Habari za Punde

Ofisi za ACT zavunjwa

Na Joseph Ngilisho, Arusha
OFISI za Chama Cha Mabadiliko na Uwazi (ACT) mkoani Arusha,zimevamiwa na watu wasiojulikana  usiku wa kuamkia jana na kuzuvunja, kisha kuiba fedha taslimu shilingi 280,000 na nyaraka muhimu za chama hicho.

Akizungumza na vyombo vya habari ofisi kwake, Katibu wa ACT mkoa wa Arusha, Matokeo Simba, alisema tukio hilo limefanyika majira ya usiku na wanahisi watu hao ni wafuasi wa Chadema.

Alisema katika nyaraka zilizoibwa ni pamoja na kadi 10 zilizokuwa za wanachama wa chama hicho.

Alisema iwapo isingekuwa watu hao kuwa ni wafuasi wa Chadema wasingeiba kadi hizo, kwakua zilikua na mzozo kutoka kwa viongozi wa Chadema baada ya wanachama hao pamoja na Mwenyekiti huyo kutangaza kukihama Chadema ambapo waliwataka warejeshe kadi hizo.

“Hivi kama sio wao inawezekanaje watu wavunje ofisi yetu halafu waibe pia kadi hizo zilizokuwa za wanachama wao, si wangeiba tu nyaraka nyingine,” alihoji.

Alitaja nyaraka nyingine zilizoibwa kuwa ni hati ya uhakiki wa wanachama kutoka kwa Msajili wa vyama vya siasa,jambo ambalo linaonesha lina lengo la kupoteza ushahidi wa uhakiki huo.

Alisema mbali na hati hiyo pia watu hao waliiba kadi tupu za uanachama pamoja na bendera jambo ambalo pia alilielezea kuwa lina lengo la kufanya hujuma katika mikutano ya hadhara, kwa kuwapandikiza watu ili waoneshe wanarejesha kadi na kujiunga na vyama vingine.


Alisema fedha hizo shilingi 280,000 zilizoibwa zilikua ni za michango kutoka kwa wanachama, ada za uanachama  na mauzo ya kadi za chama ambazo zilikua ofisini hapo kwa ajili ya shughuli za chama.

Alisema waligundua tukio hilo saa 2:00 asubuhi wakati walipokua wakifungua ofisi ambapo walikuta mlango wa mbao na wa chuma uko wazi na ndipo walipotoa taarifa polisi ambapo walipatiwa namba AR/RB/12473/2014 na kuahidiwa kufanyika upelelezi.

Akijibu tuhuma hizo, Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Arusha, Aman Golugwa, alisema kamwe viongozi na wafuasi wa chama chake hawawezi kufanya kitendo hicho kwa kuwa viongozi waliokihama chama chao hawana shida nao.


Alisema chama chake kwa sasa hakina muda wa kuhangaika kutafuta wanachama bali kinachofanya ni kutafuta wapiga kura kwa ajili ya chaguzi zijazo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.