Habari za Punde

Wapuuzeni Madiwani vigeugeu’

Na Kadama Malunde,Shinyanga
Mwenyekiti CCM mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja, aliwataka wananchi katika manispaa ya Shinyanga,kuwapuuza waliokuwa madiwani wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA),waliohamia CCM na baada ya miezi sita kurudi tena Chadema.

Alisema hayo wakati akizungumza kwenye mikutano ya hadhara iliyofanyika siku mbili katika kata ya Masekelo na Ngokolo mjini humo.

Kata hizo zilikuwa zikiongozwa na madiwani kutoka Chadema, Sebastian Peter na Zacharia Mfuko kabla ya kujiuzulu na kuhamia CCM kabla ya kurejea tena CHADEMA.

Alisema kutokana na madiwani hao kukosa nidhamu ya kisiasa, wananchi wanapaswa kuwapuuiza.

Alisema shutuma zilizotolewa na madiwani hao ni za uchonganishi zinazolenga kusababisha uvunjifu wa amani.

“Nawataka wananchi wa manispaa ya Shinyanga na taifa kwa ujumla kuwapuuza madiwani wa Chadema, waliohamia CCM na kurudi tena Chadema, huku wakitoa kashfa zenye shutuma za mauaji kwenye mikutano ya hadhara,maneno ambayo ni ya kichonganishi na kutaka kuvuruga amani ya Tanzania,” alisema.

“Kipindi madiwani hao walipokuwa wakihamia CCM, walitoa shutuma za mauji, kuwa viongozi wa Chadema taifa ndio waliomuua Philip Magadula SheLembi, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Shinyanga ,kutokana na kutaka madaraka ya ngazi ya juu,” alisema.


“Na waliporudi tena Chadema, wakatoa shutuma za mauaji, kuwa viongozi wa CCM wakiongozwa na Mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Steven Masele,  waliwapa pesa madiwani hao kwa ajili ya kuitungua ndege ya Dk. Wilbroad Slaa mjini Shinyanga, hamuoni maneno hayo kama ni uchonganishi,”alihoji.

Akijibu shutuma hizo, Mbunge  wa Shinyanga mjini, Steven Masele, alikanusha na kusema hazina ukweli wowote na kwamba  ni propaganda za kisiasa, zenye uchonganishi za kukosa sera za kuwaambia wananchi nini sababu za kuhama kwenye chama chao na kwenda kingine.

Naye Mbunge wa jimbo la Kishapu,Suleimani Nchambi, alisema madiwani hao walikuwa wanasumbuliwa na njaa, huku akiwataka wananchi kuepukana na watu wanaofanya siasa kama biashara.


Madiwani hao walijiuzulu nyazifa zao Februari 25, na Februari 26  wakapokelewa rasmi na kujiunga na CCM, mbele ya Katibu wa Itikadi, Siasa na Uenezi CCM Taifa , Nape Nauye  na Julai 30 mwaka huu wakabwaga manyanga na kurudi tena Chadema.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.