Habari za Punde

Mwakyembe awafyeka wezi TRL

Na Mwanajuma Abdi, DAR ES SALAAM
WAZIRI wa Uchukuzi Tanzania, Dk. Harrison Mwakyembe, amewafukuza kazi wafanyakazi sita wa Shirika la Reli (TRL) kwa wizi wa mafuta na fedha za tiketi za treni na kumuagiza Kamanda wa Polisi kuwakamata mara moja na kuwafikisha katika vyombo vya sheria.

Alitoa kauli hiyo jana, wakati alipokuwa akihutubia mkutano wa wafanyakazi wa TRL jijini hapa, ambapo alisema shirika hilo limekuwa likipata hasara kubwa kutokana na wizi wa mafuta uliokithiri na kuliibia fedga za mauzo ya  tiketi halali wanazotozwa abiria.

Watumishi wengine sita wamepewa barua za kusimamishwa kazi.
Aliwataja waliofukuzwa kazi na wanatakiwa wapelekwe rumande kwa ajili ya kupandishwa mahakamani ni pamoja na Stanley Makunja, Stanley Endrew, Jason Mosesn wa Tabora, B Looga, Edward Benedeto na Lucy Ntinga, ambae ni mwanamke pekee katika sakata hilo.

Alisema serikali haitavumilia wizi huo, ambao unafanyika kweupe ambao watu hao wanalisimamisha treni njiani kwa ajili ya kuiba mafuta, hivyo alitoa wito wa jeshi la polisi kuwafikisha mahakamani watuhumiwa hao.

Hata hivyo, aliuagiza uongozi wa TRL kuhakiki mali za wafanyakazi waliokufuzwa kazi na ikithibitika wana mali nyingi bila ya kuzitolea maelezo zipigwe mnada ili fedha zingizwe katika shirika hilo.

Alisema  mbali ya wizi wa mafuta lakini alidokeza mtindo wa uuzaji wa tiketi kihalali za treni kwa abiria zipo teketi zimeuzwa kwa shilingi 61,200 lakini katika risiti ya kopi inasomeka shilingi 16,800 zinazoingia TRL.

“Tiketi imeuzwa kwa shilingi 50,200 kwa mteja halali lakini TRL imeingia shilingi 13,600 na nyengine imeuzwa kwa shilingi 74,400 lakini katika kopi ya risiti ambayo fedha imeingia ni shilingi 13,600 na kuna tiketi imeuzwa kwa shilingi 57,600 lakini fedha iliyoingia shirika ni shilingi 6,700, jambo ambapo mchezo huu umechezwa kwa kipindi cha miaka mitano mpaka 10, na wanachukua robo tatu wa kile kinachoingizwa katika mapato ya serikali,” alisema.


Aidha alisema kamati ya wataalamu wanne iliyoundwa wakiwemo SUMATTA, TRL na Bodi ya wahandisi iongezwe watu wawili ili waweze kuchunguza mabehewa mapya yanayoanguka, sambamba na kwenda nchi India yanapotengenezwa kwa ajili ya kuangalia ubora wake, ambapo yakithibitika kuwa hayafai yazuiliwe huko yasiingie nchini.

Alifahamisha kuwa, mabehewa 125 ya kokoto yameingizwa na yanatarajiwa mengine 174 yataingizwa nchini , hivyo jopo la kamati hiyo lifike kuyakaguwa ubora wake kabla ya kuingia  Tanzania.

Hata hivyo, aliitaka Bodi ya Wakurugenzi na uongozi wa TRL kusitisha mikataba yote iliyoingia na kampuni nyengine ili kazi hizo zifanywe na wafanyakazi kwa ajili ya kuokoa fedha za umma zisitumike vibaya na kusababisha kujiendesha kwa hasara.


Mapema Katibu Mkuu, Erasto John alisema mabehewa mapya ya treni yaliyoingizwa awamu ya kwanza ni mabovu yanavunjika kama muhogo lakini pia yaliyofuata nayo ni mabovu hayapo katika kiwango.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.