Habari za Punde

Kilango, Dk. Kadeghe watunishiana misuli

Na Kija Elias, Same
Mbunge wa Same Mashariki,Anne Kilango Malecela, amesema atapeleka malalamiko Sekretarieti ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma, kupinga hatua ya Mkuu wa wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya, Dk. Michael Kadeghe, kupeperusha bendera ya taifa kwenye gari lake akiwa wilaya ya Same ambayo haiongozi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kilango alisema atamshtaki Kadeghe kwa Mwenyekiti wa Baraza hilo, Jaji Mstaafu, Hamis Msumi kutafuta haki kwa kuwa kufanya hivyo ni kukiuka sheria na taratibu za nchini.

Mgogoro huo ulianza wiki iliyopita baada ya Kilango na Dk. Kadeghe kuingia kwenye mtafaruku jimboni huo.

Wakati Kilango akikagua barabara zinazojengwa kwa ahadi ya Rais Jakaya Kikwete alikutana ana kwa ana na Mkuu huyo wa wilaya akipeperusha bendera kwenye gari lake na kuanza kurushiana maneno.

Kilango anadai kwamba, Dk. Kadeghe, akiwa na gari lake lenye namba za usajili STK 3764 aina ya Land Cruiser, alifanya kosa hilo kwa minajili ya kuwatisha wananchi wa jimbo lake ili wamwamini anafaa kuwa mbunge wa jimbo hilo katika uchaguzi mkuu ujao, unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.


“Nitakutana na Mwenyekiti wa Sekretarieti ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma ili kutafuta haki. Haiwezekani wewe siyo DC wa Same upeperushe bendera kwenye wilaya ambayo huiongozi? huko ni kuwatisha wananchi lakini pia asitake abebwe,”alisema.

Alisema ingawa Kadeghe hana ubavu wa kumng’oa kwenye kiti chake, lakini pia hapaswi kumkejeli katika kipindi ambacho anatekeleza ilani ya uchaguzi ya chama chake, kuelekea uchaguzi mkuu na badala yake anatakiwa kuvuta subira hadi filimbi itakapopulizwa rasmi.

Mkuu huyo wa wilaya hiyo, alipotafutwa kutoa ufafanuzi wa madai ya Kilango, alisema hajawahi kufanya vikao vya siri vya chama kwa ajili ya kuendesha kampeni ya kumng’oa kwenye ubunge, lakini pia bendera hiyo ilikuwa ikifanyiwa usafi na wala haikuwa inapepea kama ambavyo inadaiwa.

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, Kilango alimshinda Dk. Kadeghe kwa kura 389 dhidi ya kura 46 alizoambulia kwenye uchaguzi wa ndani wa CCM na mwaka 2010, Kilango pia  alimpiga mwereka mpinzani wake huyo kwenye kura za maoni kwa kupata kura 7,900 dhidi ya kura 2,200 alizoambulia Kadeghe.


Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Same, Herman Kapufi alipotakiwa kutoa ufafanuzi kuhusu mgogoro huo, alisema taratibu zipo wazi kwamba Mkuu wa wilaya akishavuka nje ya mipaka yake ya utawala kwa mujibu wa madaraka ya ukuu wa wilaya chini ya sheria ya tawala za mikoa namba 19 ya mwaka 1977 na sheria ya serikali za mitaa namba 7 na 8 za mwaka 1982, Dk. Kadeghe amekosea  kupeperusha bendera kwenye wilaya ambayo si ya kwake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.