Habari za Punde

Dk Shein : Nichagueni tena tuendelee kushirikiana kuongeza kasi ya kuijenga Zanzibar

DK. SHEIN: NICHAGUENI TENA TUENDELEE KUSHIRIKIANA KWA KUONGEZA KASI YA KUIJENGA ZANZIBAR

Mgombea wa nafasi ya urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wananchi kumpa tena fursa ya kuongoza ili waendelee kushirikiana kuijenga Zanzibar.

Amesema katika kipindi cha miaka mitano kinachomalizika sasa Zanzibar imepiga hatua kubwa kimaendeleo kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM hivyo kumchagua tena yeye na chama chake kuongoza ni fursa nyingine kwa wananchi wa Zanzibar kuendeleza kasi ya maendeleo ya nchi yao.

Katika mkutano wa kampeni uliofanyika huko Paje katika jimbo la uchaguzi la Paje,Mkoa wa Kusini Unguja, mgombea huyo wa CCM aliueleza umati mkubwa wa wananchi ambao haujawahi kutokea kuwa ahadi alizozitoa kwa jimbo hilo katika mkutano wa kampeni kama huo mwaka 2010 zimetekelezwa na kuahidi kuongeza kasi ya utekelezaji wa Ilani mpya ya chama hicho ya mwaka 2015-2020.

“Tumetekeleza Ilani yetu kama tulivyopanga katika sekta ya afya, elimu, maji, umeme na sekta ya utalii”na kuongeza kuwa kwa sekta ya barabara utekelezaji umeanza na utakamilishwa katika kipindi kijacho.

Alifafanua kuwa baada ya kukamilisha kuifanya hospitali ya Makunduchi kuwa ya wilaya, Serikali itaendelea kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo kwa kuiimarisha hospitali ya Kivunge na kituo cha afya cha Paje kwa kivipatia vifaa na wataalamu wa afya.

“Kazi ya kuipandisha hospitali ya Makunduchi kuwa ya wilaya imekamilika kwa kuiwekea vifaa vipya na kuwapatia madaktari wakiwemo kutoka nje ya nchi na tunatarajia kuongeza majengo mengine mapya kuiwezesha hospitali hiyo kuwahudumia watu wengi zaidi” alieleza Dk. Shein na kuongeza kuwa hivi sasa hata wananchi wa mjini wanafika katika hospitali hiyo kufuata huduma.


Aliongeza kuwa Serikali hivi karibuni ilifungua kituo kipya cha afya huko Kajengwa Makunduchi ikiwa ni sehemu utekelezaji wa mpango wa Serikali wa uimarishaji wa huduma za afya nchini.

Dk. Shein aliwaeleza wananchi hao kuwa katika kipindi kijacho Serikali itajenga dakhalia katika skuli ya sekondari Paje Mtule ambayo ni skuli mpya ya kisasa ambayo imejengwa ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya mwaka 2010 -2015 ya kuimarisha elimu nchini.

Katika kuendelea kuimarisha elimu, Dk. Shein ameahidi katika kipindi cha miaka mitano ijayo kuzipatia skuli zote za sekondari kompyuta ili ziweze kwenda na mabadiliko ya sayansi na tekinolojia.

Kuhusu ahadi ya kusambaza umeme vijijini, Dk. Shein alieleza kuwa  utekelezaji wake umezidi asilimia mia na kwa upande wa Paje ni maeneo machache yaliyobaki na kuahidi kukamilishwa muda mfupi ujao baada Shirika la Umeme 
Zanzibar (ZECO) kwa kuweka transfoma mpya.


Mgombea huyo wa CCM anatarajiwa kwenda Pemba kuendelea na kampeni zake kesho.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.