriamali wadogo wadogo kwa kushirikiana na Wizara ya Biashara, Viwanda
na Masoko.
43.
Mheshimiwa Spika, Ili Idara
ya Uendelezaji na Uratibu wa Programu za Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi
iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu
liidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Sitini na Moja, Laki Tano na Elfu Sabini
na Tano (Tshs. 61,575,000/=) kwa matumizi ya kazi za kawaida.
IDARA YA USHIRIKA
44.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/14, Idara ya Ushirika ilipanga
kutekeleza malengo yafuatayo:
- Kuongeza uelewa wa wanachama 3,000 juu ya
Wajibu, Haki na ushiriki katika vyama vya ushirika;
2. Kusimamia
utekelezaji wa Sheria katika uendeshaji wa vyama vya ushirika 1,200;
3. Kuwezesha
uanzishwaji wa vyama viwili vya ushirika vya uzalishaji vinavyohusisha vijana;
4. Kuwezesha
upatikanaji wa mitaji kwa kuendeleza vyama vya ushirika;
5. Kuimarisha
utendaji wa vyama vikuu 6 na Shirkisho la Vyama
vya Ushirika (CUZA);
6. Kuimarisha
mahusiano na washirika wa sekta ya ushirika; na
7. Kuimarisha
mazingira ya kazi, ikiwemo mafunzo kwa wafanyakazi na upatikanaji wa vifaa.
Utekelezaji wa Malengo ya Idara ya Ushirika kwa
mwaka 2013/2014.
45.
Mheshimiwa
Spika, Idara ya Ushirika katika mwaka 2013/2014 imetekeleza yafuatayo:
·
imetoa mafunzo juu ya mbinu za ubunifu,
ushindani, wajibu na haki za wanachama pamoja na dhana ya Ushirika kwa jumla kwa wanachama 2,372 (Wanawake 1,569 na Wanaume 803). Wanachama hao walitoka
kwenye vyama
vya ushirika
209 (Unguja 157 na Pemba 52). Kati ya vyama vilivyopatiwa mafunzo hayo, 67 ni SACCOS na 142 ni vyama vya uzalishaji na
utoaji huduma. Mafunzo hayo yamesaidia kuongeza uelewa wa wanachama hao juu ya haki zao na kwa kiasi fulani yametoa msukumo
kwa
wanachama kufuatilia shughuli za vyama vyao.
·
Katika kusimamia utekelezaji wa Sheria
kwenye vyama
vya ushirika,
Wizara imefanya ufuatiliaji, ukaguzi wa kawaida na kutoa mafunzo ya vitendo kwa
vyama
vya ushirika
629 (360 Unguja na 269 Pemba). Hii ni
miongoni mwa juhudi za kuhakikisha kuwa vyama vya ushirika vinatunza vitabu vya
hesabu na kuweka kumbukumbu
nyengine kwa usahihi, kwa
mujibu wa Sheria na Katiba za vyama husika.
·
Vyama vya ushirika 135 (99 Unguja na 36
Pemba) vimefanyiwa ukaguzi wa hesabu,
ambapo kati
yao 18 ni SACCOS na 117 ni vyama vya uzalishaji mali
na utoaji huduma. Lengo la ukaguzi huo ni kutambua hali ya mahesabu ilivyo kwenye vyama hivyo na
kutoa maoni na ushauri wa kitaalamu juu ya hali halisi ya fedha kwa vyama hivyo. Matokeo ya ukaguzi huo
yameonesha ukuwaji wa wastani wa mitaji kwa baadhi ya vyama vya ushirika. Hata hivyo, elimu zaidi
inahitajika ili kuimarisha udhibiti wa rasilimali na kuleta tija kwenye vyama vya ushirika.
·
Vyama viwili (2) vya Ushirika vya vijana wenye
taaluma ya elimu ya juu vimeanzishwa, kimoja kinajishughulisha na kilimo cha
mboga mboga na chengine kinashughulika na kutoa huduma za kitaalamu kwenye vyama vya ushirika. Vyama hivyo ni; Zanzibar
Professionals Cooperative (ZAPROCO) chenye wanachama 21 (wanawake 10 na wanaume 11) kilichopo
Dole, na Zanzibar Fresh Vegetable Production chenye wanachama 14 (Wanawake 10 na Wanaume 4) kilichopo Maungani, Wilaya
ya Magharibi. Wizara kwa kushirikiana na Shirika
la Kazi Duniani (ILO) imepanga kuvijengea uwezo vyama hivyo kupitia
programu za
ajira kwa vijana, ili viwe mfano kwa vijana wengine kuwapa hamasa ya kujiajiri.
·
Jumla ya
vyama vya ushirika
41 (Unguja 34 na
Pemba 7)
vimepatiwa mafunzo shirikishi ya kuandaa mipango ya biashara. Miradi
iliyoandikiwa mipango ya biashara
inajumuisha ya kilimo cha mboga mboga, ushoni, ufugaji wa samaki, ufugaji kuku, ukaushaji samaki, usagaji wa nafaka, uvuvi, upandaji miti, ufugaji nyuki, ufyatuaji matofali, useremala, kazi za mikono na ufundi umeme. Vikundi hivyo vimeunganishwa
na taasisi za kifedha ili viweze kupatiwa
mikopo kwa utekelezaji wa mipango
yao ya
biashara.
·
Juhudi
za kuimarisha uendeshaji wa Vyama Vikuu na Shirikisho la Vyama vya
Ushirika Zanzibar (CUZA) zimeendelea.
Ziara za ufuatiliaji wa utekelezaji wa majukumu kwa mujibu wa Mipango Mikakati ya
Vyama Vikuu hivyo na
CUZA zimefanywa. Aidha, vikao viwili baina ya Mrajisi wa Vyama vya Ushirika na Bodi ya
CUZA vimefanyika ili kujadili
na kutoa ushauri wa kitaalamu kwa lengo
la kurekebisha kasoro za utendaji zilizobainika. Hatahivyo, Wizara
inaendelea kutoa mafunzo na ushauri zaidi kwa vyama hivyo ili viweze kufanya shughuli zake ipasavyo.
·
Wizara iliandaa maadhimisho ya Siku ya Ushirika Duniani, ambayo huadhimishwa
Jumamosi ya mwanzo ya mwezi Julai kila mwaka. Maadhimisho hayo yalijumuisha
mkutano wa wadau wa kujadili maendeleo na namna ya kukabiliana na changamoto
kwenye vyama vya Ushirika. Aidha, Tamko
Rasmi
la Waziri kuhusiana na maadhimisho ya siku
hiyo lilitolewa. Vile vile, kipindi maalum kupitia Shirika la Utangazaji
Zanzibar (ZBC - TV) kiliandaliwa. Maadhimisho haya pia yalilenga kuwashajiisha wananchi juu ya umuhimu wa Sekta ya Ushirika kwa
maendeleo
ya watu, hasa
wenye kipato cha chini.
·
Ili kuimarisha
mashirikiano na wahusika wengine wa masuala ya ushirika, watendaji
wawili (2) wa Wizara walishiriki katika Mkutano uliofanyika Chuo Kikuu cha
Ushirika na Biashara, Moshi.
Mkutano huo ulijadili hali ya maendeleo
ya ushirika
nchini pamoja na changamoto za upatikanaji wa huduma za mikopo. Pia watendaji hao
walibadilishana mawazo na uongozi wa Chuo Kikuu cha Ushirika juu ya uwezekano wa
Chuo hicho kushirikiana na Vyuo
vilivyopo Zanzibar ili kutoa mafunzo na elimu ya Ushirika.
Malengo ya Idara ya Ushirika kwa mwaka 2014/2015
46.
Mheshimiwa
Spika, Kwa kipindi cha mwaka 2014/ 2015, Idara ya
Ushirika imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kukuza
uwezo wa ushindani wa vyama vya ushirika 10 ili vitoe huduma kwenye soko la
utalii ifikapo Juni 2015;
2. Kuongeza
uelewa kwa wanachama na viongozi 3,000
juu ya maadili, kanuni za ushirika, na mbinu za utendaji bora kwenye vyama vya ushirika
ifikapo Juni 2015;
3. Kusimamia
utekelezaji wa Sheria katika uendeshaji wa vyama vya ushirika 1,400 ifikapo
Juni 2015;
4. Kuimarisha
mashirikiano na washirika ili kubadilishana taarifa na kujifunza mambo mapya ya
kuendeleza sekta ya Ushirika ifikapo 2015;
5. Kuimarisha
ufuatiliaji na tathmini ya maendeleo ya vyama vya ushirika ifikapo Juni 2015;
na
6. Kuimarisha
mazingira ya kazi ikiwemo mafunzo kwa wafanyakazi na upatikanaji wa vifaa.
47.
Mheshimiwa
Spika, Ili Idara ya Ushirika iweze kutekeleza majukumu yake
kwa mwaka 2014/15, naliomba Baraza lako Tukufu kuidhinisha jumla ya Shilingi
Milioni Arobaini na Tisa, Laki Tisa na Elfu Thelathini na Nane (Tshs. 49,938,000/=) kwa matumizi ya kazi
za kawaida.
IDARA YA MIKOPO
48.
Mheshimiwa Spika, Katika
kipindi cha mwaka wa fedha wa 2013/2014, Idara hii ilipanga kutekeleza malengo
yafuatayo:
1.Kutoa mikopo 1,000 kwa vikundi vya kiuchumi na watu
binafsi/mjasiriamali mmoja mmoja yenye thamani ya Tshs. 300,000,000/=;
2.Kuongeza kiwango cha marejesho ya Mikopo kutoka asilimia
85 hadi zaidi ya asilimia 95;
3.Kuimarisha uwekaji wa kumbukumbu za mikopo; na
4.Kuimarisha mashirikiano na uratibu wa shughuli za mikopo
nafuu hapa nchini.
Utekelezaji
wa Malengo ya Idara ya Mikopo 2013/2014
49.
Mheshimiwa
Spika, Kwa
mwaka wa fedha wa 2013/2014 Idara ya Mikopo ilitekeleza yafuatayo:
·
Imetoa
mikopo 550 (Unguja 328 na Pemba 222) kupitia Mfuko wa Kujitegemea, yenye
thamani ya Shilingi Milioni Mia Mbili Tisini na Nne, Laki Nane na Elfu Sabini
na Saba (Tshs. 294,877,000/=). Kati yafedha hizo, Shilingi Milioni Mia Mbili Kumi na Moja, Laki
Nane na Elfu Sabini na Saba (TShs. 211,877,000/=) zilitolewa kwa wakopaji wa Unguja
na Shilingi Milioni Themanini na tatu (Tshs.83,000,000/=)
zilitolewa kwa wakopaji wa Pemba. (Angalia Kiambatanisho Namb. 4). Aidha,
Wizara imetoa mafunzo
kwa Wakopaji 550 kuhusiana na
uwekaji wa kumbukumbu za hesabu, faida za kutumia huduma za kibenki kwa
wakopaji, umuhimu wa kujiwekea akiba na utafutaji
wa masoko. Mafunzo haya yalitolewa ili kuwawezesha wajasiriamali kuzitumia
fedha za mikopo vizuri na kwa malengo
yaliyokusudiwa, pamoja na kusimamia vizuri biashara zao.
·
Imeendelea
kufuatilia marejesho ya mikopo ya Mfuko wa JK/AK, ambapo jumla
ya Shilingi Milioni Thelathini, Laki Sita Elfu Themanini, Mia Nne na Sabini na Nane
(Tshs. 30,680,478/=) zimekusanywa katika kipindi cha kuanzia
Julai 2013 hadi Machi, 2014. (Angalia Kiambatanisho
Namb. 5). Idara pia imefanya
ziara za ufuatiliaji wa marejesho ya mikopo katika Wilaya zote za Unguja na
Pemba. Ziara hizo zililenga kuangalia maendeleo ya miradi ya wakopaji na
changamoto zao, pamoja na kuwashauri juu ya namna bora ya kuendesha biashara
zao, ili waweze kupata tija na kulipa mikopo yao kama inavyotakiwa.
·
Idara
imeanzisha mtandao wa taasisi zinazotoa huduma za kifedha kwa wajasiriamali wadogo
ili kubadilishana taarifa za wakopaji na kufuatilia kwa karibu mwenendo wa
uchukuaji na urejeshaji mikopo. Mtandao huo umejumuisha taasisi mbalimbali za kifedha,
zikiwemo WEDTF; YOSEFO; CRDB; CHANGAMOTO; Jumuiya ya Wafanyabiashara, Wenye
Viwanda na Wakulima Zanzibar; na SACCOS mbalimbali za mijini na vijijini. Kupitia mtandao huo, imeripotiwa kuwa hadi kufikia
mwezi wa Aprili 2014, Jumuiya ya WEDTF imetoa mikopo 196 yenye thamani ya Shilingi
Milioni Sitini na Moja (Tshs. 61,000,000/=);
SACCOS kubwa 16 zimetoa mikopo 216 yenye thamani ya Shilingi Milioni Arobaini
na Mbili (Tshs.42,000,000/=); na CRDB kupitia
Mfuko wa Vijana imetoa mikopo kwa vikundi 116 yenye thamani ya Shilingi Milioni
Mia Mbili Arobaini na Tano (Tshs.245,000,000/=).
·
Idara
imefanya mikutano kadhaa na Mamlaka za Wilaya na Shehia kuhimiza
urejeshwaji wa fedha za mkopo. Mikutano hii pia ilitumika kuwaelewesha washiriki
juu ya madhumuni ya Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, pamoja na Muongozo
wa uendeshaji wake, ikiwemo taratibu za uombaji na utoaji wa mikopo. Aidha, mikutano
hiyo ilisaidia kuongezeka urejeshwaji wa fedha
za mikopo, ambapo hadi kufikia mwezi wa Aprili 2014, jumla ya Shilingi Milioni
Mia Moja na Kumi na Moja, Laki Moja, Elfu Tano na Mia Moja (T.shs
111,105,100/=) zimerejeshwa
katika Mfuko wa Kujitegemea Unguja na Pemba. Kati
ya fedha hizo, Shilingi Milioni Themanini na Tatu, Elfu Hamsini na Nane na Mia
Sita (TShs. 83,058,600/-) zilirejeshwa kutoka kwa wakopaji wa Unguja na Shilingi
Milioni Ishirini na Nane, Elfu Arobaini na Sita
na Mia Tano (Tshs. 28,046,500/=) kutoka kwa wakopaji wa Pemba (Angalia Kiambatanisho
Namb. 6).
·
Ili kujifunza uzoefu wa taasisi
nyengine katika masuala ya mikopo, Idara imefanya ziara za kujifunza kwa
taasisi bora zinazotoa mikopo huko Tanzania Bara. Taasisi zilizotembelewa ni
Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (National Economic Empowerment Council)
na BLUE Finance zilizoko Dar es Salaam.
Pia ziara mbili kwa wafanyakazi wa Idara baina ya Unguja na Pemba zilifanyika,
ambapo waliweza kujifunza na kubadilishana uzoefu katika uwekaji wa kumbukumbu
za mikopo.
·
Idara imeendelea
kufuatilia ahadi za uchangiaji wa fedha zilizotolewa na taasisi,
wafanyabiashara na wananchi mbali mbali kwa ajili ya kutunisha Mfuko wa Uwezeshaji
Wananchi Kiuchumi. ambao ulizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein, tarehe 21 Disemba, 2013. Katika
uchangishaji huo, ahadi za jumla ya Shilingi Bilioni Moja, Milioni Ishirini na
Tatu, Laki Nne na Elfu Tisini (Tshs. 1,023,490,000/=) zilitolewa. Hadi sasa jumla
ya Shilingi Milioni Mia Tisa Sitini na Moja, Laki Nane na Elfu Tisini (Tshs. 961,890,000/=)
fedha taslim zimekusanywa ambazo ni sawa na asilimia 94 ya ahadi zote. Zoezi la
kufuatilia ahadi zilizobaki linaendelea. Naomba nichukue fursa hii kuwapongeza
na kuwashukuru sana Wajumbe wa Kamati ya Rais ya kusimamia uchangiaji wa Mfuko
wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, kwa kazi nzuri waliyoifanya. Chini ya
Mwenyekiti wake Mheshimiwa Haroun A. Suleiman, Waziri wa Nchi (Ofisi ya Rais)
Kazi na Utumishi wa Umma, Kamati hii imefanya kazi kubwa na nzuri ya kupigiwa
mfano. Aidha, nachukua fursa hii kutoa shukurani maalumu kwa taasisi,
wafanyabiashara na wananchi mbali mbali ambao wamechangia fedha kwa ajili ya
kutunisha Mfuko huu. Nataka niwaahidi kwamba Wizara yangu itasimamia vyema
Mfuko huu ili, kuhakikisha unafikia malengo yake ya kuwawezesha wananchi wa
Zanzibar wenye kipato cha chini, kwa
kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu, ili waweze kujiajiri kwa shughuli za
kiuchumi na kujikwamua kutoka kwenye umasikini.
·
Ili kuimarisha utendaji, wafanyakazi
watatu (Unguja mmoja na Pemba wawili) wamegharamiwa kuendelea na mafunzo ya
muda mrefu katika fani ya mikopo na ujasiriamali, usimamizi wa masoko na
usimamizi wa rasilimali watu. Mafunzo hayo yatasaidia kuongeza idadi ya
wafanyakazi wenye taaluma, jambo ambalo ni muhimu katika kuleta ufanisi kwenye
utendaji wa shughuli za Idara.
50.
Mheshimiwa
Spika, Katika kipindi cha mwaka 2014/2015, Idara
hii imepanga kuendelea kutekeleza malengo yafuatayo:
1.Kutoa
mikopo 1,000 yenye thamani ya Shilingi 500,000,000/= kupitia vikundi vya
kiuchumi na Mjasiriamali Mmoja Mmoja katika sekta za kiuchumi;
2.Kuongeza
kiwango cha marejesho ya mikopo kutoka asilimia 85 hadi asilimia 95;
3.Kuanzisha
fursa mpya za mikopo na kuwaelewesha wananchi juu ya Muongozo wa Uendeshaji wa Mfuko wa Uwezeshaji
Wananchi Kiuchumi;
4.Kuimarisha
uwekaji wa kumbukumbu za wateja wa mikopo;
5.Kuendelea
na juhudi za kutafuta fedha kwa ajili ya kutunisha Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi
Kiuchumi ili uendelee kuwasaidia wajasiriamali wengi zaidi;
6.Kuimarisha
mashirikiano na uratibu wa shughuli za mikopo nafuu hapa nchini; na
7.Kuimarisha
uwezo wa watendaji ili kuongeza ufanisi wa kazi.
51.
Mheshimiwa
Spika, Ili
Idara ya
Mikopo iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka wa fedha 2014/2015, naliomba
Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Thamanini na Nne, Laki
Tisa na Elfu Arobaini (T.shs 84,940,000/=) kwa matumizi ya kawaida.
IDARA YA USTAWI WA JAMII
52.
Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, Idara ya Ustawi wa
Jamii ilipanga kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kuimarisha
Mfumo wa Hifadhi ya Mtoto;
2. Kuimarisha
uratibu na kufuatilia masuala ya malezi na makuzi ya awali ya watoto kuanzia
miaka 0-8;
3. Kuimarisha
Hifadhi ya Wazee;
4. Kusimamia
ulipaji wa fidia kwa Wafanyakazi waliopata ajali kazini; na
5. Kuimarisha
shughuli za kuwapatia wanajamii misaada ya kiustawi.
Utekelezaji wa Malengo kwa Idara ya Ustawi wa
Jamii kwa mwaka wa fedha 2013/2014
53.
Mheshimiwa
Spika, Katika
mwaka wa fedha wa 2013/204, Idara ya Ustawi wa Jamii imetekeleza shughuli zifuatazo:
·
Imekusanya
taarifa za udhalilishaji wa watoto kutoka Wilaya za Unguja na Pemba na
kuziingiza katika mfumo
wa kuhifadhi taarifa. Aidha, Vituo vyengine viwili vya Mkono kwa
Mkono vimeanzishwa katika
Hospitali za Wete na Micheweni kwa ajili ya
kurahisisha ushughulikiaji wa kesi za udhalilishaji katika maeneo hayo. Pia, mkutano mmoja (1) umefanywa ili kuwakutanisha wafanyakazi wa Vituo vya Mkono kwa Mkono vya Hospitali ya Mnazimoja, Kivunge na
Makunduchi kwa lengo la kubadilishana uzoefu na kujadili mafanikio
pamoja na changamoto
zinazowakabili katika kutoa huduma
hizo. Pamoja na hayo, Kitengo
cha Hifadhi
ya Mtoto cha Mkoa
wa Kaskazini Unguja kimeimarishwa kwa
kupatiwa
vifaa vya kufanyia kazi,
ikiwemo kompyuta, printa, fotokopi na samani. Hadi kufikia mwezi wa Machi 2014, jumla ya malalamiko 2,356
(2,258 Unguja na 98 Pemba) ya udhalilishaji wa watoto yaliripotiwa na
kushughulikiwa katika vituo vya Mkono kwa Mkono (Angalia
Kiambatanisho Namb. 7a na 7b).
·
Kwa
kushirikiana na Wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Hifadhi ya Watoto, Idara imefuatilia
kesi 20 za watoto waliodhalilishwa zilizoripotiwa katika kipindi cha miezi sita (Agosti -
Januari). Aidha, Mkutano mmoja wa kuratibu na kujadili
changamoto zinazozikabili
Kamati za Hifadhi ya Mtoto za Wilaya zote za Unguja na Pemba umefanyika. Vile vile, familia 10 zimepatiwa msaada wa
kisaikolojia, ushauri nasaha na kupatiwa rufaa kwenda vituo vya Mkono kwa Mkono
kwa kupata
huduma za afya. Kwa upande wa Pemba, kamati zimefuatilia katika Vyombo vya
Sheria jumla ya kesi 60 za udhalilishaji wa watoto. Pia, Idara imeandaa mikutano ya Kamati za Hifadhi ya Mtoto kwa Wilaya nne
za Pemba na ya Kamati
ya Kitaifa ya kushughulikia masuala
ya Hifadhi ya Mtoto, ili kujadili changamoto, matatizo na jinsi ya kukiimarisha kitengo cha
hifadhi ya mtoto Pemba.
·
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kutoka Mahkama mbali mbali Unguja, jumla ya kesi Themanini na Tano (85) za udhalilishaji zimeripotiwa katika
kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014 Unguja; kati ya kesi hizo, kesi za kubakwa ni Sitini na Saba (67) ambapo kesi nne (4) zimeshatolewa
uamuzi, kesi (mbili (2) zimefutwa, kesi mbili (2) zimehukumiwa kifungo na Kesi Sitini na Tatu
(63) zinaendelea kusikilizwa. Kesi za kutorosha watoto ni tatu (3) ambazo zote zinaendelea kusikilizwa na kesi za kulawiti ni kumi na tano (15), ambapo kesi mbili (2) zimetolewa uamuzi wa kufutwa na kesi
kumi na tatu (13) zinaendelea kusikilizwa. Kwa upande wa
Pemba jumla ya kesi 24 zimeripotiwa kutoka Mahkama za Mkoa katika kipindi
cha mwezi wa Julai 2013 hadi Aprili 2014. Kati ya hizo kesi za kubaka ni kumi
na tatu (13), kulawiti tano (5), kutorosha nne (4) na shambulio la aibu mbili (2). Miongoni
mwa hizo, kesi tatu (3), zote
za kubaka, zimeshatolewa hukumu.
·
Katika kuimarisha ufuatiliaji wa
masuala yanayohusu hifadhi ya watoto,
hususan masuala ya ubakaji, Wizara imefanya mikutano miwili ya Kamati ya Hifadhi ya Mtoto inayohusisha Viongozi wa Juu (Mawaziri
na watendaji wakuu wa Serikali kutoka Taasisi zinazohusika), ambayo ilijadili mikakati mbalimbali
ya kuwalinda watoto dhidi ya udhalilishaji. Vile
vile, Wizara imefanya mkutano wa kujadili Kitini cha Kufundishia Masuala ya Hifadhi ya Mtoto na pia
kuwajengea uwezo Maafisa Ustawi, Maafisa Wanawake na Watoto na Masheha
juu ya jinsi ya kuripoti kesi za udhalilishaji, Unguja na Pemba.
·
Kamati za Shehia za kuhudumia
watoto wanaoishi katika mazingira magumu zaidi katika Shehia mbili za Pemba (Kiuyu
Kigongoni na Minungwini Wilaya ya Wete Pemba) zilifuatiliwa na kupatiwa mafunzo juu ya namna ya kuwatambua na kuwahudumia
watoto wanaoishi katika mazingira
magumu. Aidha,
utambuzi wa watoto wanaoishi katika mazingira magumu
zaidi katika maeneo hayo
ulifanyika. Pia,
ili kuimarisha upatikanaji wa taarifa, Wizara
kwa kushirikiana na ‘Measure Evaluation’ imeandaa Mpango Kazi wa miaka mitatu wa ufuatiliaji
na tathmini ya
watoto wanaoishi katika mazingira magumu zaidi.
·
Idara imeendelea
kuhudumia Nyumba ya Kulelea Watoto Mazizini yenye jumla ya watoto 38. Watoto
hao walipatiwa huduma za chakula, afya, vifaa vya skuli na nguo. Aidha, Wizara
imeendelea kutoa misaada ya kijamii kwa watu wasiojiweza na watu wanaoishi
katika mazingira magumu zaidi katika jamii, wakiwemo wazee 163 wanaoishi katika
nyumba za wazee Sebleni na Welezo Unguja na Limbani na Makundeni Pemba. Pia, familia
75 Unguja na 55 Pemba zinazoishi katika mazingira magumu zaidi zimepatiwa
misaada ya fedha za kujikimu.
·
Idara imeanza
kufanya utambuzi wa wazee wote wa Zanzibar ili kujua idadi yao halisi na kuweza
kupanga mipango bora kwa mujibu wa mahitaji yao. Aidha, Idara iliandaa maadhimisho ya Siku ya Wazee duniani tarehe 01.10.2013 Unguja
na Pemba. Katika maadhimisho hayo, Wizara ilisisitiza umuhimu wa jamii kutunza
na kuwaenzi wazee, na kuwa jukumu la Serikali ni kuwahudumia wazee ambao hawana
wa kuwahudumia kabisa. Pamoja na hayo, Wizara ilizika maiti nane (8) zisizokuwa
na wenyewe zilizoripotiwa katika hospitali na maeneo mbalimbali.
·
Idara
inaendelea na kazi ya kupokea madai na kulipa fidia kwa wafanyakazi wanaopatwa
na ajali wakiwa kazini, ambapo kwa mwaka 2013/14 jumla ya wafanyakazi 11 (10
Unguja na mmoja Pemba) walilipwa. Aidha,
Wizara bado ina deni kubwa la fidia lililofikia TShs. 96,808,293/= kwa wafanyakazi 89 wa Unguja na
Pemba. Fedha
hizo zimeshapatikana na watu wote
wanaodai madeni hayo wameanza kulipwa. (Angalia
Kiambatanisho 8a
na 8b).
54.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015
Idara ya Ustawi wa Jamii imejipangia kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kuimarisha
mfumo wa Hifadhi ya Mtoto ifikapo mwaka 2015;
2. Kuratibu na kufuatilia masuala ya malezi na makuzi ya watoto;
3. Kuimarisha Hifadhi ya Wazee ;
4.
Kuendeleza utoaji wa misaada ya kiustawi kwa wananchi
wanaoishi katika mazingira magumu zaidi ;
5.
Kuimarisha Mfumo wa hifadhi ya Jamii ifikapo mwaka
2015; na
6.
Kusimamia ulipaji wa fidia kwa watu wanaopatwa na
ajali kazini.
55.
Mheshimiwa
Spika, Ili Idara ya Ustawi wa Jamii
iweze kutekeleza vyema malengo yake kwa mwaka 2014/2015, naliomba Baraza
lako Tukufu liiidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Mia Mbili Tisini na Moja
na Laki Tano (Tshs. 291,500,000/=)
kwa kazi za kawaida.
IDARA YA MAENDELEO YA VIJANA
56.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2013/2014, Idara ya Maendeleo ya Vijana ilipanga
kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kuratibu
uanzishwaji wa Baraza la Vijana;
2. Kuratibu
Mpango wa Mikopo kwa Vijana na kuwahamasisha kujiunga na vyama vya ushirika na
mikopo;
3. Kuratibu
na kufuatilia utekelezaji wa Mpango wa Elimu ya Stadi za Maisha kwa Vijana
walio nje ya Skuli;
4. Kuratibu
Mbio za Mwenge wa Uhuru na Wiki ya Vijana Kitaifa;
5. Kufanya
uratibu, ufuatiliaji na uhamasishaji wa vikundi vya vijana;
6. Kuimarisha
mashirikiano na uhusiano wa Taasisi za Vijana ndani na nje ya nchi; na
7. Kuendeleza
na kuimarisha miundo mbinu ya uzalishaji wa mazao ya kilimo cha rossela na mbogamboga
kwa vijana Unguja na Pemba.
Utekelezaji wa malengo ya
Idara ya Maendeleo ya Vijana kwa mwaka 2013/2014
57.
Mheshimiwa Spika, Katika
kufanikisha malengo iliyojiwekea, Idara ya Maendeleo ya Vijana katika mwaka 2013/2014 imeweza kutekeleza yafuatayo:
·
Iliendelea
na taratibu za Kisheria za kuanzisha Baraza la Vijana la Zanzibar. Sheria ya
kuanzisha Baraza hilo tayari imepitishwa na Baraza lako Tukufu na mchakato wa
kuandaa kanuni kwa ajili ya utekelezaji wa Sheria hiyo unaendelea.
·
Imeshiriki katika kuratibu
Mbio za Mwenge wa Uhuru na Wiki ya Vijana Kitaifa, ambapo
kilele chake kiliadhimishwa tarehe 14/10/2013 Mkoani Iringa. Jumla ya miradi ya
maendeleo 1,229 yenye thamani ya Shilingi Bilioni Mia Moja Thamanini na Nne, Milioni Mia Tano
Thamanini
na Saba, Laki Sita Sitini na Saba, Mia Sita Kumi na Tatu na Senti Arobaini (Tshs. 184,587,667,613.40/=) ilikaguliwa,
kuzinduliwa au kuwekewa mawe ya msingi Tanzania
nzima. Kati ya hiyo, miradi 78
ilikuwa ya Zanzibar, ambapo kati yao 38 ilikaguliwa, 21 iliwekewa mawe ya
msingi na 19 ilizinduliwa. Aidha, jumla ya fedha taslimu kiasi cha Shilingi
Milioni Sitini na Sita, Elfu Tisini
na Nne, Mia Sita na Arobaini (Tshs.66,094,640/=) zilikusanywa wakati wa Mbio
za Mwenge katika Mikoa ya Zanzibar, kwa ajili ya kusaidia
utekelezaji wa miradi iliyozinduliwa (Angalia
Kiambatanisho
Namb. 9 na 10).
·
Kupitia
Idara hii, Wizara imeshirikiana na Wizara ya Habari,
Vijana, Utamaduni na Michezo ya SMT katika kufanya maandalizi ya uzinduzi wa Mbio
za Mwenge wa Uhuru,
uliofanyika tarehe 02/05/2014 katika Wilaya ya Bukoba, Mkoani Kagera. Ujumbe Mkuu wa
mwaka huu ni “Katiba ni
Sheria Kuu ya Nchi”, chini ya kauli mbiu “Jitokeze kupiga kura ya maoni tupate Katiba mpya
iliyo bora”. Sambamba
na ujumbe huo mapambano dhidi ya UKIMWI, Dawa za Kulevya, Rushwa na Malaria umekuwa
ni ujumbe wa kudumu unaoendelea kutolewa wakati wa Mbio za Mwenge.
·
Idara
iliendelea kuratibu utoaji na urejeshaji wa mikopo ya Mfuko wa Vijana, ambapo mikopo 116 imetolewa yenye thamani ya Shilingi
Milioni Mia Mbili Arobaini na Tano (Tshs.245,000,000/=) Unguja na Pemba. Aidha,
fedha zote zilizokopwa zimesharejeshwa.
Hata hivyo, kulijitokeza changamoto ya
ucheleweshaji wa marejesho ya mikopo kwa upande wa Pemba, hali iliyopelekea Wizara
kwa kushirikiana na Benki ya CRDB kuandaa
ziara maalumu, ambayo
ilifanikisha kurejeshwa kwa fedha za mikopo iliyocheleweshwa, yenye
thamani ya Shilingi Milioni Ishirini na Sita (Tshs. 26,000,000/=).
·
Katika jitihada za kukuza ajira
kwa vijana, Idara imendelea na juhudi za
kuwahamasisha vijana
Unguja na Pemba kujiunga katika vyama
vya ushirika
na kuanzisha miradi ya kiuchumi katika sekta za kilimo, uvuvi, ufugaji, biashara na ufundi wa
aina mbali mbali.
Kufuatia juhudi hizo, vikundi 30 vimeanzishwa katika Wilaya ya Chake Chake na viongozi wake kupatiwa
mafunzo ya ujasiriamali. Aidha, mafunzo yalitolewa kwa vijana 60 (40 Unguja na 20 Pemba) katika
nyanja za ukuzaji biashara, masoko, utawala na usimamizi wa miradi, ili kuimarisha uzalishaji katika
vikundi vyao. Pia, jumla ya vikundi 103 vya Vijana
vilitembelewa na kupewa ushauri na maelekezo ya jinsi ya kuendesha miradi yao (Angalia
Kiambatanisho
Namb. 11). Vilevile, kwa kushirikiana na SACCOS ya Vijana Pemba, jumla ya vikundi 55 vya
ujasiriamali vya vijana vilihamasishwa
juu ya umuhimu
wa kujiunga na SACCOS hiyo ili
waweze kupata mikopo yenye masharti nafuu, kwa lengo la kuweza kuimarisha
na kuendeleza shughuli zao za uzalishaji (Angalia Kiambatanisho
Namb. 12).
·
Katika kuimarisha mashirikiano na
uhusiano wa Taasisi za Vijana ndani na nje ya nchi, Vijana wanne (4)
wameshiriki katika Mikutano ya Vijana huko Austria na Misri. Aidha, kwa
kushirikiana na Shirika la UVIKIUTA, vijana wa Zanzibar kwa kushirikiana
na vijana
wa Tanzania Bara,
walipatiwa mafunzo ya uongozi wa kambi za kimataifa za vijana, ambazo madhumuni
yake ni kuhamasisha vijana juu ya uzalendo na kuipenda nchi yao,
kubadilishana mawazo juu ya changamoto mbalimbali zinazowakabili vijana na namna ya
kukabiliana nazo. Kupitia makambi haya,
vijana hushiriki katika shughuli za ujenzi wa taifa katika miradi ya jamii kama
vile ujenzi wa skuli, vituo vya afya na uhifadhi wa mazingira.
·
Wizara kwa kushikiana na Shirika la
Idadi ya Watu Duniani (UNFPA) na Tume ya UKIMWI Zanzibar, imeandaa Kitini na Muongozo wa Mafunzo
ya Stadi za Maisha kwa Vijana.
Kitini na Muongozo huo vimefanyiwa majaribio kwa maandalizi ya mwisho ya
kutumika rasmi. Muongozo huu utasaidia kutoa elimu kwa vijana, itakayowasaidia kujitambua na
kuepukana na changamoto wanazokabiliana nazo.
·
Ili kuyaimarisha mashamba ya mauwa na mbogamboga ya vijana Tunguu, Unguja na Mbuzini, Pemba, Wizara
kupitia Idara ya Maendeleo ya
Vijana, imeendelea
na taratibu za uwekaji wa miundo mbinu. Hii ni pamoja na kuweka miundombinu ya umwagiliaji
majii kwa kutumia mfumo wa “drip irrigation”, pamoja na “green house” mbili
kwa Unguja. Kwa upande wa Pemba, Wizara
inaendelea na hatua za uimarishaji miundo mbinu, ambapo imeweza kumalizia utiaji
wa milango na madirisha ya kibanda cha kuwekea pampu ya maji. Lengo kwa upande
wa Pemba ni kuweka “green house” kama Tunguu. Kwa hivi sasa vijana wanalitumia shamba hilo la
Mbuzini kwa kulima mpunga.
58.
Mheshimiwa Spika; Kwa
mwaka wa fedha 2014/2015 Idara ya Maendeleo ya Vijana imepanga
kutekeleza Malengo yafuatayo:
1)
Kuratibu utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya
Vijana;
2)
Kuratibu na kufuatilia uanzishwaji wa Baraza la
Vijana;
3)
Kuratibu mbio za Mwenge wa Uhuru na Wiki ya Vijana
kitaifa;
4)
Kuwahamasisha, kuwaandaa na kuwaunganisha vijana
na fursa mbali mbali za kiuchumi zilizopo;
5)
Kuratibu utekelezaji wa Kitini na Muongozo wa Stadi
za Maisha kwa Vijana walio nje ya Skuli;
6)
Kufanya ufuatiliaji wa shughuli za kiuchumi na
kijamii za Vijana; na
7)
Kuimarisha ushirikiano na taasisi
zinazoshughulikia masuala ya Vijana ndani na nje ya nchi.
59.
Mheshimiwa Spika; Ili Idara ya Vijana iweze
kutekeleza majukumu yake naliomba Baraza lako tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Sabini
na Tatu, Laki Tano na Elfu Thelathini na Tatu (Tshs. 73,533,000/=) kwa
kazi za kawaida.
IDARA YA MAENDELEO YA
WANAWAKE NA WATOTO
60.
Mheshimiwa Spika, Kwa
kipindi cha mwaka wa fedha wa 2013/2014, Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto
ilipanga kutekeleza malengo yafuatayo:
1. Kuratibu na kusimamia haki za wanawake na watoto;
2. Kuratibu na
kufuatilia utekelezaji wa Sera na Sheria ya Mtoto;
3. Kuimarisha uratibu wa shughuli za kiuchumi na maendeleo ya
wanawake na watoto;
4. Kuimarisha mashirikiano ya kitaifa, kikanda na kimataifa kwa
mambo yanayohusu wanawake na watoto.
Utekelezaji wa malengo ya
Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto kwa mwaka 2013/2014
61.
Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa malengo ya Idara hii kwa mwaka
2013/2014 ulikuwa kama ifuatavyo:
·
Katika
kuratibu na kusimamia, haki za wanawake na watoto, Kamati ya kupambana
na vitendo vya udhalilishaji dhidi ya
watoto imeanzishwa. Kamati hiyo imejumuisha wawakilishi 30 kutoka katika
taasisi za Serikali na zisizo za Serikali. Tayari Kamati hiyo imeanza kazi na
imekuwa ikiendesha mikutano ya kujadili masuala mbali mbali yanayohusu hali na
ustawi wa watoto wa Zanzibar.
·
Wizara kupitia Idara hii, imetayarisha nyenzo za mawasiliano za masuala ya
udhalilishaji wa watoto na kuzifanyia mapitio kwa kuwashirikisha wadau wa
masuala ya watoto wakiwemo wanafunzi,
walimu na wazazi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja. Pia, Wizara imetayarisha Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini
ambao utasaidia upatikanaji wa taarifa
na takwimu zinazohusu haki za watoto.
·
Idara imeendelea kuyapokea, kuyashughulikia na kuyapatia ufumbuzi malalamiko
yanayohusu wanawake, ambapo kwa mwaka 2013/2014 jumla
ya malalamiko 119 (Unguja24 na Pemba 95)
yalipokelewa na kupatiwa ushauri na maelekezo yanayofaa. Malalamiko hayo yalihusu kupigwa, kupewa ujauzito,
kubakwa, kutelekezwa na mume, kuunguzwa moto, madai ya fedha na madai ya nyumba
(Angalia Kiambatanisho Namb.13a, 13b).
·
Idara iliratibu maandaalizi ya
Siku ya Wanawake Duniani,
ambayo huadhimishwa kila mwaka ifikapo mwezi wa Machi. Kauli mbiu ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2014 ilikuwa ni “ONGOZA MABADILIKO KWA MAENDELEO YA WANAWAKE”. Kwa upande wa Zanzibar, maadhimisho hayo yalihusisha shughuli mbali mbali
zikiwemo: Kuandaa vipindi vya redio na Televisheni; Kufanya
usafi wa mazingira katika nyumba za
wazee Sebleni; Kuendesha makongamano katika Wilaya za Kusini na Mjini; Maonesho ya kazi za Sayansi kwa
wanafunzi wanawake; na Kufanya
uhamasishaji wa upimaji na uchangiaji wa
damu salama. Siku ya Kilele (tarehe 08
Machi, 2014), kuliendeshwa Kongamano la Wanawake, ambapo washiriki walipata fursa ya kujadiliana juu ya hali ya Wanawake katika nyanja za kuchumi,
kisiasa, kijamii na afya, pamoja na udhalilishaji wa kijinsia.
·
Katika kupiga vita vitendo vya
udhalilishaji kwa wanawake, Umoja wa Mataifa umeweka siku 16 maalum (kuanzia
tarehe 25 Novemba hadi tarehe 10 Disemba ya kila mwaka) kwa nchi wanachama
kufanya kampeni na kuhamasisha jamii juu ya kupambana na vitendo hivyo. Kwa
Unguja, kampeni hiyo iliendeshwa kwa kuandaa kongamano la siku moja
lililowashirikisha wadau kutoka taasisi
za Serikali na zisizo za Serikali. Kwa upande wa Pemba, Wizara ilishirikiana na
SOS kuandaa maandamano na mkutano
wa hadhara
iliyohusisha, pamoja na mambo mengine, mabango yenye ujumbe wa kupinga
udhalilishaji, michezo ya kuigiza na hotuba za viongozi. Kwa mwaka 2014, kampeni hii iliendeleza ujumbe
unaosema “AMANI YA DUNIA HUANZA NYUMBANI; TUPINGANE NA
VITENDO VYA UTUMIAJI WA NGUVU DHIDI YA WANAWAKE NA WATOTO”.
·
Idara imeratibu uanzishwaji wa Mabaraza ya Watoto 38 ya Shehia (Unguja 29 na Pemba 9) ili kuinua
ushiriki wa watoto katika mambo yanayowahusu. Kwa Unguja Mabaraza hayo yameanzishwa katika Wilaya za Kaskazini B
(8), Kaskazini A (1), Mjini (10) na Kati (10) na kwa Pemba yameanzishwa katika Wilaya
za Wete (3) na Mkoani (6). Mabaraza haya yanasaidia watoto kujua haki zao na
kusaidia kuripoti matukio mbali mbali yanayohusu watoto. Mabaraza mawili ya watoto ya Wilaya ya Magharibi katika maeneo ya
Mwanakwerekwe na Welezo yamekaguliwa ili kuangalia utendaji wao. Hali ya
Mabaraza ya Watoto imeonesha kuwa yamekuwa yakikosa ushirikianao kutoka kwa
viongozi, wakiwemo Madiwani, Wabunge na Wawakilishi katika maeneo yao. Aidha, kwa
upande wa Pemba Mabaraza kumi na moja (11) yametembelewa
kuangalia utendaji wake, ambapo ilibainika kuwa yanaendelea vizuri, watoto
wanasaidiana na wanatoa taarifa juu ya
mambo yanayohusu watoto yanayotokezea katika shehia zao.
·
Katika
Kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa Sera na Sheria ya
Mtoto, Idara imeendesha
mafunzo juu ya ushughulikiaji wa masuala ya
watoto wanaokinzana na Sheria. Mafunzo hayo yalitolewa kwa watendaji 53 kutoka taasisi za Serikali na zisizo za Serikali
zinazoshughulikia masuala ya watoto.
Lengo ni kuhakikisha kuwa watoto wanaokinzana
na sheria wanashughulikiwa katika ngazi ya jamii, badala ya utaratibu wa kimahkama uliopo sasa, ikizingatiwa suala zima la kulinda haki zao za msingi kama ilivyoelekezwa katika
Mkataba wa Haki za Mtoto.
·
Idara pia imesimamia uandaaji wa Mkakati wa Haki za Mtoto (2013-2018) pamoja
na Mpango wa Utekelezaji kwa mwaka 2014. Uandaaji wa Mkakati huo
pamoja na Mpango wake wa utekelezaji ulishirikisha taasisi nyengine zinazohusika, zikiwemo Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka, Mahkama, Vyuo vya Mafunzo, Polisi, na
Taasisi zisizo za Serikali. Aidha, Wizara
imeandaa kanuni kwa ajili ya uendeshaji wa Mahkama ya Watoto kwa lengo la kuimarisha
upatikanaji wa haki za watoto.
·
Kwa kushirikiana na UNICEF, Wizara imo katika hatua
za kuandaa Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Masuala ya Haki za Kisheria za Mtoto (Child Justice Monitoring
and Evaluation Framework). Mfumo
huu, pamoja na mambo mengine, utawezesha Wizara kufahamu kesi za watoto
zilizopo na hatua zilizofikiwa katika Mahkama, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka
na Polisi. Aidha, utawezesha kujua kama mfumo wa sheria unazingatia ipasavyo
masuala ya haki za watoto, kama yalivyoainishwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watoto na Mkataba wa
Afrika kuhusu haki za Watoto.
·
Kupitia
Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto, juhudi
za kuviimarisha vikundi vya kiuchumi vya wanawake zimeendelezwa. Jumla ya vikundi 70 vilitembelewa kwa lengo la kutathmini mahitaji na
maendeleo yao, pamoja na
kuona changamoto zinazowakabili ili kuwapatia ushauri unaofaa kwa
ajili ya kuimarisha shughuli zao za kiuchumi (Angalia Kiambatanisho Namb. 14). Aidha, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Biashara, Viwanda na
Masoko imeviwezesha vikundi 49 vya wajasiriamali wanawake (42
Unguja na 7 Pemba) kushiriki katika Maonesho
ya 36 ya Sabasaba, kwa lengo
la kutangaza biashara zao. Vile
vile, mafunzo ya ujasiriamali na namna
ya kutafuta masoko yametolewa kwa Waratibu
wa Shehia 99 wa shughuli za wanawake na
watoto katika Wilaya za Kaskakazini A, Magharibi na Kati Unguja, ili waweze
kutoa mafunzo kwa vikundi vilivyopo katika maeneo yao. Kwa upande wa Pemba, tathmini
ya vikundi vya ujasiriamali vya wanawake imefanywa katika Shehia 33 za Mkoa wa
Kaskazini (21 Wete na 11 Micheweni) kwa lengo la kupata taarifa sahihi za
vikundi hivyo. Taarifa hizo zitatumika
katika kuandaa mipango ya kuviimarisha vikundi hivyo (Angalia Kiambatanisho Namb. 15).
62.
Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha wa
2014/2015, Idara ya Maendeleo ya Wanawake na Watoto imepanga kutekeleza malengo
yafuatayo:
1. Kuratibu na kusimamia haki za wanawake na watoto;
2. Kuratibu na kufuatilia
utekelezaji wa Sera na Sheria ya Mtoto;
3. Kuimarisha uratibu na ufuatiliaji wa shughuli za kiuchumi,
kijamii na maendeleo ya wanawake na watoto;
4. Kuratibu na kufuatilia utekelezaji wa Mabaraza ya Watoto;
5. Kuimarisha mashirikiano ya kitaifa, kikanda na kimataifa
kwa mambo yanayohusu wanawake na watoto; na
6. Kuratibu na kusimamia mapambano dhidi ya udhalilishaji wa
wanawake na watoto.
63.
Mheshimiwa Spika, Ili Idara ya Maendeleo ya
Wanawake na Watoto iweze kutekeleza malengo yake kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015,
naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi Milioni Sitini, Laki
Saba na Elfu Sitini na Tatu (Tshs. 60,763,000/=) kwa kazi za kawaida na
Shilingi Milioni Mia Moja Tisini na Tano
na Laki Sita (Tshs.195,600,000/=) kwa
kazi za Maendeleo.
OFISI KUU PEMBA
64.
Mheshimiwa Spika, Ofisi kuu Pemba inasimamia shughuli zote za Wizara kwa
upande wa Pemba, ikiwemo utekelezaji wa majukumu ya Idara mbali mbali za
Wizara. Hivyo, utekelezaji wa majukumu kwa mwaka 2013/2014 pamoja na malengo kwa mwaka
2014/2015 kwa Ofisi hii, ni kama ilivyoainishwa katika Idara husika, ambazo
maelezo yake yamehusisha pia na Pemba.
65.
Mheshimiwa Spika, Ili Ofisi Kuu Pemba iweze kutekeleza majukumu yake kwa
mwaka wa fedha 2014/2015, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya
Shilingi Milioni Mia Tatu Thelathini na Nane, Laki Tano na Elfu Hamsini (Tshs. 338,550,000/=) kwa Kazi za Kawaida
na Shilingi Milioni Mia Nne Hamsini na Thelathini na Sita Elfu (Tshs. 450,036,000/=) kwa ajili ya mishahara,
mchango wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii na maposho ya wafanyakazi.
HITIMISHO
66.
Mheshimiwa Spika, Tunatambua na kuthamini sana
michango ya Washirika wa Maendeleo katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu
ya Wizara. Napenda nichukue nafasi hii adhimu, kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi
ya zanzibar, kuwashukuru sana washirika wetu wa maendeleo kwa mashirikiano
waliyotupa katika utekelezaji wa majukumu yetu ya kuimarisha ustawi na
maendeleo ya vijana, wanawake, watoto, wazee na wananchi wanaoishi katika
mazingira magumu zaidi. Washirika hao ni pamoja na nchi wahisani, ikiwemo Umoja
wa Ulaya, India na Jamhuri ya Watu wa China na Mashirika ya Kimataifa, ikiwemo UNFPA, UNICEF, UNESCO, UNDP, ILO, SAVE THE CHILDREN, FHI, Tunajali
Program, CHAI, Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika, pamoja na Jumuiya
ya Afrika ya Mashariki na Jumuiya ya Madola;
67.
Mheshimiwa Spika, Katika
kutekeleza majukumu yake, Wizara pia ilishirikiana na Wizara na taasisi nyengine
za Serikali pamoja na zisizo za Serikali, ikiwemo sekta binafsi. Napenda
kuchukua fursa hii kuzishukuru taasisi hizo kwa mashirikiano waliyotupa na
naziomba tuendelee kushirikiana, ili kwa pamoja tuweze kufikia malengo
tuliyopanga kwa maslahi ya wananchi na Taifa letu kwa jumla.
68.
Mheshimiwa Spika,
Natoa shukrani maalum kwa Ofisi za Mikoa, Wilaya na Shehia kwa mchango wao
katika usimamizi na ufuatiliaji wa masuala mbali mbali yanayohusu Wizara kwenye
maeneo yao, ikiwa pamoja na masuala ya kupiga vita udhalilishaji wa wanawake na
watoto. Pia natoa shukrani kwa taasisi za kiraia ambazo zimechangia katika
juhudi za Serikali za kuimarisha ustawi na maendeleo ya vijana, wanawake,
watoto, wazee na wanaoishi katika mazingira magumu zaidi. Taasisi hizo ni
pamoja na ZAYEDESA, ZACA, ZAIADA, ZAWDO,
ZAFELA, ZAWCO, ZAMWASO, ZANGOC, ZLSC, COWPZ, PIRO, UVIKIUTA, UWT, ACTION AID, WEDTF,
TAWLA, TAMWA, CHANGAMOTO, PRIDE, TMC na TGNP. Shukurani zangu pia ziende kwa taasisi za kifedha, ikiwemo BOT, PBZ, CRDB, FBME,
na Benki ya Posta kwa mashirikiano yao mazuri kwa Wizara, hususan kwenye
program za uwezeshaji wananchi kiuchumi.
69.
Mheshimiwa Spika, Vyombo
vya habari navyo vimetoa mchango mkubwa katika utekelezaji wa shughuli zetu,
ikiwemo kutangaza matukio mbali mbali yaliyohusu Wizara, pamoja na kuelimisha
jamii juu ya masuala ambayo Wizara inayafanyia kazi, ikiwemo programu za kupinga
vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto. Hivyo, nachukuwa fursa hii
kuwapongeza viongozi na watendaji wa vyombo hivyo vya habari, vikiwermo redio,
televisheni na magazeti kwa mashirikiano yao kwa Wizara.
70.
Mheshimiwa Spika, Yote
ambayo nimeyaeleza yametekelezwa kwa shirikiano mkubwa wa Watendaji Wakuu na Wafanyakazi
wote wa Wizara. Napenda kuwashukuru na kuwapongeza Wafanyakazi wote wa
Wizara ya Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto kuanzia
Katibu Mkuu Nd. Asha Ali Abdulla, Manaibu Katibu Wakuu Nd. Ali Khamis Juma na
Nd. Msham Abdalla Khamis, Wakurugenzi, Ofisa Mdhamini pamoja na Maafisa wafanyakazi
wa ngazi zote kwa kufanya kazi kwa umakini na juhudi kubwa. Mashirikiano haya yamepelekea
kutekeleza malengo na majukumu yetu kwa ufanisi mkubwa. Aidha, nawaomba waendeleze
umoja, mashirikiano, mshikamano, upendo na nidhamu ili tuweze kufanikisha vyema
malengo yetu kwa mwaka wa fedha unaokuja na itakayofuata.
71.
Mheshimiwa Spika, Ili Wizara ya Uwezeshaji,
Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto iweze kutekeleza malengo na
majukumu yake kwa mwaka wa fedha 2014/2015, kwa heshima
na taadhima
nawaomba Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati yako wapokee, wajadili, watupe ushauri
na maelekezo na hatimae wapitishe na kuidhinisha matumizi ya jumla ya Shilingi Bilioni Saba,
Milioni Mia Tano Sabini, Laki Sita na Elfu Sabini (Tshs. 7,570,670,000/=). Kati ya
hizo, Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Moja Hamsini na Tano na Laki Mbili (Tshs.
2,155,200,000/=) ni kwa ajili ya mishahara, michango ya Mfuko wa Hifadhi ya
Jamii na maposho maalum kwa
wafanyakazi; Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Nne Thamanini na Tano na Laki Nane (Tshs. 1,485,800,000/=) ni kwa
matumizi mengineyo; Shilingi Bilioni Moja, Milioni Mia Tano na Elfu Ishirini na Nne (Tshs. 1,524,000,000/=) ni kwa
kazi za Maendeleo na Shilingi Bilioni Mbili, Milioni Mia Nne na Tano, Laki Sita
na Elfu Sabiini (Tshs. 2,405,670,000/=) ni fedha zilizoahadiwa kutolewa na
Washirika wa Maendeleo (Angalia Kiambatanisho Namb. 16). Pia naomba idhini ya kukusanya mapato ya Shilingi Milioni Kumi (Tshs.
10,000,000/=) kupitia usajili na ukaguzi wa vyama vya ushirika kwa mwaka
2014/2015.
72.
Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja.
Ahsanteni
No comments:
Post a Comment