Habari za Punde

Dk Shein Awataka Wananchi Kuheshimu Sheria Wakati Wote.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
 Zanzibar                                                              6.10.2015
---
WANANCHI wa Zanzibar wametakiwa kuheshimu sheria za uchaguzi ziliopo kwa wakati wote hasa wakati huu wa Kampeni, siku ya kupiga kura, siku ya kutangaza matokeo pamoja na siku za baadae.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika uzinduzi wa jengo jipya la Wizara ya Katiba na Sheria lilioko Mazizini nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Dk. Shein aliendelea kuwasisitiza wananchi kuheshimu misingi ya Katiba na Sheria ziliopo na kuwaeleza kuwa Sheria za uchaguzi zipo na zinalindwa na Katiba ya Zanzibar.

Katika hotuba yake hiyo ya uzinduzi wa jengo jipya la Wizara ya Katiba na Sheria lililopewa jina la ‘Nyumba ya Sheria’, Dk. Shein aliwahakikishia wananchi wa Zanzibar kuwa Zanzibar itafanikiwa kufanya uchaguzi huru na wa haki.

Dk. Shein aliwataka wananchi daima wasikubali mifarakano ambayo ni chanzo cha kusababisha maafa kama wanavyoshuhudia hivi sasa katika mataifa mbali mbali duniani.

“Nachukua fursa hii leo kwa mara nyengine tena kusisitiza umuhimu wa mshikamano na umoja wetu..tutafanikiwa kufanya uchaguzi huru na wa haki”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa wananchi wanawajibu wa kushikamana ili kutekeleza wajibu wa kikatiba na kisheria wa kuwachagua viongozi wa kuongoza kila baada ya miaka mitano kwa mafanikio.


Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwaeleza wananchi historia ya katiba ya Zanzibar na kusema kuwa kabla ya kuja kwa wageni, Zanzibar ilikuwa na utawala wa wenyeji ambapo na sheria zilikuwepo na zilikuwa kwa ajili ya kuongoza na kusimamia mfumo wa maisha uliokuwepo wakati huo.

Alisema kuwa leo wananchi wa Zanzibar wamefanikiwa kwa kuwa na Katiba yao ambayo mwaka 2010 ilifanyiwa marekebisho ambayo yalileta Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye Muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

Alisema kuwa  katika mfumo wa utawala wa kidemokrasia duniani kote, Katiba ni kitu muhimu na cha lazima ambapo pia, ni kieleezo au nembo ya utawala na mamlaka ya nchi na kuwataka wananchi kuiheshimu na kuitii katika yao ya Zanzibar ambayo ni msingi wa utawala wao.

Licha ya hayo alieleza kuwa kuwa na Katiba tu peke yake haitoshi  kuwaletea nafuu watu  bali utekelezaji wa Katiba ndiyo jambo muhimu na kusisitiza kuwa utii wa Sheria ndio msingi wa maendeleo kwa nchi yoyote duniani.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa Wizara hiyo ina jukumu la kusimamia masuala yote ya katiba na Sheria katika kipindi hiki ambacho Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika Muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa.

Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa jengo hilo la ghorofa saba ni wazo la kimaendeleo kwa matumizi bora ya ardhi na utekelezji kwa vitendo wa Mipango Miji iliyopitishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi karibuni.

Alisema kuwa katika kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi, Serikali itaendelea kujenga majengo ya kisasa yanayopendeza na kuvutia sambamba a kuweka vifaa vya kufanyia kazi vinavyoendana na mabadiliko, pamoja na mahitaji ya wakati huu.

Nae Waziri wa Katiba na Sheria Abubakar Khamis Bakary alisema kuwa ni ukweli usiopingika kwamba jengo hilo limetatua changamoto kubwa ya ufinyu wa nafasi kwa wafanyakazi wa taasisi za Wizara hiyo pamoja na wananchi wanaopatiwa huduma na taasisi hizo.

Waziri Bakary alitoa shukurani kwa Dk. Shein kwa nia yake njema ya kuitakia mema Zanzibar kwa kudumisha amani na utulivu na kuongoza gurudumu la maendeleo ya wananchi wa Zanzibar.

Kwa mujibu wa maelezo ya Waziri Bakary harakati za mradi wa jengo hilo zilianza mwaka 2011 na mkataba wa ujenzi ulifungwa mwezi April 2012 ambapo kazi hiyo ilitarajiwa kuchukua kipindi cha miezi 18 hadi kukamilika kwake mwezi Novemba 2013 lakini kutokana na changamoto jengo lilihamiwa Jaulai 2015.

Alisema kuwa jengo hilo litaiwezesha Wizara hiyo pamoja na Idara zake saba kuimarisha  utunzaji wa kumbukumbu zake na kujenga mifumo ya kielektroniki itakayarahisisha na kuharakisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.

Jengo hilo limejengwa na Kampuni ya  China Railways JiangChang Engineering (CRJE) na Mshauri ni Kampuni ya The National Estate Development Company Ltd (NEDCO)  ambapo Mhandisi Mkaazi ni Bwana Ali Othman ambapo gharama za ujenzi wa  jengo hilo ni Tsh.Bilioni 8.3.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.